Ayubu 29

Ayubu 29

Ayubu amalizia hoja zake

1Kisha Ayubu akaendelea na hoja yake, na kusema,

2Laiti ningekuwa kama nilivyokuwa katika miezi ya zamani,

Kama katika siku hizo Mungu aliponilinda;

3Hapo taa yake ilipomulika juu yangu kichwani,[#Ayu 18:6; Zab 18:28]

Nami nilitembea gizani kwa njia ya mwanga wake;

4Kama nilivyokuwa katika siku zangu za kukomaa,[#Zab 25:14; Mit 3:32]

Hapo siri ya Mungu ilipokuwa hemani mwangu;

5Wakati Mwenyezi alipokuwa angali pamoja nami,

Nao watoto wangu walipokuwa wakinizunguka;

6Wakati hatua zangu zilipokuwa zikioshwa kwa siagi,[#Mwa 49:11; Kum 32:13; Zab 81:16]

Nalo jabali liliponimiminia mito ya mafuta!

7Wakati nilipotoka kwenda mjini, kupitia langoni,

Nilipokitengeneza kiti changu katika njia kuu,

8Hao vijana waliniona wakanipisha,

Nao wazee wakasimama kwa heshima;

9Wakuu wakanyamaza wasinene,

Na kuweka mikono yao vinywani mwao;

10Sauti yao wakuu ilinyamaa,[#Zab 137:6]

Na ndimi zao zilishikamana na makaakaa yao.

11Maana sikio liliponisikia, ndipo likanibarikia;

Na jicho liliponiona, likanishuhudia.

12Kwa sababu nilimwokoa maskini aliyenililia;[#Zab 72:12; Mit 21:13]

Yatima naye, na yule asiyekuwa na mtu wa kumsaidia.

13Baraka yake yeye aliyekuwa karibu na kupotea ilinijia;

Nikaufanya moyo wa mjane kuimba kwa furaha.

14Nilijivika haki, ikanifunika,[#Zab 132:9; Rum 13:14; Efe 6:14]

Adili yangu ilikuwa kama joho na kilemba.

15Nilikuwa macho kwa kipofu,[#Hes 10:31]

Nilikuwa miguu kwa aliyechechemea.

16Nilikuwa baba kwa mhitaji,[#Mit 29:7]

Na kesi ya mtu nisiyemjua niliichunguza.

17Nami nilizivunja taya za wasio haki,

Na kumpokonya mawindo katika meno yake.

18Ndipo niliposema, Nitakufa ndani ya kiota changu,[#Zab 30:6]

Nami nitaziongeza siku zangu kama mchanga;

19Shina langu limeenea hata kufika majini,[#Zab 1:3; Yer 17:8]

Na umande hukaa usiku kucha katika matawi yangu;

20Utukufu wangu utakuwa mpya kwangu,[#Mwa 49:24]

Na uta wangu hurejeshwa upya mkononi mwangu.

21Watu walitega masikio kunisikiliza, na kungoja,

Wakanyamaza kimya wapate kusikia mashauri yangu.

22Hawakunena tena baada ya kusikia maneno yangu;

Matamko yangu yakadondoka juu yao.

23Walikuwa wakiningojea kama kungojea mvua;

Wakafunua vinywa vyao sana kama mvua ya masika.

24Walipokata tamaa nikacheka nao;

Na mwanga wa uso wangu hawakuuangusha.

25Niliwachagulia njia, nikakaa kama mkuu wao.

Nikakaa kama mfalme katika jeshi la askari,

Mfano wa awafarijiye hao waombolezao.

The Holy Bible in Kiswahili, Revised Union Version © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 2013. 
Published by: Bible Society of Tanzania