The chat will start when you send the first message.
1Ikawa, Apolo alipokuwa Korintho, Paulo, akiisha kupita kati ya nchi za juu, akafika Efeso; akakutana na wanafunzi kadhaa huko;
2akawauliza, Je! Mlipokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu hatukusikia.[#Mdo 2:38]
3Akawauliza, Basi mlibatizwa kwa ubatizo gani? Wakasema, Kwa ubatizo wa Yohana.
4Paulo akasema, Yohana alibatiza kwa ubatizo wa toba, akiwaambia watu wamwamini yeye atakayekuja nyuma yake, yaani, Yesu.[#Mt 3:11; Mk 1:4,7-8; Lk 3:4,16; Yn 1:26-27]
5Waliposikia haya wakabatizwa kwa jina la Bwana Yesu.
6Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.[#Mdo 8:17; 10:44,46]
7Na idadi yao ilikuwa kama wanaume kumi na wawili.
8Akaingia ndani ya sinagogi, akanena kwa ushujaa kwa muda wa miezi mitatu, akihojiana na watu, na kuwavuta katika mambo ya ufalme wa Mungu.
9Lakini wengine walikaidi, wakakataa kuamini, wakiitukana ile Njia mbele ya mkutano; basi, akaondoka akawaacha, akawatenga wanafunzi, akahojiana na watu kila siku katika darasa la mtu mmoja, jina lake Tirano.[#2 Tim 1:15; Mdo 9:2; Tit 3:10,11; 2 Kor 6:17; 2 Yoh 1:10]
10Mambo haya yakaendelea kwa muda wa miaka miwili, hata wote waliokaa Asia wakalisikia neno la Bwana, Wayahudi kwa Wagiriki.
11Mungu akafanya kwa mikono ya Paulo miujiza ya kupita kawaida;[#Mdo 14:3]
12hata wagonjwa wakaletewa leso na nguo zilizotoka mwilini mwake, magonjwa yao yakawatoka, pepo wachafu wakawatoka.[#Mdo 5:15]
13Baadhi ya Wayahudi wenye kutangatanga, nao ni wapunga pepo, wakajaribu kutaja jina la Bwana Yesu juu yao waliopagawa na pepo wachafu, wakisema, Nawaapisha kwa Yesu, yule anayehubiriwa na Paulo.[#Lk 9:49]
14Walikuwapo wana saba wa mtu mmoja Skewa, Myahudi, kuhani mkuu, waliofanya hivyo.
15Yule pepo mchafu akawajibu, akawaambia, Yesu namjua na Paulo namfahamu, lakini ninyi ni nani?[#Mk 1:34; Lk 4:41]
16Na yule mtu aliyepagawa na pepo mchafu akawarukia wawili, akawaweza, akawashinda, hata wakatoka mbio katika nyumba ile wakiwa uchi na kujeruhiwa.
17Habari hii ikajulikana na Wayahudi wote na Wagiriki waliokaa Efeso, hofu ikawaingia wote, na jina la Bwana Yesu likatukuzwa.[#Mdo 5:5,11]
18Na wengi wa wale walioamini wakaja wakaungama, wakidhihirisha matendo yao.
19Na watu wengi katika wale waliotumia mambo ya uganga wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha elfu hamsini.[#19:19 Yapata kama shilingi 34,000.]
20Hivyo ndivyo neno la Bwana lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.[#Mdo 6:7; 12:24]
21Mambo hayo yalipokwisha kumalizika, Paulo akaazimu rohoni mwake, akiisha kupita katika Makedonia na Akaya, aende Yerusalemu, akisema, Baada ya kuwako huko, yanipasa kuuona na Rumi pia.[#Mdo 23:11; Rum 1:13]
22Akatuma watu wawili miongoni mwa wale waliomtumikia kwenda Makedonia, nao ni Timotheo na Erasto, yeye mwenyewe akakaa katika Asia kwa muda.[#Mdo 17:14; Rum 16:23; 1 Kor 4:17]
23Wakati huo kukatokea ghasia si haba kuhusu Njia ile.[#Mdo 19:9; 2 Kor 1:8,9]
24Kwa maana mtu mmoja, jina lake Demetrio, mfua fedha, aliyekuwa akifanya vihekalu vya fedha vya Artemi, alikuwa akiwapatia mafundi faida nyingi.[#Mdo 16:16]
25Akawakusanya hao, pamoja na wengine wenye kazi ile ile, akasema, Enyi wanaume, mnajua ya kuwa utajiri wetu hutoka katika kazi hii.
26Tena mnaona na kusikia ya kwamba si katika Efeso tu, bali katika Asia yote pia Paulo huyo ameshawishi watu wengi na kuwageuza nia zao, akisema ya kwamba hiyo inayofanywa kwa mikono siyo miungu.[#Mdo 17:29]
27Si kwamba kazi hii yetu ina hatari ya kudharauliwa tu; bali na hekalu la mungu mke aliye mkuu, Artemi, kuhesabiwa si kitu, na kuondolewa utukufu wake, ambaye Asia yote pia na walimwengu wote humwabudu.
28Waliposikia haya wakajaa ghadhabu, wakapiga kelele, wakisema, Artemi wa Waefeso ni mkuu.
29Mji wote ukajaa ghasia, wakaenda mbio wakaingia ukumbi wa michezo kwa pamoja, wakiisha kuwakamata Gayo na Aristarko, watu wa Makedonia waliosafiri pamoja na Paulo.[#Mdo 20:4]
30Na Paulo alipotaka kuingia kati ya watu, wanafunzi hawakumwacha aingie.
31Na baadhi ya wakuu wa Asia, walio rafiki zake, wakatuma watu kwake, wakimsihi asiingie ndani katika ukumbi wa michezo.
32Basi wengine walikuwa wakilia hivi na wengine hivi; kwa maana ule mkutano ulikuwa umechafukachafuka, na wengi wao hawakuijua sababu ya kukusanyika kwao pamoja.
33Wakamtoa Iskanda katika mkutano, Wayahudi wakimweka mbele ya watu. Iskanda akawapungia mkono, akitaka kujitetea mbele ya wale watu.
34Lakini walipotambua ya kuwa yeye ni Myahudi, wakapiga kelele wote pia kwa sauti moja kwa muda wa kama saa mbili, wakisema, Artemi wa Waefeso ni mkuu.
35Na karani wa mji alipokwisha kuwatuliza watu, akasema, Enyi wanaume wa Efeso, ni mtu gani asiyejua ya kuwa mji wa Efeso ni mtunzaji wa hekalu la Artemi, aliye mkuu, na wa kitu kile kilichoanguka kutoka mbinguni?
36Basi kwa kuwa mambo haya hayawezi kukanushwa, imewapasa kutulia; msifanye neno la haraka haraka.
37Kwa maana mmewaleta watu hawa, wasioiba vitu vya hekalu wala kumtukana mungu mke wetu.
38Basi ikiwa Demetrio na mafundi walio pamoja naye wana neno juu ya mtu yeyote, baraza ziko, na watawala wako; na washitakiane.
39Ikiwa kuna mambo mengine yoyote mnayotaka kujua, ni sharti yasuluhishwe katika kusanyiko lililo halali.
40Kwa maana tuna hatari ya kushitakiwa kwa ajili ya ghasia hizi za leo, ambazo hazina sababu; maana hakuna sababu tunayoweza kutoa kama chanzo cha ghasia hizi.
41Alipokwisha kusema haya akauvunja mkutano.