Yeremia 47

Yeremia 47

Mapatilizo yao Wafilisti na Watiro na Wasidoni.

1Hili ndilo neno la Bwana lililomjia mfumbuaji Yeremia kwa ajili ya Wafilisti, Farao alipokuwa hajaupiga Gaza.[#Yes. 14:29-32; Ez. 25:15-17.]

2Hivi ndivyo, Bwana anavyosema: Mtaona, maji yatakapokuja na kutoka kaskazini, yatakuwa mto ufurikao, yataifunikiza nchi nayo yote yaliyomo, miji nao wakaamo. Ndipo, watu watakapopiga makelele, watalia wote wakaao katika nchi hiyo.

3Kwa mashindo ya farasi wao wenye nguvu, wakipiga kwato zao, na kwa makelele ya magari yao na kwa uvumi wa magurudumu yao, baba hawatawageukia wana wao, kwani mikono itakuwa imewalegea.

4Kwani inakuja ile siku ya kuwaangamiza Wafilisti wote, ndiyo ya kuwang'olea Watiro na Wasidoni wasaidiaji wote waliosalia; ndipo, Bwana atakapowaangamiza Wafilisti walio masao yao waliokitoka kisiwa cha Kafutori.[#Amo. 9:7.]

5Wagaza watajinyoa vichwa, Waaskaloni pamoja nao waliosalia bondeni kwao watanyamazishwa, watajikata chale, mpaka lini?[#Yer. 41:5; 48:37; Amo. 1:6-8; Sef. 2:4; Zak. 9:5.]

6Mpaka lini upanga wake Bwana utakuwa hautulii? Jirudie alani mwako, upumzike na kunyamaza!

7Lakini utawezaje kutulia, Bwana akiuagiza kufanya kazi yake? Askaloni na pwani ndiko, Bwana alikoutuma.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania