Mwanzo 24

Mwanzo 24

Ndoa ya Isaka na Rebeka

1Basi Abrahamu alikuwa mzee mwenye miaka mingi, na BWANA alikuwa amembariki Abrahamu katika vitu vyote.[#Mwa 18:11; 13:2; Gal 3:9]

2Abrahamu akamwambia mtumishi wake, mzee wa nyumba yake, aliyetawala vitu vyake vyote, Tafadhali uutie mkono wako chini ya paja langu,[#Mwa 15:2; 24:10; 39:4-6; 47:29; Omb 5:6]

3nami nitakuapisha kwa BWANA, Mungu wa mbingu, na Mungu wa nchi, kwamba hutamtwalia mwanangu mke katika binti za Wakanaani ambao nakaa kati yao;[#Kut 34:16; Kum 7:3; 2 Kor 6:14-17]

4bali nenda hata nchi yangu, na kwa jamaa zangu, ukamtwalie mwanangu Isaka mke.[#Mwa 28:2]

5Yule mtumishi akamwambia, Labda yule mwanamke hatakubali kufuatana nami mpaka nchi hii, je! Nimrudishe mwanao mpaka nchi ulikotoka?

6Abrahamu akamwambia, Ujihadhari, usimrudishe mwanangu huko.[#2 Pet 2:20-22]

7BWANA, Mungu wa mbingu, aliyenitoa katika nyumba ya babangu, na kusema nami katika nchi niliyozaliwa, aliniapia akisema, Nitawapa uzao wako nchi hii; yeye atamtuma malaika wake mbele yako, nawe utamtwalia mwanangu mke kutoka huko;[#Mwa 12:1,7; 13:15; Kut 32:13; 23:20; Zab 34:7; Isa 63:9]

8na yule mwanamke asipokubali kufuatana nawe, basi, utafunguliwa kiapo changu hiki; lakini usimrudishe mwanangu huko.[#Yos 2:17-20]

9Yule mtumishi akaweka mkono wake chini ya paja la Abrahamu bwana wake, akamwapia katika neno hilo.

10Kisha huyo mtumishi akatwaa ngamia kumi katika ngamia za bwana wake akaenda zake, maana mali zote za bwana wake zilikuwa mkononi mwake, akaondoka, akaja mpaka Mesopotamia, mpaka mji wa Nahori.[#Mwa 27:43]

11Akawapigisha magoti ngamia nje ya mji karibu na kisima cha maji wakati wa jioni, wakati ambapo wanawake wanakwenda kuteka maji.[#Kut 2:16; 1 Sam 9:11]

12Naye akasema, Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, nakuomba mambo yangu uyajalie yawe heri leo, ukamfadhili bwana wangu Abrahamu.[#Mwa 24:27; 26:24; Kut 3:6,15; Flp 4:6]

13Tazama! Nimesimama karibu na kisima cha maji, na binti za watu wa mjini wanatoka kuteka maji,

14basi na iwe hivi; yule msichana nitakayemwambia, Tua mtungi wako, nakuomba, ninywe; naye akasema, Unywe, nami nitawanywesha na ngamia zako pia; basi huyu na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako Isaka; na kwa hayo nitajua ya kuwa umemfadhili bwana wangu.[#Mit 19:14; Amu 6:17-37; 1 Sam 6:7]

15Ikawa, kabla hajaisha kunena, tazama, Rebeka anatokea, binti wa Bethueli mwana wa Milka, mkewe Nahori, ndugu wa Abrahamu, naye ana mtungi begani pake.[#Zab 34:15; Mwa 11:29]

16Naye yule msichana alikuwa mzuri sana uso wake, bikira, wala mwanamume hajamjua bado; akashuka kisimani, akajaza mtungi wake, akapanda.[#Mwa 26:7]

17Ndipo yule mtumishi akapiga mbio kwenda kumlaki, akasema, Tafadhali unipe maji kidogo katika mtungi wako ninywe.[#Yn 4:7]

18Naye akasema, Unywe, bwana wangu, akafanya haraka, akatua mtungi wake mkononi mwake, akamnywesha.[#1 Pet 3:8; 4:9]

19Hata alipokwisha kumnywesha akasema, Na ngamia wako nitawatekea, hadi watakapokwisha kunywa.

20Akafanya haraka, akamwaga maji ya mtungi wake katika birika, akapiga mbio kisimani ateke, akawatekea ngamia wake wote.

21Basi yule mtu akamkazia macho, akanyamaza, ili ajue kama BWANA ameifanikisha safari yake ama sivyo.[#Lk 2:19,51]

22Ikawa, ngamia walipokwisha kunywa, yule mtu akatwaa pete ya dhahabu, uzani wake ulikuwa nusu shekeli, na vikuku viwili kwa mikono yake, uzani wake ulikuwa shekeli kumi za dhahabu,[#Kut 32:2,3; Isa 3:19,20; 1 Pet 3:3]

23akasema, U binti wa nani wewe? Tafadhali uniambie. Je! Iko nafasi katika nyumba ya baba yako tupate mahali pa kukaa kwa muda?

24Akasema, Mimi ni binti wa Bethueli mwana wa Milka, aliyemzalia Nahori.

25Tena akamwambia, Kwetu kuna majani na malisho ya kutosha, na mahali pa kukaa wageni.[#1 Pet 4:9]

26Yule mtu akainama akamsujudu BWANA.[#Mwa 24:52; Kut 4:31]

27Akasema, Na atukuzwe BWANA, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye hakuacha rehema zake na kweli yake kwa bwana wangu. BWANA akaniongoza mimi nami njiani hata nyumba ya nduguze bwana wangu.[#Kut 18:10; Rut 4:14; 1 Sam 25:32; 2 Sam 18:28; Lk 1:68; Mwa 32:10; Zab 98:3; Mwa 24:48; Mit 3:6]

28Basi yule msichana akapiga mbio, akawaambia watu wa nyumba ya mama yake mambo hayo.

29Na Rebeka alikuwa na kaka, jina lake Labani. Labani akatoka mbio kumwendea yule mtu kisimani.[#Mwa 29:5]

30Ikawa, alipoiona ile pete, na vikuku mikononi mwa dada yake, akasikia maneno ya Rebeka dada yake, akisema, Hivyo ndivyo alivyoniambia mtu huyo, basi akamjia mtu yule, na tazama, amesimama karibu na ngamia kisimani.

31Akasema, Karibu, wewe uliyebarikiwa na BWANA, mbona unasimama nje? Kwa maana nimeiweka nyumba tayari, na nafasi kwa ngamia.[#Mwa 26:29; Amu 17:2; Rut 3:10; Zab 115:15]

32Na mtu yule akaingia katika nyumba, akawafungua ngamia; naye akatoa majani na malisho kwa ngamia, na maji ya kuoshea miguu yake, na miguu ya watu waliokuwa pamoja naye.[#Mwa 43:24; Amu 19:21]

33Akaandaliwa chakula, lakini akasema, Sili mpaka niseme kwanza maneno yangu. Akamwambia, Haya, sema.[#Ayu 23:12; Yn 4:34; Efe 6:5-7]

34Akasema, Mimi ni mtumwa wa Abrahamu,

35na BWANA amembarikia sana bwana wangu, amekuwa mtu mkuu; amempa kondoo, na ng'ombe, na fedha, na dhahabu, na watumishi, na wajakazi, na ngamia, na punda.[#Mwa 24:1; 13:2; Ayu 1:3]

36Naye Sara, mkewe bwana wangu, akamzalia bwana wangu mwana wa kiume, katika uzee wake; naye amempa yote aliyo nayo.[#Mwa 21:2,10; 25:5]

37Kisha bwana wangu akaniapisha akisema, Usimtwalie mwanangu mke wa binti za Wakanaani, ambao nakaa katika nchi yao.[#Mwa 24:3]

38Ila uende mpaka nyumbani kwa babangu, na kwa jamaa zangu, ukamtwalie mwanangu mke.

39Nikamwambia bwana wangu, Labda huyo mwanamke hatafuatana nami.

40Akaniambia, BWANA, ambaye naenenda machoni pake, atatuma malaika wake pamoja nawe, atafanikisha njia yako; nawe umtwalie mwanangu mke katika jamaa zangu, na wa nyumba ya babangu.[#Mwa 24:7; 5:22-24; 17:1; Kut 23:20]

41Ndipo utafunguliwa kiapo changu hapo utakapowafikia jamaa zangu; hata wasipokupa msichana huyo, utafunguliwa kiapo changu.[#Mwa 24:8]

42Nami nikaja leo kisimani, nikasema, Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ukinifanikishia sasa njia yangu niendayo mimi,[#1 Fal 1:36; Mdo 10:7,8,22; Neh 1:11; Zab 90:17; Rum 1:10]

43tazama! Nimesimama karibu na kisima cha maji; basi na iwe hivi, msichana ajaye kuteka maji, nikamwambia, Nipe, nakuomba, maji kidogo katika mtungi wako ninywe,[#Mwa 24:13]

44naye akaniambia, Unywe wewe, na ngamia wako pia nitawatekea, huyo na awe ndiye mke BWANA aliyemwekea mwana wa bwana wangu.[#Ebr 13:2]

45Hata kabla sijaisha kusema moyoni mwangu, tazama! Rebeka akatokea, na mtungi begani mwake. Akashuka kisimani akateka. Nami nikamwambia, Tafadhali nipe maji ninywe.[#Mwa 24:15; 1 Sam 1:13; Isa 65:24]

46Akafanya haraka akatua mtungi wake chini, akasema, Unywe, na ngamia wako nitawanywesha pia; basi nikanywa, akawanywesha na ngamia nao.

47Kisha nikamwuliza, U binti wa nani wewe? Naye akasema, Mimi ni binti Bethueli, mwana wa Nahori, Milka aliyemzalia. Nami nikamtia kishaufu puani mwake na vikuku mikononi mwake.[#Eze 16:11,12]

48Nikainama, nikamsujudia BWANA, nikamtukuza BWANA, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, aliyeniongoza njiani, nimtwalie mwana wa bwana wangu binti wa ndugu yake.[#Mwa 24:26; Zab 32:8; 48:14; 107:7; Isa 48:17]

49Basi, kama mnataka kumfanyia rehema na kweli bwana wangu, niambieni kama sivyo, niambieni; ili nigeuke upande wa kulia au wa kushoto.[#Mwa 47:29; Yos 2:14]

50Ndipo Labani na Bethueli wakajibu wakasema, Neno hili limetoka kwa BWANA, wala sisi hatuwezi kukuambia neno jema wala baya.[#Zab 118:23; Mt 21:42; Mk 12:11]

51Tazama, huyo Rebeka yuko mbele yako, umchukue, ukaende zako awe mke wa mwana wa bwana wako, kama alivyosema BWANA.[#Mwa 20:15]

52Ikawa mtumishi wa Abrahamu aliposikia maneno yao, akainama hata nchi mbele za BWANA.

53Kisha huyo mtumishi akatoa vyombo vya fedha, na vyombo vya dhahabu, na mavazi, akampa Rebeka; na vitu vya thamani akampa nduguye na mamaye pia.[#Kut 3:22; 11:2; 12:35; 2 Nya 21:3; Ezr 1:6]

54Wakala, wakanywa, yeye na watu waliokuwa pamoja naye, nao wakakaa usiku. Wakaondoka asubuhi, naye akasema, Nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu.[#Mwa 24:56,59]

55Kaka yake na mama yake wakasema, Msichana na akae kwetu kama siku kumi, zisipungue, baadaye aende.

56Naye akawaambia, Msinikawilishe, mradi BWANA amefanikisha njia yangu; nipeni ruhusa niende kwa bwana wangu.[#Mwa 24:40]

57Wakasema, Na tumwite huyo msichana, tumwulize mwenyewe.

58Wakamwita Rebeka wakamwuliza, Je! Utakwenda na mtu huyu? Akasema, Nitakwenda.

59Ndipo wakampeleka Rebeka dada yao, na yaya wake, na mtumishi wa Abrahamu, na watu wake.[#Mwa 35:8]

60Wakambariki Rebeka, wakamwambia, Dada yetu, wewe uwe mama wa elfu kumi, mara elfu nyingi, na wazao wako waurithi mlango wa hao wawachukiao.[#Mwa 17:16; 22:17; Rut 4:11]

61Rebeka akaondoka na vijakazi wake, nao wakapanda juu ya ngamia, wakamfuata yule mtu. Naye huyo mtumishi akamchukua Rebeka akaenda zake.

62Basi Isaka alikuwa amekuja kwa njia ya Beer-lahai-roi, maana alikaa katika nchi ya kusini.[#Mwa 16:14; 25:11]

63Isaka akatoka ili kutafakari shambani wakati wa jioni; akainua macho yake, akaona, kuna ngamia wanakuja.[#Yos 1:8; Zab 1:2; Dan 6:10; Mt 6:5,6; Mk 1:35; Lk 5:16; Mdo 10:9]

64Rebeka akainua macho, naye alipomwona Isaka, alishuka juu ya ngamia.[#Yos 15:18; 1 Sam 25:23]

65Akamwambia mtumishi, Ni nani mtu huyu ajaye shambani kutulaki? Mtumishi akasema, Huyu ndiye bwana wangu. Basi akatwaa shela yake akajifunika.[#1 Kor 11:3-10; 1 The 4:13]

66Yule mtumishi akamwambia Isaka mambo yote aliyoyatenda.

67Isaka akamwingiza Rebeka katika hema ya mama yake, Sara, akamtwaa Rebeka, akawa mkewe, akampenda; Isaka akafarijika kwa ajili ya kufa kwa mama yake.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya