Zaburi 116

Zaburi 116

Shukrani kwa kuponywa maradhi

1Haleluya.

Nampenda BWANA kwa kuwa anaisikiliza

Sauti yangu na dua zangu.

2Kwa maana amenitegea sikio lake,

Kwa hiyo nitamwita siku zangu zote.

3Kamba za mauti zilinizunguka,

Shida za kuzimu zilinipata.

Nilipata dhiki na mateso;

4Nikaliitia jina la BWANA.

Ee BWANA, nakuomba sana,

Uniokoe nafsi yangu.

5BWANA ni mwenye neema na haki,[#Ezr 9:15; Neh 9:8; Zab 11:7; Yer 12:1; Omb 1:18; Ufu 16:5]

Naam, Mungu wetu ni mwenye rehema.

6BWANA huwalinda wasio na hila;

Nilidhilika, akaniokoa.

7Ee nafsi yangu, urudi pumzikoni mwako,[#Yer 6:16; Mt 11:29]

Kwa kuwa BWANA amekutendea ukarimu.

8Maana umeniponya nafsi yangu na mauti,

Macho yangu na machozi,

Na miguu yangu na kuanguka.

9Nitaenenda mbele za BWANA

Katika nchi za walio hai.

10Nilidumisha imani yangu, hata niliposema,[#2 Kor 4:13]

Mimi nateseka sana.

11Nikiwa katika hangaiko langu nikasema,[#2 Fal 4:16; Yer 9:5; Rum 3:4]

Wanadamu wote ni waongo.

12Nimrudishie BWANA nini

Kwa ukarimu wake wote alionitendea?

13Nitakipokea kikombe cha wokovu;

Na kulitangaza jina la BWANA;

14Nitaziondoa nadhiri zangu kwa BWANA,[#Zab 22:25; Yon 2:6]

Naam, mbele ya watu wake wote.

15Kifo cha waaminifu wa Mungu,[#Ayu 5:26; Zab 72:14; Lk 16:22; Ufu 14:13]

kina thamani machoni pa BWANA.

16Ee BWANA, hakika mimi ni mtumishi wako,

Mtumishi wako, mwana wa mjakazi wako,

Umevifungua vifungo vyangu.

17Nitakutolea dhabihu ya kushukuru;

Na kulitangaza jina la BWANA;

18Nitaziondoa nadhiri zangu kwa BWANA,

Naam, mbele ya watu wake wote.

19Katika nyua za nyumba ya BWANA,

Ndani yako, Ee Yerusalemu.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya