Danieli 7

Danieli 7

Maono ya wanyama wanne

1Katika mwaka wa kwanza wa Belshaza, mfalme wa Babeli, Danieli alipata ndoto, na maono kichwani nwake, akiwa kitandani mwake; kisha akaiandika hiyo ndoto, akatoa habari ya jumla ya mambo hayo.[#Dan 2:28]

2Danieli akanena, akisema, Niliona katika maono yangu wakati wa usiku; na tazama, hizo pepo nne za mbinguni zilivuma kwa nguvu juu ya bahari kubwa.

3Ndipo wanyama wakubwa wanne wakatoka baharini, wote wa namna mbalimbali.[#Zek 6:1-4; Ufu 13:1; 17:8]

4Wa kwanza alikuwa kama simba, naye alikuwa na mabawa ya tai; nikatazama, hata mabawa yake akanyonyoka manyoya, akainuliwa katika nchi, akasimamishwa juu kwa miguu miwili kama mwanadamu; naye akapewa moyo wa kibinadamu.[#Kum 28:49; Yer 4:7,13; Ufu 13:2]

5Na tazama, mnyama mwingine, wa pili, kama dubu, naye aliinuliwa upande mmoja, na mifupa mitatu ya mbavu ilikuwamo kinywani mwake katika meno yake; wakamwambia mnyama huyo hivi, Inuka, ule nyama tele.[#Dan 2:39]

6Kisha nikatazama, na kumbe! Mnyama mwingine, kama chui, naye juu ya mgongo wake alikuwa na mabawa manne kama ya ndege; mnyama huyo alikuwa na vichwa vinne; akapewa mamlaka.[#Dan 8:8,22]

7Baadaye nikaona katika njozi ya usiku, na tazama, mnyama wa nne, mwenye kutisha, mwenye nguvu, mwenye uwezo mwingi, naye alikuwa na meno ya chuma, makubwa sana; alikula na kuvunja vipande vipande, na kuyakanyaga mabaki kwa miguu yake; na umbo lake lilikuwa mbali kabisa na wale wa kwanza, naye alikuwa na pembe kumi.[#Ufu 12:3; 13:1]

8Nikaziangalia sana pembe zake, na tazama, pembe nyingine ikazuka kati yao, nayo ilikuwa ndogo, ambayo mbele yake pembe tatu katika zile za kwanza zikang'olewa kabisa; na tazama, katika pembe hiyo mlikuwa na macho kama macho ya mwanadamu, na kinywa kilichokuwa kikinena maneno makuu.[#Dan 8:9; Ufu 13:5-6]

Hukumu mbele ya mzee wa kale

9Nikatazama hata viti vya enzi vikawekwa, na mmoja aliye mzee wa siku ameketi; mavazi yake yalikuwa meupe kama theluji, na nywele za kichwa chake kama sufu safi; kiti chake cha enzi kilikuwa miali ya moto, na gurudumu zake moto uwakao.[#1 Kor 15:24; Zab 90:2; 104:2-4; Ufu 20:4; 1:14]

10Mto kama wa moto ukatoka ukapita mbele zake; maelfu wakamtumikia, na mamilioni wakasimama mbele zake; hukumu ikawekwa, na vitabu vikafunuliwa.[#Kum 33:2; Zab 68:17; Mt 25:31,32; Ufu 5:11; 20:12]

11Nikatazama wakati huo; kwa sababu ya sauti ya yale maneno makubwa iliyoyasema ile pembe; nilitazama hata mnyama yule akauawa, mwili wake ukaharibiwa, akatolewa ateketezwe kwa moto.[#Ufu 19:20]

12Na kwa habari za wale wanyama wengine, walinyang'anywa mamlaka yao; lakini maisha yao yalidumishwa kwa wakati na majira.

13Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye.[#Isa 9:6,7; Eze 1:26; Mt 24:30; 26:64; Mk 13:26; 14:62; Lk 21:27; Ufu 1:7,13; 14:14]

14Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa.[#Zab 2:6; 110:1; Mt 11:27; Yn 3:35; Isa 9:7; Oba 1:21; Mik 4:7; Lk 1:33; Ebr 12:28; Ufu 11:15]

Maono ya Danieli yafasiriwa

15Basi, mimi Danieli, roho yangu ilihuzunika ndani yangu, na hayo maono ya kichwa changu yakanifadhaisha.

16Nikamkaribia mmoja wa hao waliosimama karibu, nikamwuliza maana ya kweli ya hayo yote. Basi akaniambia, akanijulisha tafsiri ya mambo hayo.

17Wanyama hao wakubwa walio wanne ni wafalme wanne watakaotokea duniani.

18Lakini watakatifu wake Aliye Juu wataupokea ufalme, na kuumiliki huo ufalme milele, naam hata milele na milele.[#Isa 60:12; Ufu 22:5]

19Kisha nilitaka kujua maana ya yule mnyama wa nne, aliyekuwa mbali na wenziwe wote, mwenye kutisha sana, ambaye meno yake yalikuwa ya chuma, na makucha yake ya shaba; aliyekula, na kuvunja vipande vipande, na kuyakanyaga mabaki kwa miguu yake;

20na habari za zile pembe kumi zilizokuwa kichwani mwake, na ile pembe nyingine iliyozuka, ambayo mbele yake zilianguka pembe tatu; yaani, pembe ile yenye macho, na kinywa kilichonena makuu, ambayo kuonekana kwake kulikuwa hodari kuliko wenzake.

21Nikatazama, na pembe iyo hiyo ilifanya vita na watakatifu, ikawashinda;[#Ufu 11:7; 13:7]

22hata akaja huyo mzee wa siku, nao watakatifu wake Aliye Juu wakapewa hukumu; na majira yakawadia watakatifu waumiliki ufalme.[#Ufu 1:6; 20:4; 2 The 2:8; 1 Kor 6:2]

23Akanena hivi, Huyo mnyama wa nne atakuwa ni ufalme wa nne juu ya dunia, utakaokuwa mbali na falme zile zote, nao utaangamiza dunia yote, na kuikanyaga, na kuivunja vipande vipande.

24Na habari za zile pembe kumi, katika ufalme huo wataondoka wafalme kumi; na mwingine ataondoka baada ya hao; naye atakuwa mbali na hao wa kwanza; naye atawashusha wafalme watatu.[#Ufu 17:12]

25Naye atanena maneno kinyume chake Aliye Juu, naye atawadhoofisha watakatifu wake Aliye Juu; naye ataazimu kubadili majira na sheria; nao watatiwa mikononi mwake kwa nyakati tatu na nusu[#Isa 37:23; Ufu 17:6; 18:24; Dan 2:21; 12:7; Ufu 12:14; 13:5-6]

26Lakini hukumu itawekwa, nao watamwondolea mamlaka yake, kuipoteza na kuiangamiza, hata milele.

27Na ufalme, na mamlaka, na ukuu wa ufalme, chini ya mbingu zote, watapewa watu wa watakatifu wake Aliye Juu; ufalme wake ni ufalme wa milele, na wote wenye mamlaka watamtumikia na kumtii.[#Zab 146:10; Lk 1:33; Ufu 11:5; Ufu 20:4; 22:5]

28Huu ndio mwisho wa jambo lile. Nami, Danieli, fikira zangu zilinifadhaisha, na uso wangu ulinibadilika; lakini nililiweka jambo hilo moyoni mwangu.[#Lk 2:19]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya