1 Wathesalonike 4

1 Wathesalonike 4

Maisha yampendezayo Mungu

1Iliyobaki, ndugu, tunawasihi na kuwaonya kwamba mwenende katika Bwana Yesu; kama mlivyopokea kwetu jinsi iwapasavyo kuenenda na kumpendeza Mungu, kama nanyi mnavyoenenda, vivyo hivyo mpate kuzidi sana.[#2 The 3:6]

2Kwa kuwa mnajua ni maagizo gani tuliyowapa kwa Bwana Yesu.

3Maana haya ndiyo mapenzi ya Mungu, kutakaswa kwenu, mwepukane na uasherati;[#1 The 5:23; Ebr 10:10; 1 Pet 1:16]

4kila mmoja wenu ajue kuuweza mwili wake katika utakatifu na heshima;[#1 Kor 6:13,15]

5si katika hali ya tamaa mbaya, kama Mataifa wasiomjua Mungu.[#Yer 10:25; Zab 79:6]

6Mtu asimpunje ndugu yake wala kumkosea katika jambo hili; kwa sababu Bwana ndiye alipizaye kisasi cha haya yote; kama tulivyowaambia kwanza, tukashuhudia sana.[#Zab 94:2]

7Maana Mungu hakutuitia uchafu, bali tuwe katika utakaso.[#2 The 2:13,14]

8Basi yeye anayekataa, hakatai mwanadamu bali Mungu, anayewapa ninyi Roho wake Mtakatifu.[#Lk 10:16; Eze 36:27; 37:14]

9Kuhusu upendano, hamna haja niwaandikie; maana ninyi wenyewe mmefundishwa na Mungu kupendana.[#Yn 13:34; Yer 31:33,34]

10Kwa maana mnafanya neno hili kwa ndugu wote walio katika Makedonia yote. Lakini tunawasihi, ndugu, mzidi sana.[#2 The 3:4]

11Tena mjitahidi kutulia, na kutenda shughuli zenu, na kufanya kazi kwa mikono yenu wenyewe, kama tulivyowaagiza;[#Efe 4:28; 2 The 3:8,12]

12ili mwende kwa adabu mbele yao walio nje, wala msiwe na haja ya kitu chochote.[#Kol 4:5; 1 Kor 5:12,13]

Kuja kwa Bwana

13Lakini, ndugu, hatutaki msijue habari zao waliolala mauti, msije mkahuzunika kama na wengine wasio na matumaini.[#1 Kor 15:20; Efe 2:12]

14Maana, ikiwa tunaamini ya kwamba Yesu alikufa akafufuka, vivyo hivyo na hao waliolala katika Yesu, Mungu atawaleta pamoja naye.[#Rum 14:9; 1 Kor 15:3,4,12]

15Kwa kuwa tunawaambieni haya kwa neno la Bwana, kwamba sisi tulio hai, tutakaosalia hata wakati wa kuja kwake Bwana, hakika hatutawatangulia wao waliokwisha kulala mauti.[#1 Kor 15:51-52; 7:10,25]

16Kwa sababu Bwana mwenyewe atashuka kutoka mbinguni pamoja na mwaliko, na sauti ya malaika mkuu, na parapanda ya Mungu; nao waliokufa katika Kristo watafufuliwa kwanza.[#1 Kor 15:52; 2 The 1:7]

17Kisha sisi tulio hai, tuliosalia, tutanyakuliwa pamoja nao katika mawingu, ili tumlaki Bwana hewani; na hivyo tutakuwa pamoja na Bwana milele.[#Yn 12:26; 17:24]

18Basi, farijianeni kwa maneno hayo.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya