The chat will start when you send the first message.
1Laiti ungekuwa kwangu kama ndugu wa kiume,
ambaye aliyanyonya matiti ya mama yangu!
Kisha, kama ningekukuta huko nje,
ningekubusu,
wala hakuna mtu yeyote angenidharau.
2Ningekuongoza na kukuleta
katika nyumba ya mama yangu,
yeye ambaye amenifundisha.
Ningekupa divai iliyokolezwa unywe,
asali ya maua ya mikomamanga yangu.
3Mkono wake wa kushoto uko chini ya kichwa changu,
na mkono wake wa kuume unanikumbatia.
4Binti za Yerusalemu, ninawaagiza:
msichochee wala kuamsha mapenzi
hata yatakapotaka yenyewe.
5Ni nani huyu anayekuja kutoka nyikani
akimwegemea mpenzi wake?
Nilikuamsha chini ya mtofaa,
huko mama yako alipotunga mimba yako,
huko yeye alipata uchungu akakuzaa.
6Nitie kama muhuri moyoni mwako,
kama muhuri kwenye mkono wako;
kwa maana upendo una nguvu kama mauti,
wivu wake ni mkatili kama Kuzimu.
Unachoma kama mwali wa moto,
kama mwali mkubwa wa moto wa Bwana hasa.
7Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo,
mito haiwezi kuugharikisha.
Kama mtu angetoa mali yote ya nyumbani mwake
kwa ajili ya upendo,
angedharauliwa kabisa.
8Tunaye dada mdogo,
matiti yake hayajakua bado.
Tutafanya nini kwa ajili ya dada yetu
wakati atakapokuja kuposwa?
9Kama yeye ni ukuta,
tutajenga minara ya fedha juu yake.
Na kama yeye ni mlango,
tutamzungushia mbao za mwerezi.
10Mimi ni ukuta,
nayo matiti yangu ni kama minara.
Ndivyo ambavyo nimekuwa machoni pake
kama yule anayeleta utoshelevu.
11Sulemani alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-Hamoni;
alikodisha shamba lake la mizabibu kwa wapangaji.
Kila mmoja angeleta kwa ajili ya matunda yake
shekeli elfu moja za fedha.
12Lakini shamba langu la mizabibu
ambalo ni langu mwenyewe
ni langu kutoa;
hizo shekeli elfu moja ni kwa ajili yako, ee Sulemani,
na shekeli mia mbili ni kwa ajili
ya wale wanaotunza matunda yake.
13Wewe ukaaye bustanini
pamoja na rafiki mliohudhuria,
hebu nisikie sauti yako!
14Njoo, mpenzi wangu,
uwe kama paa
au kama ayala mchanga
juu ya milima iliyojaa manukato.