Waefeso 2

Waefeso 2

Kutoka mauti hadi uhai

1Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi zenu;[#Kol 1:21; 2:13]

2ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa kuasi;[#Efe 6:12; Tit 3:3; Yn 12:31; Kol 1:13]

3ambao zamani, sisi sote nasi tulienda kati yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia, tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira, kama wengineo wote.[#Kol 3:6]

4Lakini Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda;

5hata wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alitufanya kuwa hai pamoja na Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema.[#Lk 15:24,32; Efe 5:14; Rum 6:13]

6Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu;[#Rum 8:10; Flp 3:20]

7ili katika zamani zinazokuja audhihirishe wingi wa neema yake upitao kiasi kwa wema wake kwetu sisi katika Kristo Yesu.[#Efe 1:7]

8Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu;[#Gal 2:16]

9wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu.[#1 Kor 1:29]

10Maana tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo.[#Tit 2:14]

Umoja katika Kristo

11Kwa ajili ya hayo kumbukeni ya kwamba zamani ninyi, mlio watu wa Mataifa kwa jinsi ya mwili, mnaoitwa Wasiotahiriwa na wale wanaoitwa Waliotahiriwa, yaani, tohara ya mwilini iliyofanyika kwa mikono;[#Efe 5:8]

12kwamba zamani zile mlikuwa hamna Kristo, mmefarakana na jamii ya Israeli, wageni wasio wa maagano ya ahadi ile. Mlikuwa hamna tumaini, hamna Mungu duniani.[#Rum 9:4; 1 The 4:13]

13Lakini sasa, katika Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake Kristo.[#Isa 57:19; 52:7; Kol 1:20]

14Kwa maana yeye ndiye amani yetu, aliyetufanya sisi sote tuliokuwa wawili kuwa mmoja; akakibomoa kiambaza cha kati kilichotutenga.[#Isa 9:5; Gal 3:28; Kol 2:14]

15Naye akiisha kuuondoa ule uadui kwa mwili wake; ndiyo sheria ya amri zilizo katika maagizo; ili afanye hao wawili kuwa mtu mpya mmoja ndani ya nafsi yake; akafanya amani.[#Kol 2:14; 2 Kor 5:17]

16Akawapatanisha wote wawili na Mungu katika mwili mmoja, kwa njia ya msalaba, akiisha kuumaliza ule uadui kwa huo msalaba.[#Kol 1:20,22]

17Akaja akahubiri amani kwenu ninyi mliokuwa mbali, na amani kwao wale waliokuwa karibu.[#Isa 57:19; Zek 9:10]

18Kwa maana kwa yeye sisi sote tumepata njia ya kumkaribia Baba katika Roho mmoja.[#Efe 3:12]

19Basi tangu sasa ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu.[#Efe 3:6; Ebr 12:22,23]

20Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni.[#Mt 16:18; Isa 28:16]

21Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana.[#Kol 2:19]

22Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho.[#1 Pet 2:5]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya