Mashangilio 36

Mashangilio 36

Wabezi hujiponza, wamchao Mungu hubarikiwa.

1Upotovu husema ndani moyoni mwake yeye asiyemcha Mungu, kumwogopa Mungu hakupo machoni pake.[#Rom. 3:18.]

2Kwani hujidanganya kwamba: Manza, nilizozikora, macho yake hayataziona, asichukizwe nazo.

3Maneno, ayasemayo, ni maovu, tena madanganyifu; hukataa kuonyeka, asifanye mema.

4Maovu ndiyo, ayawazayo hapo, anapolala, hujisimamisha katika njia isiyo njema, nacho kilicho kibaya hana mwiko nacho.[#Mika 2:1.]

5Bwana, mpaka mbinguni unafika wema wako. welekevu wako unayafikia nayo mawingu.[#Sh. 57:11; 108:5.]

6Welekevu wako unasimama kama milima ya Mungu, maamuzi yako nayo hujenga, kama vilindi vijengavyo, Bwana, unawaokoa wote, watu na nyama.[#Sh. 125:1-2.]

7Kuliko wema wako, Mungu, hakuna chenye kiasi, wana wa watu hukikimbilia kivuli cha mabawa yako.

8Unono wa nyumba yako wanaushiba, navyo vinywaji vya urembo, unavyowanywesha, ni vingi kama vya mto.[#Sh. 23:5.]

9Kwani kwako kiko kisima chenye uzima, namo mwangani mwako tunauona mwanga.[#Yer. 2:13.]

10Ueneze wema wako kwao wakujuao nao wongofu wako kwao wanyokao mioyo!

11Miguu yao wajivunao isinijie, wala mikono yao wasiokucha isinifukuze!

12Kwao wafanyao maovu itakuja siku, watakapokuwa wameanguka, watakuwa wamebwagwa, wasiweze kuinuka tena.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania