Zaburi 77

Zaburi 77

Zaburi 77

Matendo makuu ya Mungu yanakumbukwa

1Nilimlilia Mungu ili anisaidie,

nilimlilia Mungu ili anisikie.

2Nilipokuwa katika taabu, nilimtafuta Bwana,

usiku nilinyoosha mikono bila kuchoka

na nafsi yangu ilikataa kufarijika.

3Ee Mungu, nilikukumbuka wewe, nikalia kwa huzuni;

nikatafakari, roho yangu ikadhoofika.

4Ulizuia macho yangu kufumba;

nilikuwa nasumbuka, nikashindwa kusema.

5Nilitafakari kuhusu siku zilizopita,

miaka mingi iliyopita,

6nilikumbuka nilivyoimba nyimbo usiku.

Moyo wangu ulitafakari

na roho yangu ikauliza:

7“Je, Bwana atakataa milele?

Je, hatatenda mema tena?

8Je, upendo wake usio na mwisho umetoweka milele?

Je, ahadi yake imekoma nyakati zote?

9Je, Mungu amesahau kuwa na huruma?

Je, katika hasira amezuia fadhili zake?”

10Ndipo nikawaza, “Huu ndio udhaifu wangu:

lakini nitakumbuka

miaka ya mkono wa kuume

wa Aliye Juu Sana.”

11Nitayakumbuka matendo ya Bwana ;

naam, nitaikumbuka miujiza yako ya zamani.

12Nitazitafakari kazi zako zote

na kuyawaza matendo yako makuu.

13Ee Mungu, njia zako ni takatifu.

Ni mungu yupi aliye mkuu kama Mungu wetu?

14Wewe ndiwe Mungu utendaye miujiza,

umeonesha uwezo wako kati ya mataifa.

15Kwa mkono wako wenye nguvu umewakomboa watu wako,

uzao wa Yakobo na Yusufu.

16Maji yalikuona, Ee Mungu,

maji yalikuona yakakimbia,

vilindi vilitetemeka.

17Mawingu yalimwaga maji,

mbingu zikatoa ngurumo kwa radi;

mishale yako ilimetameta huku na huko.

18Ngurumo yako ilisikika katika upepo wa kisulisuli,

umeme wako wa radi ukaangaza dunia,

nchi ikatetemeka na kutikisika.

19Njia yako ilipita baharini,

mapito yako kwenye maji makuu,

ingawa nyayo zako hazikuonekana.

20Uliongoza watu wako kama kundi

kwa mkono wa Musa na Haruni.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.