Mathayo 23

Mathayo 23

Yesu awakana Waandishi na Mafarisayo

1Kisha Yesu akawaambia makutano na wanafunzi wake, akasema,[#Mk 12:38-40; Lk 20:45-47; Lk 11:39-52]

2Waandishi na Mafarisayo wameketi katika kiti cha Musa;

3basi, yoyote watakayowaambia, myashike na kuyatenda; lakini kwa mfano wa matendo yao, msitende; maana wao hunena lakini hawatendi.[#Mal 2:7,8]

4Wao hufunga mizigo mizito na kuwatwika watu mabegani mwao; wasitake wenyewe kuigusa kwa kidole chao.

5Tena matendo yao yote huyatenda ili kutazamwa na watu; kwa kuwa hupanua hirizi zao, huongeza matamvua yao;[#Mt 6:1; Hes 15:38; Kum 6:8; Kut 13:9]

6hupenda viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi,[#Lk 14:7; Mt 6:5]

7na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi.

8Bali ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu.

9Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni.

10Wala msiitwe viongozi; maana Kiongozi wenu ni mmoja, naye ndiye Kristo.

11Naye aliye mkubwa wenu atakuwa mtumishi wenu.[#Mt 20:26-27; Mk 9:35; 10:43-44; Lk 22:26]

12Na yeyote atakayejikweza, atadhiliwa; na yeyote atakayejidhili, atakwezwa.[#Lk 14:11; 18:14; Mit 29:23; Ayu 22:29; Eze 21:26; 1 Pet 5:5]

13Ole wenu Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnawafungia watu ufalme wa mbinguni; ninyi wenyewe hamwingii, wala wanaoingia hamwaachi waingie.

14[Ole wenu Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnakula nyumba za wajane, na kwa unafiki mnasali sala ndefu; kwa hiyo mtapata hukumu iliyo kubwa zaidi.]

15Ole wenu Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu; na akiisha kufanyika, mnamfanya kuwa mwana wa Jehanamu mara mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe.

16Ole wenu viongozi vipofu, ninyi msemao, Mtu atakayeapa kwa hekalu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa dhahabu ya hekalu, amejifunga kwa kiapo.[#Mt 15:14]

17Wapumbavu ninyi na vipofu; maana ni ipi iliyo kubwa, ile dhahabu, au lile hekalu liitakasalo dhahabu?

18Tena, Mtu atakayeapa kwa madhabahu, si kitu; bali mtu atakayeapa kwa sadaka iliyo juu yake, amejifunga kwa kiapo.

19Vipofu ninyi; maana ni ipi iliyo kubwa, ile sadaka, au ile madhabahu iitakasayo sadaka?[#Kut 29:37]

20Basi yeye aapaye kwa madhabahu, huapa kwa hiyo, na kwa vitu vyote vilivyo juu yake.

21Naye aapaye kwa hekalu, huapa kwa hilo, na kwa yeye akaaye ndani yake.

22Naye aapaye kwa mbingu, huapa kwa kiti cha enzi cha Mungu, na kwa yeye aketiye juu yake.[#Isa 66:1; Mt 5:34]

23Ole wenu Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa, bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache.[#Law 27:30; Mik 6:8]

24Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia.

25Ole wenu Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano, na ndani yake vimejaa unyang'anyi na kutokuwa na kiasi.[#Mk 7:4]

26Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza ndani ya kikombe, ili nje yake nako kupate kuwa safi.[#Tit 1:15; Yn 9:40]

27Ole wenu, Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa chokaa, nayo kwa nje yaonekana kuwa mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na uchafu wote.[#Mdo 23:3]

28Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje mwaonekana na watu kuwa wenye haki, bali ndani mmejaa unafiki na maasi.[#Lk 16:15]

29Ole wenu, Waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnayajenga makaburi ya manabii, na kuyapamba maziara ya wenye haki,

30na kusema, Kama sisi tungalikuwako zamani za baba zetu, hatungalishirikiana nao katika damu ya manabii.

31Hivi mwajishuhudia wenyewe, ya kwamba ninyi ni wana wao waliowaua manabii.[#Mdo 7:52]

32Kijazeni basi kipimo cha baba zenu.

33Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya Jehanamu?[#Mt 3:7; 12:34; Lk 3:7]

34Kwa sababu hiyo, angalieni, mimi natuma kwenu manabii na wenye hekima na waandishi; na wengine wao ninyi mtawaua na kuwasulubisha, na wengine wao mtawapiga katika masinagogi yenu, na kuwafukuza mji kwa mji;[#Mt 13:52; 10:23; 1 The 2:15]

35hivyo ije juu yenu damu yote ya haki iliyomwagika juu ya nchi, tangu damu ya Habili, yule mwenye haki, hata damu ya Zakaria mwana wa Barakia, mliyemwua kati ya patakatifu na madhabahu.[#Mwa 4:8; 2 Nya 24:20-21]

36Amin, nawaambieni, Mambo hayo yote yatakuja juu ya kizazi hiki.

Maombolezo juu ya Yerusalemu

37Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku awakusanyavyo pamoja vifaranga wake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka![#Lk 13:34,35; Mdo 7:59; 1 The 2:15]

38Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.[#Yer 22:5; 12:7; 1 Fal 9:7,8]

39Kwa maana nawaambia, Hamtaniona kamwe tangu sasa, hadi mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana.[#Zab 118:26; Mt 21:9]

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya