Ezekieli 28

Ezekieli 28

Utabiri juu ya mfalme wa Tiro

1Neno la BWANA likanijia tena, kusema,

2Mwanadamu, mwambie mkuu wa Tiro, Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa moyo wako umeinuka, nawe umesema, Mimi ni mungu, nami nimeketi katika kiti cha Mungu, kati ya bahari; lakini u mwanadamu wala si Mungu, ujapokuwa umeweka moyo wako kama moyo wa Mungu.[#Kum 8:14; 2 Nya 26:16; Mit 16:18; Dan 5:22,23; Isa 2:12; 31:3; 1 Tim 3:6; Zab 9:20]

3Tazama, una hekima kuliko Danieli; hapana neno la siri watu wawezalo kukuficha;[#Dan 2:48; Zek 9:2]

4kwa hekima yako na kwa fahamu zako umejipatia utajiri, nawe umepata dhahabu na fedha katika hazina zako;

5kwa hekima yako nyingi, na kwa biashara yako, umeongeza utajiri wako, na moyo wako umeinuka kwa sababu ya utajiri wako;[#Kum 8:12-14]

6basi, kwa hiyo, Bwana MUNGU asema hivi; Kwa kuwa umeweka moyo wako kama moyo wa Mungu;[#Dan 7:25,26; Mdo 12:22; 2 The 2:4]

7basi, tazama, nitaleta wageni juu yako, watu wa mataifa wenye kutisha; nao watafuta panga zao juu ya uzuri wa hekima yako, nao watautia uchafu mwangaza wako.[#Eze 30:11]

8Watakushusha hadi shimoni; nawe utakufa kifo chao waliouawa kati ya bahari.

9Je! Utazidi kusema mbele yake huyo akuuaye, Mimi ni mungu? Lakini u mwanadamu, wala si Mungu, mkononi mwake akutiaye jeraha.

10Utakufa kifo cha hao wasiotahiriwa, kwa mikono ya wageni; kwa maana mimi nimenena neno hili, asema Bwana MUNGU.[#Eze 31:18]

Maombolezo juu ya mfalme wa Tiro

11Tena neno la BWANA likanijia, kusema,

12Mwanadamu, umfanyie maombolezo mfalme wa Tiro, umwambie, Bwana MUNGU asema hivi; Wewe wakitia mhuri kipimo, umejaa hekima, na ukamilifu wa uzuri.[#Eze 27:3]

13Ulikuwa ndani ya Adeni, bustani ya Mungu; kila jiwe la thamani lilikuwa kifuniko chako, akiki, na yakuti manjano, na almasi, na zabarajadi, na shohamu, na yaspi, na yakuti samawi, na zumaridi, na baharamani, na dhahabu; kazi ya matari yako na filimbi zako ilikuwa ndani yako; katika siku ya kuumbwa kwako zilitengenezwa tayari.[#Mwa 2:8; 3:23,24; Eze 31:8,9; 26:13; Yoe 2:3]

14Wewe ulikuwa kerubi mwenye kutiwa mafuta afunikaye; nami nilikuweka hata ukawa juu ya mlima mtakatifu wa Mungu, umetembea huku na huko kati ya mawe ya moto.[#Kut 25:20; Eze 20:40]

15Ulikuwa mkamilifu katika njia zako tangu siku ile ulipoumbwa, hata uovu ulipoonekana ndani yako.

16Kwa wingi wa uchuuzi wako watu walikujaza udhalimu ndani yako, nawe umetenda dhambi; kwa sababu hiyo nimekutoa kwa nguvu katika mlima wa Mungu, kama kitu kilicho najisi; nami nimekuangamiza, Ewe kerubi ufunikaye, utoke katika mawe hayo ya moto.

17Moyo wako uliinuka kwa sababu ya uzuri wako; umeiharibu hekima yako kwa sababu ya mwangaza wako; nimekutupa chini, nimekulaza mbele ya wafalme, wapate kukutazama.[#2 Pet 2:6; Yud 1:7]

18Kwa wingi wa maovu yako, katika uovu wa uchuuzi wako, umepatia unajisi patakatifu pako; basi nimetokeza moto kutoka ndani yako, nao umekuteketeza, nami nimekufanya kuwa majivu juu ya nchi, machoni pa watu wote wakutazamao.[#Amo 1:10]

19Wote wakujuao kati ya makabila ya watu watakustaajabia; umekuwa kitu cha kutisha, wala hutakuwapo tena hata milele.

Utabiri juu ya Sidoni

20Neno la BWANA likanijia, kusema,[#Yoe 3:4-8; Zek 9:1-2; Mt 11:21-22; Lk 10:13-14]

21Mwanadamu, uuelekezee Sidoni uso wako, ukatabiri juu yake,[#Isa 23:4,12; Yer 25:22; Eze 32:30]

22useme, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ee Sidoni, nami natukuzwa kati yako; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA, nitakapokuwa nimetekeleza hukumu zangu ndani yake, na kutakasika ndani yake.[#Kut 14:4; Zab 9:16; Eze 39:13; 20:41]

23Maana nitampelekea tauni, na damu, katika njia kuu zake, na hao waliotiwa jeraha wataanguka kati yake, kwa upanga juu yake pande zote; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA.[#Eze 38:22]

24Wala hautakuwapo mchongoma uchomao kwa nyumba ya Israeli; wala mwiba uumizao miongoni mwa wote wamzungukao, waliowatenda mambo ya jeuri; nao watajua ya kuwa mimi ndimi Bwana MUNGU.[#Hes 33:55; Yos 23:13]

Baraka ijayo kwa Israeli

25Bwana MUNGU asema hivi; Nitakapokuwa nimewakusanya nyumba ya Israeli, na kuwatoa katika watu ambao wametawanyika kati yao, na kutakasika kati yao machoni pa mataifa, ndipo watakapokaa katika nchi yao wenyewe, niliyompa mtumishi wangu, Yakobo.[#Isa 11:12; Hos 1:11; Eze 20:41]

26Nao watakaa humo salama; naam, watajenga nyumba, na kupanda mashamba ya mizabibu, na kukaa salama; nitakapokuwa nimetekeleza hukumu zangu juu ya watu wote, wanaowatenda mambo ya jeuri pande zote; nao watajua ya kuwa mimi ndimi BWANA, Mungu wao.[#Isa 65:21; Amo 9:14; Yer 31:5]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya