Kumbukumbu la Torati 24

Kumbukumbu la Torati 24

Sheria kuhusu ndoa na talaka

1Mtu akiisha kutwaa mke kwa kumwoa, asipopata kibali machoni mwake, kwa kuwa ameona neno ovu kwake, na amwandikie hati ya kumwacha, akamtilie mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake.[#Mt 5:31; 19:7; Mk 10:4]

2Naye akiisha kuondoka katika nyumba yake, ana ruhusa kwenda akawa mke wa mtu mwingine.

3Na huyo mumewe wa sasa akimchukia, na kumwandikia hati ya kumwacha, na kumpa mkononi mwake, na kumtoa katika nyumba yake; au akifa yeye mumewe wa sasa, aliyemtwaa kuwa mkewe;

4yule wa kwanza aliyemwacha asimtwae kuwa mkewe tena, akiisha kutiwa unajisi; kwa kuwa haya ni machukizo mbele za BWANA; kwa hiyo usiitie dhambini nchi, akupayo BWANA, Mungu wako, iwe urithi.[#Yer 3:1]

Sheria mbalimbali

5Mtu atwaapo mke mpya, asiende vitani pamoja na jeshi, wala asipewe shughuli juu yake yoyote; akae faragha mwaka mmoja nyumbani mwake, apate mfurahisha mkewe aliyemtwaa.[#Mit 5:18]

6Mtu awaye yote asitwae jiwe la kusagia, la juu wala la chini, kuwa rehani; kwani hivi ni kutwaa maisha ya mtu kuwa rehani.[#Isa 47:2]

7Mtu akionekana anamwiba nduguze mmojawapo katika wana wa Israeli, akamfanya kama mtumwa, au kumwuza; na afe mwizi huyo; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako.[#Kut 21:16]

8Angalia katika pigo la ukoma, utunze kwa bidii, kwa kufanya mfano wa yote watakayowafundisha makuhani Walawi; tunzeni kwa kuyafanya vile vile kama nilivyowaamuru wao.[#Law 13:2; 14:2; Mt 8:4; Mk 1:44; Lk 5:14; 7:14]

9Kumbukeni na BWANA, Mungu wako alivyomtenda Miriamu katika njia mlipotoka Misri.[#Hes 12:10; Lk 17:32; 1 Kor 10:6]

10Umkopeshapo jirani yako chochote kikopeshwacho usiingie katika nyumba yake kwenda kutwaa rehani kwake.[#Kut 22:26-27]

11Simama nje, yule umkopeshaye akuletee nje ile rehani.

12Naye akiwa ni mtu maskini, usilale na rehani yake.

13Sharti umrudishie rehani lichwapo jua, apate kulala na mavazi yake, na kukubarikia; nayo itakuwa ni haki kwako mbele za BWANA, Mungu wako.[#Kut 22:26; Ayu 24:7,8; 31:16-20; Eze 18:7,12,16; 33:15; Amo 2:8; Ayu 29:11; 31:20; 2 Kor 9:13; 2 Tim 1:18; Kum 6:25; Zab 106:31; 112:9; Dan 4:27]

14Usimwonee mtumishi mwenye ujira aliye maskini na uhitaji, kama ni wa nduguzo, au kama ni wageni wako mmojawapo walio katika nchi yako, ndani ya malango yako;[#Law 19:13; Mit 14:31; Amo 4:1; Mal 3:5]

15mpe ujira wake kwa siku yake, wala jua lisichwe juu yake; kwa maana ni maskini, moyo wake umeutumainia huo; asije akamlilia BWANA juu yako, ikawa ni dhambi kwako.[#Law 19:13; Yer 22:13; Ayu 27:13; 35:9; Yak 5:4]

16Mababa wasiuawe kwa ajili ya watoto wao, wala watoto wasiuawe kwa ajili ya baba zao; kila mtu na auawe kwa ajili ya dhambi yake mwenyewe.[#2 Fal 14:6; 2 Nya 25:4; Yer 31:29,30; Eze 18:20]

17Usipotoshe hukumu ya mgeni, wala ya yatima; wala usitwae mavazi ya mjane, yawe rehani;[#Kut 23:9; Law 19:33-34; Kum 27:19; Kut 22:21,22; Mit 22:22; Isa 1:23; Yer 5:28; Zek 7:10; Mal 3:5; Kut 22:26]

18bali kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika Misri, BWANA, Mungu wako, akakukomboa huko; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili.

19Uvunapo mavuno yako katika shamba lako, ukasahau mganda shambani, usirudi kuuchukua; na uwe wa mgeni, au yatima, au mjane; ili BWANA, Mungu wako, akubariki katika kazi yote ya mikono yako.[#Law 19:9-10; 23:22; Mit 19:17]

20Utakapochuma matunda ya mizeituni yako, usirudi kuchuma mara ya pili; yaliyobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane.

21Uchumapo zabibu katika shamba lako la mizabibu, usichume mara ya pili; zilizobaki apewe mgeni, na yatima, na mjane.

22Nawe kumbuka ya kuwa ulikuwa mtumwa katika nchi ya Misri; kwa hiyo nakuamuru kutenda neno hili.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya