Warumi 15

Warumi 15

Usijipendeze mwenyewe tu

1Sisi tulio na nguvu, hatuna budi kuchukuliana na kushindwa kwa wale walio dhaifu wala si kujipendeza nafsi zetu wenyewe.

2Kila mmoja wetu inampasa kumpendeza jirani yake kwa mambo mema, ili kumjenga katika imani.

3Kwa maana hata Kristo hakujipendeza mwenyewe, bali kama ilivyoandikwa: “Matukano yao wale wanaokutukana wewe yalinipata mimi.”[#15:3 Za 69:9]

4Kwa maana kila kitu kilichoandikwa zamani, kiliandikwa kutufundisha, ili kwa saburi na faraja tunayopata katika Maandiko tuwe na tumaini.

5Mungu atoaye saburi na faraja awajalie ninyi roho ya umoja miongoni mwenu mnapomfuata Kristo Yesu,

6ili kwa moyo mmoja mpate kumtukuza Mungu aliye Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo.

Injili sawa kwa Wayahudi na kwa watu wa Mataifa

7Karibishaneni ninyi kwa ninyi kama Kristo alivyowakaribisha ninyi ili kumletea Mungu utukufu.

8Kwa maana nawaambia kwamba Kristo amekuwa mtumishi kwa wale waliotahiriwa ili kuonesha kweli ya Mungu, na kuthibitisha zile ahadi walizopewa baba zetu wa zamani,

9na pia ili watu wa Mataifa wamtukuze Mungu kwa rehema zake. Kama ilivyoandikwa:

“Kwa hiyo nitakutukuza kati ya watu wa Mataifa;

nitaliimbia sifa jina lako.”

10Tena yasema,

“Enyi watu wa Mataifa, furahini

pamoja na watu wa Mungu.”

11Tena,

“Msifuni Bwana, ninyi watu wa Mataifa wote,

na kumwimbia sifa, enyi watu wote.”

12Tena Isaya anasema,

“Shina la Yese litachipuka,

yeye atakayeinuka ili kuyatawala mataifa.

Watu wa Mataifa watamtumaini.”

13Mungu wa tumaini awajaze ninyi furaha yote na amani katika kumwamini, ili mpate kujawa na tumaini tele kwa nguvu ya Roho Mtakatifu.

Paulo mhudumu wa watu wa Mataifa

14Ndugu zangu, mimi mwenyewe ninasadiki kwamba mmejaa wema, mkijazwa ufahamu wote na mnaweza kufundishana ninyi kwa ninyi.

15Hata hivyo, nimewaandikia kwa ujasiri vipengele kadha wa kadha katika waraka huu ili kuwakumbusha tena kuvihusu, kutokana na ile neema Mungu aliyonipa

16niwe mhudumu wa Kristo Yesu kwa watu wa Mataifa. Alinipa huduma ya kikuhani ya kutangaza Injili ya Mungu, ili watu wa Mataifa wapate kuwa dhabihu inayokubalika na Mungu, kwa kutakaswa na Roho Mtakatifu.

17Kwa hiyo ninajisifu katika Kristo Yesu, kwenye utumishi wangu kwa Mungu.

18Kwa maana sitathubutu kusema kitu chochote zaidi ya kile ambacho Kristo amefanya kwa kunitumia mimi katika kuwaongoza watu wa Mataifa wamtii Mungu kwa yale niliyosema na kufanya,

19kwa nguvu za ishara na miujiza, kwa uweza wa Roho wa Mungu, hivyo kuanzia Yerusalemu hadi maeneo yote ya kandokando yake hadi Iliriko, nimekwisha kuihubiri Injili ya Kristo kwa ukamilifu.

20Hivyo imekuwa nia yangu kuhubiri Habari Njema pale ambapo Kristo hajajulikana, ili nisije nikajenga juu ya msingi wa mtu mwingine.

21Lakini kama ilivyoandikwa:

“Wale ambao hawajahubiriwa habari zake wataona,

nao wale ambao hawajazisikia watafahamu.”

22Hii ndiyo sababu nimezuiliwa mara nyingi nisiweze kuja kwenu.

Paulo apanga kwenda Rumi

23Lakini sasa kwa kuwa hakuna nafasi zaidi kwa ajili yangu katika sehemu hii, ninatamani kuja kwenu kama ambavyo nimekuwa na shauku kwa miaka mingi.

24Nimekusudia kufanya hivyo nitakapokuwa njiani kwenda Hispania. Natarajia kuwaona katika safari yangu na kusafirishwa nanyi hadi huko, baada ya kufurahia ushirika wenu kwa kitambo kidogo.

25Ila sasa niko njiani kuelekea Yerusalemu kwa ajili ya kuwahudumia watakatifu huko.

26Kwa kuwa imewapendeza watu wa Makedonia na Akaya kufanya changizo kwa ajili ya maskini walio miongoni mwa watakatifu huko Yerusalemu.

27Imewapendeza kufanya hivyo, naam, kwani ni wadeni wao. Kwa maana ikiwa watu wa Mataifa wameshiriki baraka za rohoni za Wayahudi, wao ni wadeni wa Wayahudi, ili Wayahudi nao washiriki baraka zao za mambo ya mwilini.

28Kwa hiyo baada ya kukamilisha kazi hii na kuhakikisha kuwa wamepokea kila kitu kilichokusanywa, nitapitia kwenu nikiwa njiani kwenda Hispania.

29Ninajua kwamba nitakapokuja kwenu, nitakuja na wingi wa baraka za Kristo.

30Basi, ndugu zangu, nawasihi kwa Jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa upendo wa Roho Mtakatifu, kujiunga nami katika taabu zangu mkiniombea kwa Mungu.

31Ombeni ili nipate kuokolewa mikononi mwa wale wasioamini walio Yudea, na kwamba utumishi wangu upate kukubaliwa na watakatifu wa huko Yerusalemu,

32ili kwa mapenzi ya Mungu niweze kuja kwenu kwa furaha, nami niburudishwe pamoja nanyi.

33Mungu wa amani na awe pamoja nanyi nyote. Amen.

Neno: Biblia Takatifu™ Neno™ Hakimiliki © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 na Biblica, Inc. Imetumiwa kwa ruhusa. Haki zote zimehifadhiwa duniani kote. Kiswahili Contemporary Version™ Copyright © 1984, 1989, 2009, 2015, 2025 by Biblica, Inc. Used with permission. All rights reserved worldwide.
Published by: Biblica, Inc.