Yesaya 16

Yesaya 16

Wamoabu wanaomba msaada kwa Wayuda, wasiupate.

1Watumeni wana kondoo wapasao mtawala nchi,

watoke magengeni, wapite nyikani,

wafike mlimani kwa Binti Sioni!

2Kama ndege wanavyohangaika na kurukaruka

wakistushwa matunduni mwao,

ndivyo, wana wa Moabu watakavyokuwa

na kuvikimbilia vivuko vya Arnoni.

3Tupatieni mzungu! Tupatanisheni!

Vikuzeni vivuli vyenu vya mchana,

viwe virefu kama vya jioni,

viwe maficho yao wafukuzwao! Msiwachongee waliokimbia!

4Acha, wafukuzwao Moabu wafikie kwako!

Wawie ficho machoni pao wanaowakimbiza,

sharti siku zao wawasongao ziishe, maangamizo yamalizike,

nao waliowaponda watoweke katika nchi yao!

5Hapo kiti cha kifalme kitasimikwa kwa upole,

naye atakayekikalia kwa welekevu hemani mwa Dawidi

atakuwa mwamuzi atafutaye yanyokayo kwa kujua wongofu.

6Tuliyasikia majivuno ya Wamoabu kuwa makuu sana,

lakini hayo matukuzo na majivuno na machafuko yao ni maneno makuu tu.

7Kwa hiyo Wamoabu wote pamoja

na waipigie kilio nchi yao ya Moabu,

na wayalilie maandazi ya zabibu ya Kiri-Hereseti

kwa kupondeka rohoni.

8Kwani mashamba ya Hesiboni yamenyauka,

hata mizabibu ya Sibuma

iliyoleta zabibu zenye mvinyo kali

za kulevya nao wakuu wa wamizimu;

matawi yao yaliendelea sana,

yakafika Yazeri, mengine yakapotea nyikani,

miche yao ikaenea po pote mpaka kwenye bahari.

9Kwa hiyo nami ninaililia mizabibu ya Sibuma

pamoja na watu wa Yazeri,

machozi yangu yazinyeshee nchi za Hesiboni na za Elale,

kwani mazomeo yamewaangukia siku hizi za kiangazi

zilizo siku zenu za mavuno yenu.

10Shangwe za furaha zikatoweka mashambani,

nako mizabibuni hawapigi vigelegele wala mashangilio,

wala hakuna anayekamulia mvinyo makamulioni,

nyimbo za wakamuliaji nimezinyamazisha.

11Kwa hiyo nasikia ndani yangu mlio

kama wa zeze wa kuwalilia Wamoabu,

namo kufuani umo mlio

wa kuwalilia watu wa Kiri-Heresi.

12Napo hapo, Wamoabu watakapotokea vilimani juu

na kujisumbulia hapohapo,

napo, watakapoingia patakatifu pao kuomba,

hakuna watakachojipatia.

13Hilo ndilo tamko zito, Bwana alilolisema kale la kuwaambia Wamoabu;

14lakini sasa Bwana anasema hivi:

Itakapotimia miaka mitatu

iliyo kama miaka ya kibarua,

ndipo, utukufu wa Moabu utakapokuwa umebezeka,

nao ulikuwa haukupimika kwa wingi wa watu,

nalo sao lao litakuwa limepunguka,

liwe dogo sana pasipo nguvu zo zote.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania