Ayubu 7

Ayubu 7

Ayubu: Mateso yangu hayana mwisho

1Je! Mtu hana huduma ngumu juu ya nchi?[#Ayu 14:5,13,14; Zab 39:4; Mhu 3:1,2]

Na siku zake, je! Si kama siku za mwajiriwa?

2Kama mtumishi atamaniye sana kile kivuli,

Kama mwajiriwa anayetazamia mshahara wake;

3Hivyo basi nami nimepewa miezi ya ubatili iwe fungu langu,[#Zab 39:5; Mhu 1:14]

Nami nimeandikiwa mateso usiku hata usiku.

4Hapo nilalapo chini, nasema,

Nitaondoka lini? Lakini usiku huwa mrefu;

Nami nimejawa na kujitupa huku na huku hata kupambazuke.

5Mwili wangu unavikwa mabuu na madongoa ya udongo;[#Ayu 17:14; Zab 38:5-7; Isa 1:6]

Ngozi yangu hufumba, kisha ikatumbuka tena.

6Siku zangu hupita upesi kuliko chombo cha kufumia,

Nazo zapita pasipokuwa na matumaini.

7Kumbuka ya kwamba maisha yangu ni upepo;[#Zab 78:39; Yak 4:14]

Jicho langu halitaona mema tena.

8Jicho lake huyo anionaye halitaniangalia tena;[#Ayu 20:9]

Macho yako yatanielekea, lakini sitakuwapo.

9Kama vile wingu likomavyo na kutoweka,[#2 Sam 12:23; Zab 39:13]

Ndivyo alivyo huyo ashukaye kuzimuni, hatazuka tena kabisa.

10Hatarudi tena nyumbani kwake,

Wala mahali pake hapatamjua tena.

11Kwa hiyo sitakizuia kinywa changu;[#Zab 39:1,9]

Nitanena kwa mateso ya roho yangu;

Nitalia kwa uchungu wa nafsi yangu.

12Je! Mimi ni bahari, au je! Ni nyangumi?

Hata ukawaweka walinzi juu yangu?

13Hapo nisemapo, kitanda changu kitanituliza moyo,

Malazi yangu yatanipunguzia kuugua kwangu;

14Ndipo unitishapo kwa ndoto,

Na kunitia hofu kwa maono;

15Hata nafsi yangu huchagua kunyongwa,

Na kuchagua kifo kuliko maumivu yangu haya.

16Ninadhoofika; sitaishi sikuzote;[#Mwa 27:46; Ayu 10:1; Zab 62:9; Mhu 6:11]

Usinisumbue, kwani siku zangu ni uvuvio.

17Je! Mtu ni kitu gani, hata ukamtukuza,[#Zab 8:4; 144:3; Ebr 2:6]

Na kumtia moyoni mwako,

18Na kumwangalia kila asubuhi,

Na kumjaribu kila dakika?

19Je! Hata lini hukomi kuniangalia;

Wala kunisumbua hata nimeze mate?

20Ikiwa nimefanya dhambi, nikufanyieje, Ee mlinda wanadamu?[#Zab 36:6]

Mbona umeniweka niwe shabaha yako,

Hata nimekuwa mzigo kwa nafsi yangu?

21Nawe, je! Mbona hunisamehe makosa yangu,

Na kuniondolea maovu yangu?

Kwa kuwa sasa nitalala mavumbini;

Nawe utanitafuta kwa bidii, lakini sitakuwapo.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya