Isaya 52

Isaya 52

Sayuni ishangilie

1Amka, amka, jivike nguvu zako, Ee Sayuni;[#Nah 1:15; Isa 26:2; Ufu 21:2,27]

Jivike mavazi yako mazuri,

Ee Yerusalemu, mji mtakatifu;

Kwa maana tokea sasa hataingia ndani yako

Asiyetahiriwa, wala aliye najisi.

2Jikung'ute mavumbi; uondoke,[#Zek 2:7]

Uketi, Ee Yerusalemu;

Jifungue vifungo vya shingo yako,

Ee binti Sayuni uliyefungwa.

3Maana BWANA asema hivi, Mliuzwa bure; nanyi mtakombolewa bila fedha.[#Zab 44:12; 1 Pet 1:18]

4Maana Bwana MUNGU asema hivi, Watu wangu hapo kwanza walishuka Misri ili wakae huko kama wageni; na Mwashuri akawaonea bila sababu.

5Basi sasa, nafanya nini hapa, asema BWANA, ikiwa watu wangu wamechukuliwa bure? Hao wanaowatawala wanapiga yowe, asema BWANA, na jina langu linatukanwa daima mchana kutwa.[#Rum 2:24]

6Kwa hiyo watu wangu watalijua jina langu kwa hiyo watajua siku ile ya kuwa mimi ndimi ninenaye; tazama ni mimi.

7Jinsi ilivyo mizuri juu ya milima[#Nah 1:15; Rum 10:15; Efe 6:15]

Miguu yake aletaye habari njema,

Yeye aitangazaye amani,

Aletaye habari njema ya mambo mema,

Yeye autangazaye wokovu,

Auambiaye Sayuni, Mungu wako anamiliki!

8Sauti ya walinzi wako![#Sef 3:9]

Wanapaza sauti zao, wanaimba pamoja;

Maana wataona jicho kwa jicho,

Jinsi BWANA arejeavyo Sayuni.

9Pigeni kelele za furaha, imbeni pamoja,

Enyi mahali pa Yerusalemu palipokuwa ukiwa;

Kwa kuwa BWANA amewafariji watu wake,

Ameukomboa Yerusalemu.

10BWANA ameweka wazi mkono wake mtakatifu[#Lk 3:6]

Machoni pa mataifa yote;

Na ncha zote za dunia

Zitauona wokovu wa Mungu wetu.

11Nendeni zenu, nendeni zenu, tokeni huko, msiguse kitu kichafu; tokeni kati yake; iweni safi ninyi mnaochukua vyombo vya BWANA.[#Yer 50:8; Ufu 18:4; 2 Kor 6:17]

12Maana hamtatoka kwa haraka, wala hamtakwenda kwa kukimbia, kwa sababu BWANA atawatangulia; na Mungu wa Israeli atawafuata nyuma; awalinde.[#Kut 12:33; 14:19; Mik 2:13; Hes 10:25]

Mtumishi atesekaye

13Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa busara, atatukuzwa, na kuinuliwa juu, naye atakuwa juu sana.[#Isa 42:1; Flp 2:9]

14Kama vile wengi walivyokustaajabia, (uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu yeyote, na umbo lake zaidi ya wanadamu),[#Zab 22:6; Isa 53:3]

15ndivyo atakavyowastusha mataifa mengi; wafalme watamfumbia vinywa vyao; maana mambo wasiyoambiwa watayaona; na mambo wasiyoyasikia watayafahamu.[#Eze 36:25; Mdo 2:33; Ebr 9:13; Efe 3:5; Rum 15:21]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya