Zaburi 52

Zaburi 52

Hukumu kwa waongo

1Kwa nini kujisifia uovu, Ewe jabari?[#1 Sam 22:9-10; 21:7]

Wema wa Mungu upo sikuzote.

2Ulimi wako watunga madhara,[#Zab 50:19; Mit 12:18; Zab 59:7]

Kama wembe mkali, Ewe mwenye hila.

3Umependa mabaya kuliko mema,[#Yer 9:4]

Na uongo kuliko kusema kweli.

4Umependa maneno yote ya kupoteza watu,

Ewe ulimi wenye hila.

5Lakini Mungu atakuharibu hata milele;[#Mit 2:22]

Atakuondolea mbali;

Atakunyakua hemani mwako;

Atakung'oa katika nchi ya walio hai.

6Nao wenye haki wataona;[#Ayu 22:19; Zab 58:10]

Wataingiwa na hofu na kumcheka;

7Kumbe! Huyu ndiye mtu yule,[#Ayu 31:24,25; Zab 49:6]

Asiyemfanya Mungu kuwa kimbilio lake.

Aliutumainia wingi wa mali zake,

Na kufanya mali kimbilio lake.

8Bali mimi ni kama mzeituni[#Zab 92:13]

Umeao katika nyumba ya Mungu.

Nazitumainia fadhili za Mungu milele na milele.

9Nitakushukuru milele kwa maana umetenda;[#Zab 54:6]

Nitalingojea jina lako kwa kuwa ni jema;

Mbele ya wacha Mungu wako.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya