Zaburi 148

Zaburi 148

Sifa kwa utukufu mkuu wa Mungu

1Haleluya.

Msifuni BWANA kutoka mbinguni;

Msifuni katika mahali palipo juu.

2Msifuni, enyi malaika wake wote;[#Dan 7:10; Ebr 1:7]

Msifuni, majeshi yake yote.

3Msifuni, jua na mwezi;

Msifuni, nyota zote zenye mwanga.

4Msifuni, enyi mbingu za mbingu,[#1 Fal 8:27]

Nanyi maji mlioko juu ya mbingu.

5Na vilisifu jina la BWANA,[#Ebr 11:3]

Kwa maana aliamuru, vikaumbwa.

6Amevithibitisha hata milele na milele,[#Yer 33:25]

Ametoa amri wala haitapita.

7Msifuni BWANA kutoka nchi,[#Isa 43:20]

Enyi nyangumi na vilindi vyote.

8Moto na mvua ya mawe, theluji na mvuke,

Upepo wa dhoruba utimizao neno lake.

9Milima na vilima vyote,[#Isa 49:13]

Miti yenye matunda na mierezi yote.

10Hayawani, na wanyama wafugwao,

Vitambaavyo, na ndege wenye mbawa.

11Wafalme wa dunia, na watu wote,[#Mdo 17:28]

Wakuu, na watawala wote wa dunia.

12Vijana wa kiume, na wanawali,

Wazee, na watoto;

13Na walisifu jina la BWANA,[#Isa 6:3; Flp 2:9]

Maana jina lake peke yake limetukuka;

Adhama yake i juu ya nchi na mbingu.

14Naye amewainulia watu wake pembe,[#Efe 2:17; 1 Pet 2:9]

Sifa za watauwa wake wote;

Wana wa Israeli, watu walio karibu naye.

Haleluya.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya