Isaya 56

Isaya 56

Agano kuwafikia watiifu wote

1BWANA asema hivi, Shikeni hukumu, mkatende haki; kwa maana wokovu wangu uko karibu kuja, na haki yangu kufunuliwa.[#Mt 3:2; Rum 13:11]

2Heri afanyaye haya, na mwanadamu ayashikaye sana; azishikaye sabato asizivunje, auzuiaye mkono wake usifanye uovu wowote.[#Kut 20:11; Isa 58:13]

3Wala mgeni, aambatanaye na BWANA, asiseme hivi, Hakika yake BWANA atanitenga na watu wake; wala towashi asiseme, Mimi ni mti mkavu.[#Kum 23:1; Mdo 8:27; 1 Pet 1:1]

4Kwa maana BWANA awaambia hivi matowashi, wanaozishika sabato zangu, na kuyachagua mambo yanipendezayo, na kulishika sana agano langu;

5Nitawapa hawa nyumbani mwangu, na ndani ya kuta zangu, kumbukumbu na jina, lililo jema kuliko kuwa na watoto wa kiume na wa kike; nitawapa jina lidumulo milele, lisilokatiliwa mbali.[#Efe 2:22; 1 Tim 3:15; Ebr 3:6; Yn 1:12; Ufu 3:12]

6Na wageni, walioandamana na BWANA ili wamhudumu, na kulipenda jina la BWANA, kuwa watumishi wake; kila aishikaye sabato asiivunje, na kulishika sana agano langu;

7Nitawaleta hao nao hadi katika mlima wangu mtakatifu, na kuwafurahisha katika nyumba yangu ya sala; makafara yao na dhabihu zao zitakubaliwa juu ya madhabahu zangu; kwa maana nyumba yangu itaitwa nyumba ya sala kwa mataifa yote.[#1 Pet 1:1; 2:5; Zab 4:5; Mal 1:11; Rum 12:1; Ebr 13:15; Mt 21:13; Mk 11:17; Lk 19:46]

8Bwana MUNGU, akusanyaye waliofukuzwa katika Israeli asema, Pamoja na hayo nitamkusanyia na wengine, zaidi ya hao walio wake waliokusanywa.[#Mwa 49:10; Isa 43:6; Efe 1:10]

Ufisadi wa watawala wa Israeli

9Enyi wanyama wote wa porini njoni

Mle, enyi wanyama wote wa porini.

10Walinzi wake ni vipofu, wote pia hawana maarifa; wote ni mbwa walio bubu, hawawezi kulia; huota ndoto, hulala, hupenda usingizi.[#Mt 15:14; Flp 3:2]

11Naam, mbwa hao wana uchu sana, hawashibi kamwe; na hao ni wachungaji wasioweza kufahamu neno; wote pia wamegeuka upande, wazifuate njia zao wenyewe, kila mmoja kwa faida yake, toka pande zote.

12Husema,

Njooni, nitaleta divai,

Na tunywe sana kileo;

Na kesho itakuwa kama leo,

Sikukuu kupita kiasi.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya