2Timotheo 3

2Timotheo 3

Uovu katika siku za mwisho

1Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.[#1 Tim 4:1]

2Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,[#Rum 1:29]

3wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema,

4wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu;[#Flp 3:19]

5walio na utaua kwa nje, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.[#Mt 7:15,21; Rum 2:20; Tit 1:16]

6Kwa maana katika hao wamo wale wajiingizao katika nyumba za watu, na kuchukua mateka wanawake wajinga wenye mizigo ya dhambi, waliochukuliwa na tamaa za kila namna;[#Mt 23:14; Tit 1:11]

7wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.[#2 Tim 2:25]

8Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani.[#Kut 7:11,22; 1 Tim 6:5; 1:12]

9Lakini hawataendelea sana; maana upumbavu wao utakuwa dhahiri kwa watu wote, kama vile na upumbavu wa hao ulivyokuwa dhahiri.

Mausia ya Paulo kwa Timotheo

10Bali wewe umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu,

11na upendo, na subira; tena na adha zangu na mateso, mambo yaliyonipata katika Antiokia, katika Ikonio, na katika Listra, kila namna ya adha niliyoistahimili, naye Bwana aliniokoa katika hayo yote.[#Mdo 13:14-52; 14:1-20; Zab 34:19]

12Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.[#Mt 16:24; Mdo 14:22]

13Lakini watu waovu na wadanganyaji wataendelea, na kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika.[#1 Tim 4:1]

14Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao;[#2 Tim 2:2]

15na ya kuwa tangu utotoni umeyajua Maandiko Matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.[#Yn 5:39; Zab 119:99]

16Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki;[#2 Pet 1:19-21; Rum 15:4]

17ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.[#1 Tim 6:11]

The Holy Bible in Kiswahili, Revised Union Version © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 2013. 
Published by: Bible Society of Tanzania