Zaburi 97

Zaburi 97

Zaburi 97

Mungu Mtawala mkuu

1Bwana anatawala, nchi na ifurahi,

visiwa vyote vishangilie.

2Mawingu na giza nene vinamzunguka,

haki na hukumu ndio msingi wa kiti chake cha enzi.

3Moto hutangulia mbele zake

na huteketeza adui zake pande zote.

4Umeme wake wa radi humulika dunia,

nchi huona na kutetemeka.

5Milima huyeyuka kama nta mbele za Bwana ,

mbele za Bwana wa dunia yote.

6Mbingu zinatangaza haki yake,

na mataifa yote huona utukufu wake.

7Wote waabuduo sanamu waaibishwa,

wale wajisifiao sanamu:

mwabuduni yeye, enyi miungu yote!

8Sayuni husikia na kushangilia,

vijiji vya Yuda vinafurahi

kwa sababu ya hukumu zako, Ee Bwana .

9Kwa kuwa wewe, Ee Bwana , ndiwe Uliye Juu Sana kuliko dunia yote;

umetukuka sana juu ya miungu yote.

10Wale wanaompenda Bwana na wauchukie uovu,

kwa maana yeye hulinda maisha ya waaminifu wake

na kuwaokoa kutoka mkononi mwa mwovu.

11Nuru huangaza wenye haki

na furaha kwa watu wanyofu wa moyo.

12Furahini katika Bwana , enyi wenye haki,

lisifuni jina lake takatifu.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.