Zaburi 74

Zaburi 74

Zaburi 74

Maombi kwa ajili ya taifa

1Ee Mungu, mbona umetukataa milele?

Mbona hasira yako inatoka moshi

juu ya kondoo wa malisho yako?

2Kumbuka watu uliowanunua zamani,

kabila la urithi wako, ambao uliwakomboa:

Mlima Sayuni, ambamo uliishi.

3Geuza hatua zako kuelekea magofu haya ya kudumu,

uharibifu wote huu ambao adui ameuleta pale patakatifu.

4Adui zako wamenguruma pale ulipokutana nasi,

wanaweka bendera zao kama alama.

5Walifanya kama watu wanaotumia mashoka

kukata kichaka cha miti.

6Walivunjavunja milango yote iliyonakshiwa

kwa mashoka na vishoka vyao.

7Waliteketeza kabisa mahali pako patakatifu,

wakayanajisi makao ya Jina lako.

8Walisema mioyoni mwao,

“Tutawaponda kabisa!”

Walichoma kila mahali Mungu

alipoabudiwa katika nchi.

9Hatukupewa ishara za miujiza;

hakuna manabii waliobaki,

hakuna yeyote kati yetu ajuaye

hali hii itachukua muda gani.

10Ee Mungu, mtesi atakudhihaki hadi lini?

Je, adui watalitukana jina lako milele?

11Kwa nini unazuia mkono wako,

mkono wako wa kuume?

Uutoe kutoka makunjo ya vazi lako

na uwaangamize!

12Lakini wewe, Ee Mungu, ni mfalme wangu tangu zamani,

unaleta wokovu duniani.

13Ni wewe uliyeigawanya bahari kwa uweza wako;

ulivunja vichwa vya mnyama mkubwa wa baharini.

14Ni wewe uliyeponda vichwa vya Lewiathani,[#74:14 Lewiathani ni mnyama mkubwa wa baharini mwenye magamba anayefanana na joka kubwa, mwenye umbo la kutisha, asiyeweza kuvuliwa.]

nawe ukamtoa kama chakula kwa viumbe vya jangwani.

15Ni wewe uliyefungua chemchemi na vijito,

ulikausha mito iliyokuwa ikitiririka daima.

16Mchana ni wako, na usiku ni wako pia;

uliziweka jua na mwezi.

17Ni wewe uliyeiweka mipaka yote ya dunia,

ulifanya kiangazi na masika.

18Ee Bwana , kumbuka jinsi mtesi alivyokudhihaki,

jinsi watu wapumbavu walivyolitukana jina lako.

19Usiukabidhi uhai wa njiwa wako kwa wanyama mwitu;

usisahau kabisa uhai wa watu wako wanaoteseka milele.

20Likumbuke agano lako,

maana mara kwa mara mambo ya jeuri

yamejaa katika sehemu za giza nchini.

21Usiruhusu waliodhulumiwa warudi nyuma kwa aibu;

maskini na wahitaji hebu walisifu jina lako.

22Inuka, Ee Mungu, ujitetee;

kumbuka jinsi wapumbavu

wanavyokudhihaki mchana kutwa.

23Usipuuze makelele ya watesi wako,

ghasia za adui zako, zinazoinuka mfululizo.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.