Mithali 10

Mithali 10

KITABU CHA PILI

Mithali za Sulemani

1Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye;

Bali mwana mpumbavu ni mzigo wa mamaye.

2Hazina za uovu hazifaidii kitu;[#Zab 49:6; Lk 12:19; Dan 4:27]

Bali haki huokoa na mauti.

3BWANA hataiacha nafsi ya mwenye haki ife na njaa;[#Zab 10:14]

Bali tamaa ya mtu mwovu huisukumia mbali.

4Atendaye mambo kwa mkono mlegevu huwa maskini;[#Mit 13:4]

Bali mkono wake aliye na bidii hutajirisha.

5Akusanyaye wakati wa joto ni mwana mwenye hekima;

Bali asinziaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha.

6Baraka humkalia mwenye haki kichwani;[#Est 7:8]

Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu.

7Kuwakumbuka wenye haki huwa na baraka;[#Zab 9:5,6; Mhu 8:10]

Bali jina la mtu mwovu litaoza.

8Aliye na akili moyoni mwake atapokea agizo;

Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.

9Aendaye kwa unyofu huenda salama;[#Zab 23:4; Isa 33:15,16]

Bali apotoshaye njia zake atajulikana.

10Akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko;

Bali mpumbavu mwenye maneno mengi ataanguka.

11Kinywa chake mwenye haki ni chemchemi ya uzima;[#Zab 37:30; 107:42]

Bali jeuri hufunika kinywa chake mtu mwovu,

12Kuchukiana huleta fitina;[#Yak 5:20; 1 Pet 4:8; 1 Kor 13:4]

Bali kupendana husitiri makosa yote.

13Hekima hupatikana midomoni mwa mwenye ufahamu;[#Lk 4:22]

Bali fimbo hufaa kwa mgongo wake asiye na ufahamu.

14Watu wenye akili huweka akiba ya maarifa;

Bali kinywa cha mpumbavu ni uangamivu ulio karibu.

15Mali ya tajiri ndio ngome yake;[#Ayu 31:24; Mit 18:11; Lk 12:19; 1 Tim 6:17]

Ufukara wa maskini ndio umwangamizao.

16Kazi yake mwenye haki huuelekea uzima;

Mazao ya wabaya huielekea dhambi.

17Akubaliye kurudiwa huwa katika njia ya uzima;

Bali yeye aachaye maonyo hukosa.

18Yeye afichaye chuki ana midomo ya uongo,

Na yeye asingiziaye ni mpumbavu.

19Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na maovu;[#Mhu 5:3; Zab 39:1; Mit 17:27,28; Yak 1:19]

Bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili.

20Ulimi wa mwenye haki ni kama fedha safi;

Moyo wa mtu mbaya haufai kitu.

21Midomo ya mwenye haki hulisha watu wengi;

Bali wapumbavu hufa kwa kuwa hawana ufahamu.

22Baraka ya BWANA hutajirisha,[#Mwa 12:2; Kum 8:17,18; 1 Sam 2:7,8; 1 Tim 4:8]

Wala hachanganyi huzuni nayo.

23Kwa mpumbavu kutenda maovu ni kama mchezo;

Bali mtu mwenye ufahamu ana hekima.

24Aogopacho mtu asiye haki ndicho kitakachomjilia;[#Ayu 15:21; Mt 5:6]

Na wenye haki watapewa matakwa yao.

25Kisulisuli kikiisha pita asiye haki hayuko tena;[#Zab 15:5; Mt 7:24; 1 Tim 6:19]

Bali mwenye haki ni msingi wa milele.

26Kama siki menoni, na kama moshi machoni,

Ndivyo alivyo mtu mvivu kwa hao waliomwajiri.

27Kumcha BWANA kwaongeza siku za mtu;[#Mhu 7:17]

Bali miaka yao wasio haki itapunguzwa.

28Matumaini yao wenye haki yatakuwa furaha;[#Zab 16:9; Rum 5:2; Ayu 8:13]

Bali matarajio yao wasio haki yatapotea.

29Njia ya BWANA ni kimbilio lake mtu mkamilifu;[#Zek 10:12; Flp 4:13; Isa 40:31; Zab 1:6]

Bali ni uharibifu kwao watendao maovu.

30Mwenye haki hataondolewa milele;

Bali wasio haki hawatakaa katika nchi.

31Kinywa cha mwenye haki hutoa hekima;

Bali ulimi wa ukaidi utakatiliwa mbali.

32Midomo ya mwenye haki huyajua yatakayokubaliwa;

Bali kinywa chao wasio haki hunena ukaidi.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya