2 Watesalonike 3

2 Watesalonike 3

Anawahimiza, wamwombee.

1Kisha, ndugu, mtuombee sisi kwa Mungu, Neno la Bwana liendelee na kutukuzwa vivyo hivyo kama kwenu![#Kol. 4:3.]

2Tena tuombeeni, tuokolewe mikononi mwa watu walio wapuzi na wabaya! Kwani sio wote wawezao kumtegemea Bwana.

3Lakini Bwana ni mwelekevu atakayewashupaza na kuwalinda, yule Mbaya asiwajie.[#1 Tes. 5:24.]

4Kwa ajili yenu tunamtumaini Bwana kwamba: Tunayowaagiza, mwayashika sasa, hata siku za nyuma mtayashika.[#2 Kor. 7:16; Gal. 5:10.]

5Bwana aiongoze mioyo yenu, iufikie upendo wa Mungu na uvumilivu wa Kristo!

Anawaonya wasiofanya kazi.

6*Ndugu, tunawaagiza ninyi, kwa nguvu ya Jina la Bwana Yesu Kristo, mtengane na kila ndugu anayeendelea na kufuata mambo yaliyo ya ovyoovyo tu, asiufuate ufundisho, mlioupata kwetu sisi.[#Mat. 18:15-17; Rom. 16:17.]

7Kwani mwajua wenyewe, jinsi inavyowapasa kutuiga, kwa sababu hatukukaa kwenu kiovyoovyo tu.[#1 Tes. 1:6.]

8Hakuna, ambaye tulikula chakula chake bure, ila tulijisumbua na kujiumiza tukifanya kazi usiku na mchana kwa kukataa kumlemea mtu ye yote wa kwenu.[#1 Kor. 4:12.]

9Hatukuvifanya hivyo kwamba: Hatu wakuu, ila tulitaka kuwapa ninyi vielezo, mpate kutuiga.[#Mat. 10:10; 1 Kor. 4:16.]

10Kwani tulipokuwa kwenu tuliwaagiza hata neno hili: Mtu asiyetaka kufanya kazi asipate chakula![#1 Mose 3:19; 2 Mose 20:9.]

11Kwani twasikia: Kwenu wako wanaoendelea na kufuata mambo yaliyo ya ovyoovyo tu, hawafanyi kazi, ila hufanya mapuzi.[#1 Tim. 1:6.]

12Walio hivyo tunawaagiza na kuwaonya machoni pake Bwana Yesu Kristo, watulie, wapate kufanya kazi na kula chakula chao wenyewe.[#1 Tes. 4:11.]

13Lakini ninyi, ndugu, msichoke kufanya yaliyo mazuri!*[#Gal. 6:9.]

14Lakini mtu asipoyatii maneno yetu yaliyomo humu baruani, huyo mjulisheni mkikataa kuchanganika naye, apatwe na soni![#2 Tes. 3:6; 1 Kor. 5:9,11.]

15Lakini msimwazie kuwa mchukivu, ila mwonyeni kindugu!

16Lakini yeye Bwana aliye mwenye utangemano awape kutengemana po pote katika mambo yote! Bwana awe nanyi nyote![#Yoh. 14:27.]

17Salamu hii naiandika kwa mkono wangu mimi Paulo; huu ndio mwandiko wangu katika barua zote. Hivi ndivyo, ninavyoandika.[#1 Kor. 16:21.]

18Upole wa Bwana wetu Yesu Kristo uwakalie ninyi nyote! Amin.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania