Ayubu 3

Ayubu 3

Ayubu ailaani siku aliyozaliwa

1Baada ya hayo Ayubu akafunua kinywa chake, na kuilaani siku yake.[#Yer 20:14-18; #3:1 siku ya kuzaliwa kwake. Katika Kiebrania ni siku yake.]

2Ayubu akajibu, na kusema;

3Na ipotelee mbali ile siku niliyozaliwa mimi,[#Ayu 10:18,19; Yer 15:10]

Na ule usiku uliosema,

Mtoto wa kiume ametungishwa mimba.

4Siku hiyo na iwe giza;

Mungu asiiangalie toka juu,

Wala mwanga usiiangazie.

5Ishikwe na giza, giza tupu, kuwa yake;[#Ayu 16:16; Zab 23:4; Isa 9:2; Yer 13:16; Mt 4:16; Lk 1:79]

Wingu na likae juu yake;

Chote kiifanyacho siku kuwa giza na kiitishe.

6Tena usiku huo, na ushikwe na giza kuu;

Usihesabiwe katika siku za mwaka;

Wala kutiwa katika hesabu ya miezi.

7Tazama, usiku huo na uwe tasa;

Wala isiwe ndani yake sauti ya shangwe.

8Na waulaani hao waulaanio mchana,[#Yer 9:17]

Hao walio tayari kumwamsha huyo Lewiathani.

9Nyota za mapambazuko yake na ziwe giza;

Na utafute mwanga lakini usiupate;

Wala usiyaone mapambazuko;

10Kwa sababu haukuifunga milango ya tumbo la mamangu.

Wala kunifichia taabu machoni.

11Mbona mimi sikufa wakati nikizaliwa?

Mbona nisitoe roho hapo nilipotoka tumboni?

12Mbona pawe na magoti ya kunipokea?

Au hayo maziwa, hata nikanyonya?

13Maana hapo ningelala na kutulia;

Ningelala usingizi; na kupata kupumzika;

14Pamoja na wafalme na washauri wa dunia,

Hao waliojijengea maganjoni;

15Au pamoja na wakuu wenye dhahabu,

Waliozijaza nyumba zao fedha;

16Au, mbona kuzikwa kama mimba iliyoharibika, nisingekuwako;

Kama wachanga wasiouona mwanga kabisa.

17Huko waovu huacha kusumbua;

Huko nako hao waliochoka wanapumzika.

18Huko wafungwa wanastarehe pamoja;

Hawaisikii sauti yake msimamizi.

19Wakuu na wadogo wako huko;

Mtumishi yuko huru kwa bwana wake.

20Mbona yeye aliye mashakani kupewa mwanga,[#Yer 20:18]

Na hao wenye uchungu rohoni kupewa uhai;

21Ambao wangojea mauti, lakini hawayapati;[#Ufu 9:6; Mit 2:4]

Na kuyachimbulia kuliko watafutavyo hazina iliyostirika;

22Ambao wafurahi mno,

Na kushangilia watakapoliona kaburi?

23Kwa nini mtu aliyezibiwa njia kupewa mwanga,[#Omb 3:7]

Ambaye Mungu amemzingira kwa ukigo?

24Kwani kuugua kwangu kwaja kana kwamba ni chakula,

Na kunguruma kwangu kumemiminika kama maji.

25Maana jambo hilo nichalo hunipata,

Nalo linitialo hofu hunijia.

26Mimi sioni raha, wala situlii, wala kupumzika;

Lakini taabu huja.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya