Yesaya 18

Yesaya 18

Utume wa Mungu wa kuwaambia wajumbe weusi waliokuja Yerusalemu.

1Ninyi mliotoka katika nchi yenye vivuli viwili

iliyoko ng'ambo ya majito ya Nubi!

2Ninyi wajumbe mliokuja mkilifuata lile jito kubwa

katika mitumbwi yenu ya mafunjo ya kwendea juu ya maji,

ninyi wajumbe wepesi, nendeni kwenu

kwenye watu warefu sana wajipakao mafuta.

Ndio watu wanaoogopwa kwao hata kungineko,

kwa kuwa ni wenye nguvu za kuponda watu,

nayo nchi yao inakatwakatwa na mito.

3Nyote mkaao ulimwenguni, nyote mliotua nchini,

bendera itakapotwekwa milimani, itazameni!

Mabaragumu yatakapopigwa, yasikilizeni!

4Kwani hivi ndivyo, Bwana Mungu wangu anavyosema:

Nitatulia, nichungulie kwenye kao langu

kama mwangaza mweupe wa jua kali la mchana,

au kama wingu lenye umande siku za mavuno.

5Kwani mavuno yanapokuwa hayajafika bado,

maua yakiisha kupakatika, kole likiivisha zabibu zake,

ndipo, anapoyakata kwa kisu matawi yenye majani tu,

ndipo, anapoiondoa miche, itoke kabisa.

6Wote pamoja wataachiliwa madege wakaao milimani

nao nyama wa porini,

madege makubwa wakae hapo siku za kiangazi,

nao nyama wote wa porini wawe hapo siku za kipupwe.

7Siku zile Bwana Mwenye vikosi ataletewa matunzo nao walio watu warefu sana wajipakao mafuta. Ndio wale watu wanaoogopwa kwao na kungineko, kwa kuwa ni watu wenye nguvu za kuponda watu, nayo nchi yao inakatwakatwa na mito. Hao watatua matunzo yao mahali penye Jina la Bwana Mwenye vikosi, ndipo mlimani kwa Sioni.[#Sh. 68:30,32.]

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania