Habakuki 3

Habakuki 3

Ombi la nabii

1Sala ya nabii Habakuki.[#3:1 iliyoimbwa kwa Shigionothi.]

2Ee BWANA, nimesikia habari zako, nami naogopa;

Ee BWANA, fufua kazi yako katikati ya miaka;

Katikati ya miaka tangaza habari yake;

Katika ghadhabu kumbuka rehema.

3Mungu alikuja kutoka Temani,

Yeye aliye mtakatifu kutoka mlima Parani.

Utukufu wake ukazifunika mbingu,

Nayo dunia ikajaa sifa yake.

4Mwangaza wake ulikuwa kama nuru;

Alikuwa na mishale ya nuru ubavuni pake;

Ndipo ulipofichwa uweza wake.

5Mbele zake ilikwenda tauni,

Na makaa ya moto yakatoka miguuni pake.

6Akasimama na kuitikisa dunia;[#Kut 23:31; Kum 32:8; Hes 21:24,34]

Akatazama, mataifa yakatetemeka;

Na milima ya zamani ikatawanyika;

Vilima vya kale vikainama;

Miendo yake ilikuwa kama siku za kale.

7Niliziona hema za Kushani zikitaabika;

Mapazia ya nchi ya Midiani yakatetemeka.

8Je! BWANA aliikasirikia mito?[#Kut 14:21,22]

Je! Hasira yako ilikuwa juu ya mito,

Au ghadhabu yako juu ya bahari,

Hata ukapanda farasi wako,

Katika magari yako ya wokovu?

9Uta wako ukafanywa wazi kabisa;

Viapo walivyopewa kabila vilikuwa neno thabiti;

Ukaipasua nchi kwa mito.

10Milima ilikuona, ikaogopa;

Gharika ya maji ikapita;

Vilindi vikatoa sauti yake,

Vikainua juu mikono yake.

11Jua na mwezi vikasimama makaoni mwao;

Mbele ya nuru ya mishale yako ilipotapakaa,

Mbele ya mwangaza wa mkuki wako umeremetao.

12Ulikwenda katikati ya nchi kwa ghadhabu;[#Zab 44:2,3; Mik 4:13]

Ukawapura mataifa kwa hasira.

13Ukatokea kwa ajili ya wokovu wa watu wako,[#2 Sam 5:20]

Kwa ajili ya wokovu wa masihi wako;

Ukakiponda kichwa cha nyumba ya waovu,

Ukiuweka wazi msingi hata mwambani.

14Ukakichoma kichwa cha mashujaa wake kwa fimbo zao wenyewe;

Wakaja kama kisulisuli ili kunitawanya;

Kama wakifurahi kuwameza maskini kwa siri.

15Ukaikanyaga bahari kwa farasi wako,

Chungu ya maji yenye nguvu.

16Nikasikia, na tumbo langu likatetemeka,

Midomo yangu ikatikisika kwa sauti ile;

Ubovu ukaingia mifupani mwangu,

Nikatetemeka katika mahali pangu;

Ili nipate kuingoja ile siku ya dhiki,

Kundi lao washambuliao wakweapo juu ya watu.

Imani na shangwe katika shida

17Maana mtini hautachanua maua,[#2 Kor 4:8,9]

Wala mizabibuni hamtakuwa na matunda;

Taabu ya mzeituni itakuwa bure,

Na mashamba hayatatoa chakula;

Zizini hamtakuwa na kundi,

Wala vibandani hamtakuwa na kundi la ng'ombe;

18Walakini nitamfurahia BWANA[#Zab 42:5; Isa 61:10]

Nitamshangilia Mungu wa wokovu wangu.

19MUNGU, aliye BWANA, ni nguvu zangu,[#2 Sam 22:34; Zab 18:33; 27:1]

Yeye huifanya miguu yangu kuwa kama ya kulungu,

Naye ataniendesha katika mahali pangu palipoinuka.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya