Ayubu 24

Ayubu 24

Ayubu alalamikia udhalimu duniani

1Mbona nyakati zisiwekwe na Mwenyezi?[#Mdo 1:7]

Na hao wamjuao mbona hawazioni siku zake?

2Wako waziondoao alama za mipaka;[#Kum 19:14]

Huyachukua makundi na kuyalisha.

3Huwanyang'anya yatima punda wao,[#Kum 24:6,10,12,17]

Humtwaa rehani ng'ombe wake mwanamke mjane.

4Humgeuza mhitaji aiache njia;[#Mit 28:28]

Maskini wa nchi hujificha pamoja.

5Tazama, kama punda mwitu jangwani

Wao hutoka kwenda kazini mwao, wakitafuta chakula kwa bidii;

Jangwa huwapa chakula cha watoto wao.

6Hukata nafaka zao mashambani;

Na kuokota zabibu za waovu.

7Hujilaza usiku kucha uchi bila nguo,[#Kut 22:26; Kum 24:12; Isa 58:7]

Wala hawana cha kujifunika baridi.

8Hutota kwa manyunyu ya milimani,[#Omb 4:5]

Na kugandamania kwa jabali ili kujikinga,

9Wako wamwondoao matitini kwa nguvu huyo asiye na baba,

Na kutwaa rehani kwa maskini;

10Hata wazunguke uchi bila mavazi,

Nao wakiwa na njaa huchukua miganda;

11Hushindika mafuta ndani ya kuta za watu hao;

Wakanyaga mashinikizo, nao wana kiu.

12Watu huugua toka mji ulio na watu wengi,[#Mhu 8:11]

Na roho yake aliyejeruhiwa hupiga ukelele;

Wala Mungu hauangalii upumbavu.

13Hawa ni katika hao waliouasi mwanga;

Hawazijui njia zake,

Wala hawakai katika mapito yake.

14Mwuaji huamka asubuhi kukipambazuka, huwaua maskini na wahitaji;

Tena wakati wa usiku yu kama mwizi.

15Tena jicho lake mzinifu hungojea wakati wa gizagiza,

Akisema, Hapana jicho litakaloniona;

Naye huuficha uso wake.

16Wao hutoboa nyumba gizani;[#Yn 3:20]

Hujifungia ndani wakati wa mchana;

Hawaujui mwanga.

17Maana asubuhi kwao wote ni kama giza tupu;

Maana wao wavijua vitisho vya hiyo giza tupu.

18Mwasema, Yeye ni mwepesi juu ya uso wa gharika;

Sehemu yao inalaaniwa duniani;

Hageuki kwenda njia ya mizabibuni.

19Ukame na joto hukausha maji ya theluji;

Kama kuzimu kuwafanyavyo watenda dhambi.

20Tumbo lililomzaa litamsahau; buu litamla na kuona tamu;[#Mit 10:7]

Hatakumbukwa tena;

Na udhalimu utavunjwa kama mti.

21Naam, yeye huwala walio tasa wasiozaa;

Wala hamtendei mema mwanamke mjane.

22Lakini Mungu huwadumisha wenye uwezo kwa nguvu zake;

Huinuka, wasiokuwa na tumaini la kuishi.

23Huwapa usalama, nao wapumzika kwao;

Na macho yake yako juu ya njia zao.

24Wao wametukuzwa; lakini kitambo kidogo hutoweka;[#Zab 37:35,36]

Naam, hushushwa, na kuondolewa njiani kama wengine wote,

Nao hukatwa kama vile masuke ya ngano.

25Na kama sivyo sasa, ni nani atakayenihukumu mimi kuwa ni mwongo,

Na kuyafanya maneno yangu kuwa si kitu?

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya