1 Wakorintho 16

1 Wakorintho 16

Michango kwa watakatifu

1Kuhusu ile michango kwa ajili ya watakatifu, kama vile nilivyoamuru makanisa ya Galatia, nanyi fanyeni vivyo hivyo.[#Rum 15:25-26; Mdo 11:29; Gal 2:10; 2 Kor 8:9]

2Siku ya kwanza ya juma kila mmoja wenu na aweke akiba kwake, kwa kadiri ya kufanikiwa kwake; ili kwamba michango isifanyike hapo nitakapokuja;[#Mdo 20:7]

3nami nitakapofika nitawatuma kwa barua wale mtakaowachagua, wachukue hisani yenu mpaka Yerusalemu.

4Na kama ikifaa niende na mimi, watasafiri pamoja nami.

Mipango ya usafiri

5Lakini nitakuja kwenu, nikiisha kupita kati ya Makedonia; maana napita kati ya Makedonia.[#Mdo 19:21]

6Labda nitakaa kwenu; naam, labda wakati wote wa baridi, mpate kunisafirisha kokote nitakakokwenda.[#Rum 15:24; Tit 3:12]

7Maana sipendi kuonana nanyi sasa, katika kupita tu, kwa sababu natarajia kukaa kwenu muda kidogo, Bwana akinijalia.[#Mdo 20:2; 18:21]

8Lakini nitakaa Efeso hadi siku ya Pentekoste;[#Law 23:15-21; Kum 16:9-11; Mdo 19:1,10; #Mdo 19:8-10]

9kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa wa kufaa sana, na wako wengi wanipingao.[#2 Kor 2:12; Kol 4:3; Ufu 3:8]

10Lakini, Timotheo akija, angalieni akae kwenu pasipo hofu; maana anaifanya kazi ya Bwana vile vile kama mimi mwenyewe;[#1 Kor 4:17; Flp 2:20]

11basi mtu yeyote asimdharau, lakini msafirisheni kwa amani, ili aje kwangu; maana ninamtazamia pamoja na ndugu zetu.[#1 Tim 4:12]

12Lakini kuhusu Apolo, ndugu yetu, nilimsihi sana aje kwenu pamoja na hao ndugu; ambaye si mapenzi yake kwenda sasa; lakini atakuja atakapopata nafasi.[#1 Kor 1:12; 3:6]

Wasia wa mwisho na salamu

13Kesheni, simameni imara katika imani, iweni na ujasiri, mkawe hodari.[#Zab 31:24; Efe 6:10]

14Mambo yenu yote na yatendeke katika upendo.

15Tena ndugu, nawasihi; (mnawajua watu wa nyumbani mwa Stefana kwamba ni malimbuko ya Akaya, nao wamejitia katika kazi ya kuwahudumia watakatifu);[#1 Kor 1:16; Rum 16:5]

16watiini watu kama hawa, na kila mtu afanyaye kazi pamoja nao, na kujitaabisha.[#Flp 2:29]

17Nami nafurahi kwa sababu ya kuja kwao Stefana na Fortunato na Akaiko; maana hawa wamenikirimia kwa wingi yale niliyopungukiwa kwenu.

18Maana wameniburudisha roho yangu, na roho zenu pia; basi wajueni sana watu kama hao.[#1 The 5:12]

19Makanisa ya Asia wawasalimu. Akila na Priska wawasalimu sana katika Bwana, pamoja na kanisa lililoko ndani ya nyumba yao.[#Mdo 18:2,18,26; Rum 16:3,5]

20Ndugu wote wawasalimu. Salimianeni kwa busu takatifu.[#Rum 16:16; 2 Kor 13:12; 1 Pet 5:14]

21Hii ni salamu yangu Paulo kwa mkono wangu mwenyewe.[#Kol 4:18; 2 The 3:17]

22Mtu awaye yote asiyempenda Bwana, na awe amelaaniwa. Maranatha.[#Gal 1:8,9; #16:22 maana yake ni, Bwana wetu anakuja.]

23Neema ya Bwana Yesu na iwe pamoja nanyi.

24Pendo langu na liwe pamoja nanyi nyote katika Kristo Yesu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya