Maombolezo 4

Maombolezo 4

Adhabu ya Sayuni

1Jinsi dhahabu ilivyoacha kung'aa,

Na dhahabu iliyo safi ilivyobadilika!

Mawe ya patakatifu yametupwa

Mwanzo wa kila njia.

2Wana wa Sayuni wenye thamani,[#2 Kor 4:7]

Walinganao na dhahabu safi,

Jinsi wanavyodhaniwa kuwa vyombo vya udongo,

Kazi ya mikono ya mfinyanzi!

3Hata mbwamwitu hutoa matiti,[#Ayu 39:14]

Huwanyonyesha watoto wao;

Binti ya watu wangu amekuwa mkali,

Mfano wa mbuni jangwani.

4Ulimi wa mtoto anyonyaye[#Zab 22:15]

Wagandamana na kinywa chake kwa kiu;

Watoto wachanga waomba chakula,

Wala hakuna hata mmoja awamegeaye.

5Wale waliokula vitu vya anasa[#Ayu 24:8; Lk 15:16]

Wameachwa peke yao njiani;

Wale waliokuzwa kuvaa nguo nyekundu

Wakumbatia jaa.

6Maana uovu wa binti ya watu wangu ni mkubwa[#Mwa 19:24]

Kuliko dhambi ya Sodoma,

Uliopinduliwa kama katika dakika moja,

Wala mikono haikuwekwa juu yake.

7Wakuu wake walikuwa safi kuliko theluji,

Walikuwa weupe kuliko maziwa;

Miili yao, walikuwa wekundu kuliko marijani,

Na umbo lao kama yakuti samawi.

8Nyuso zao ni nyeusi kuliko makaa;[#Zab 102:5]

Hawajulikani katika njia kuu;

Ngozi yao yagandamana na mifupa yao

Imekauka, imekuwa kama mti.

9Heri wale waliouawa kwa upanga

Kuliko wao waliouawa kwa njaa;

Maana hao husinyaa, wakichomwa

Kwa kukosa matunda ya mashamba.

10Mikono ya wanawake wenye huruma[#Omb 2:20; Kum 28:57; Eze 5:10]

Imewatokosa watoto wao wenyewe;

Walikuwa ndio chakula chao

Katika uharibifu wa binti ya watu wangu.

11BWANA ameitimiza ghadhabu yake,[#Kum 32:22]

Ameimimina hasira yake kali;

Naye amewasha moto katika Sayuni

Ulioiteketeza misingi yake.

12Wafalme wa dunia hawakusadiki,[#Kum 29:24]

Wala wote wakaao duniani,

Ya kwamba mtesi na adui wangeingia

Katika malango ya Yerusalemu.

13Ni kwa sababu ya dhambi za manabii wake[#Yer 5:31; Mt 23:31]

Na maovu ya makuhani wake,

Walioimwaga damu ya wenye haki

Katikati yake.

14Hutangatanga njiani kama vipofu,[#Yer 2:34]

Wametiwa unajisi kwa damu;

Hata ikawa hakuna aliyeweza

Kuyagusa mavazi yao.

15Watu waliwapigia kelele, Ondokeni, Uchafu,

Ondokeni, ondokeni, msiguse;

Walipokimbia na kutangatanga, watu walisema kati ya mataifa,

Hawatakaa hapa tena.

16Hasira ya BWANA imewatenga,[#Omb 5:12]

Yeye hatawaangalia tena;

Hawakujali nafsi za wale makuhani,

Hawakuwaheshimu wazee wao.

17Macho yetu yamechoka[#2 Fal 24:7; Isa 20:5,6]

Kwa kuutazamia bure msaada wetu;

Katika kungoja kwetu tumengojea taifa

Lisiloweza kutuokoa.

18Wanatuvizia hatua zetu,[#2 Fal 25:4; Yer 51:33]

Hata hatuwezi kwenda katika njia zetu;

Mwisho wetu umekaribia, siku zetu zimetimia;

Maana mwisho wetu umefika.

19Waliotufuatia ni wepesi

Kuliko tai za mbinguni;

Hao walitufuatia milimani,

Nao walituotea jangwani.

20Pumzi ya mianzi ya pua zetu, masihi wa BWANA,[#Mwa 2:7; Yer 52:9; #4:20 Au, mtiwa mafuta (tazama 1 Sam 2:10).]

Alikamatwa katika marima yao;

Ambaye kwa habari zake tulisema,

Chini ya kivuli chake tutakaa kati ya mataifa.

21Furahi, ushangilie, Ee binti Edomu,

Ukaaye katika nchi ya Usi;

Hata kwako kikombe kitapita,

Utalewa, na kujifanya uchi.

22Adhabu ya uovu wako imetimia, Ee binti Sayuni;

Hatakuhamisha tena;

Atapatiliza uovu wako, Ee binti Edomu;

Atazivumbua dhambi zako.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya