2 Mambo ya Nyakati 8

2 Mambo ya Nyakati 8

Mengine aliyotenda Sulemani

1Ikawa miaka ishirini ilipopita, ambayo katika hiyo Sulemani aliijenga nyumba ya BWANA, na nyumba yake mwenyewe;[#1 Fal 9:10]

2ndipo Sulemani akaijenga miji ile Hiramu aliyompa Sulemani, akawapa makao humo wana wa Israeli.

3Naye Sulemani akaenda Hamath-zoba, akauteka.[#Hes 13:21; 2 Sam 8:3]

4Akaujenga Tadmori wa nyikani, na miji yote ya hazina, aliyoijenga katika Hamathi.[#1 Fal 9:17]

5Tena akaujenga Beth-horoni wa juu, na Beth-horoni wa chini, miji yenye boma, yenye kuta, na malango, na makomeo;

6na Baalathi, na miji yote ya hazina Sulemani aliyokuwa nayo, na miji yote ya magari yake, na miji ya wapanda farasi wake, na ya anasa yote aliyopenda Sulemani kujenga humo Yerusalemu, na katika Lebanoni, na katika nchi yote ya mamlaka yake.[#Yos 15:11]

7Basi kwa habari ya watu wote waliosalia wa Wahiti, na wa Waamori, na wa Waperizi, na wa Wahivi, na wa Wayebusi, wasiokuwa wa Israeli;[#1 Fal 9:20; Mwa 10:15; 15:18; Kum 7:1]

8wa watoto wao waliosalia baada yao katika nchi, ambao wana wa Israeli hawakuwakomesha, katika hao Sulemani akawatumikisha shokoa hata leo.

9Wala katika wana wa Israeli Sulemani hakuwafanya watumwa kazini mwake; lakini hao walikuwa watu wa vita, na wakuu wa majemadari wake, na makamanda wa magari yake na wa wapanda farasi wake.[#Kut 19:5; Kum 23:19; Law 25:39; Gal 4:28,31]

10Na hao walikuwa maofisa wakuu wa Sulemani, watu mia mbili na hamsini, waliotawala juu ya watu.[#1 Fal 5:16; 9:23; 2 Nya 2:18]

11Sulemani akamleta binti Farao kutoka mji wa Daudi mpaka nyumba aliyomjengea; kwa kuwa alisema, Mke wangu hatakaa nyumbani mwa Daudi mfalme wa Israeli, kwa kuwa ni patakatifu, mahali palipofika sanduku la BWANA.[#1 Fal 3:1; 7:8; 9:24]

12Ndipo Sulemani akamtolea BWANA sadaka za kuteketezwa juu ya madhabahu ya BWANA, aliyoijenga mbele ya ukumbi,

13kadiri ilivyohitajiwa huduma ya kila siku, akitoa sawasawa na amri ya Musa, siku za sabato, na za mwezi mpya, na za sikukuu zilizoamriwa, mara tatu kila mwaka, yaani, sikukuu ya mikate isiyochachwa, na sikukuu ya majuma, na sikukuu ya vibanda.[#Kut 29:38; Hes 28:3-26; 29:1; Kut 23:14; Kum 16:16; 1 Fal 9:25]

14Akaziamuru, kulingana na agizo la Daudi babaye, zamu za makuhani za kutumika, nao Walawi kwa kadiri ya malinzi yao, ili kusifu, na kuhudumu mbele ya makuhani, kama ilivyohitajiwa kila siku; tena mabawabu kwa zamu zao za kila mlango; maana ndivyo alivyoamuru Daudi mtu wa Mungu.[#1 Nya 24:1; 2 Nya 5:11; 31:2; Lk 1:5,8; 1 Nya 25:1; 9:17; 26:1; 2 Sam 23:2]

15Wala hawakuyaacha maagizo ya mfalme aliyowaamuru makuhani na Walawi kwa neno lolote, wala kwa habari ya hazina.

16Basi ikatengenezwa kazi yote ya Sulemani hata siku ya kutiwa msingi wa nyumba ya BWANA, na hata ilipokwisha. Hivyo ikamalizika nyumba ya BWANA.

17Ndipo Sulemani akaenda Esion-geberi, na Elothi, pwani ya nchi ya Edomu.[#1 Fal 9:26; Kum 2:8; 2 Fal 14:22]

18Naye Hiramu akamletea merikebu kwa mikono ya watumishi wake, na watumishi waliokuwa wanamaji; nao wakafika Ofiri pamoja na watumishi wa Sulemani, wakachukua kutoka huko talanta mia nne na hamsini za dhahabu, wakamletea mfalme Sulemani.[#1 Fal 9:27; 2 Nya 9:10,13; Mwa 10:29; Ayu 22:24; Isa 13:12]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya