Mwanzo 13

Mwanzo 13

Kutengana kwa Abramu na Lutu

1Abramu akapanda kutoka Misri, yeye, na mkewe, na kila alichokuwa nacho, na Lutu pamoja naye, mpaka kusini.

2Naye Abramu alikuwa tajiri sana kwa mifugo, kwa fedha, na kwa dhahabu.[#Mwa 24:35; Zab 112:3; Mit 10:22]

3Akaendelea kusafiri kutoka kusini mpaka Betheli, mahali pale palipokuwapo hema yake kwanza, kati ya Betheli na Ai;

4napo ndipo palipokuwa na madhabahu aliyofanya hapo kwanza; naye Abramu akaliitia jina la BWANA hapo.[#Mwa 12:7,8]

5Na Lutu aliyesafiri pamoja na Abramu, yeye naye alikuwa na makundi ya ng'ombe na kondoo, na hema.

6Na ile nchi haikuwatosha, ili wakae pamoja; maana mali zao zilikuwa nyingi, hata wasiweze kukaa pamoja.[#Mwa 36:7; Lk 12:17,18]

7Kukawako ugomvi kati ya wachunga wanyama wa Abramu, na wachunga wanyama wa Lutu; na siku zile Wakanaani na Waperizi walikuwa wakikaa katika nchi.[#Mwa 26:20]

8Abramu akamwambia Lutu, Basi, usiwepo ugomvi, nakusihi, kati yangu na wewe, wala kati ya wachungaji wangu na wachungaji wako; maana sisi tu jamaa moja.[#Flp 2:14,15; Zab 133:1]

9Je! Nchi hii yote haiko mbele yako? Basi jitenge nami, nakusihi; ukienda upande wa kushoto, nitakwenda upande wa kulia; ukienda upande wa kulia, nitakwenda upande wa kushoto.[#Mwa 20:15; Rum 12:18; Ebr 12:14; Yak 3:13-18]

10Lutu akainua macho yake, akaliona Bonde lote la Yordani, ya kwamba lote pia lina maji, kabla BWANA hajaharibu Sodoma na Gomora, lilikuwa kama bustani ya BWANA, kama nchi ya Misri hapo unapokwenda Soari.[#Mwa 2:10; Hes 32:1; Kum 34:3; Zab 107:34; Mwa 14:2; 19:22,24]

11Basi Lutu akajichagulia Bonde lote la Yordani; Lutu akasafiri kwenda upande wa mashariki; wakatengana wao kwa wao.

12Abramu akakaa katika nchi ya Kanaani, na Lutu akakaa katika miji ya lile Bonde; akajongeza hema yake mpaka Sodoma.[#Mwa 19:29]

13Lakini watu wa Sodoma walikuwa wabaya, wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya BWANA.[#Mwa 6:11; 18:20; Eze 16:49; 2 Pet 2:7]

14BWANA akamwambia Abramu, alipokwisha kutengana na Lutu, Inua sasa macho yako, ukatazame kutoka hapo ulipo, upande wa kaskazini, na wa kusini na wa mashariki na wa magharibi;[#Isa 49:18; Mwa 28:14]

15maana nchi hii yote uionayo, nitakupa wewe na uzao wako hata milele.[#Mdo 7:5; 2 Nya 20:7]

16Na uzao wako nitaufanya uwe kama mavumbi ya nchi; ikiwa mtu ataweza kuyahesabu mavumbi ya nchi, uzao wako nao utahesabika.[#Mwa 26:4; Kut 32:13; Hes 23:10; Kum 1:10; 1 Nya 27:23; Yer 33:22; Rum 4:16; Ebr 11:12]

17Ondoka, ukatembee katika nchi hii katika mapana yake, na marefu yake, maana nitakupa wewe nchi hiyo.

18Basi Abramu akahamisha hema yake, akaja na kukaa karibu na mialoni ya Mamre, nayo ni miti iliyoko Hebroni, akamjengea BWANA madhabahu huko.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya