Yoshua Mwana wa Sira 26

Yoshua Mwana wa Sira 26

Furaha ya Mke Mwema

1Bali yu heri mumewe akipata mke mwema, hata jumla ya siku zake zitakuwa maradufu.

2Mwanamke hodari humfurahisha mumewe, naye ataitimiza miaka yake katika amani.

3Mke mwema ndiye tunu bora, mcha BWANA atatunukiwa huyo kifuani pake.

4Kwamba mtu ni tajiri au kwamba ni maskini, moyo mwema humwia sikuzote uso wa kuchangamka.

Maovu ya Hali ya Juu: Mke Mwovu

5Mambo matatu moyo wangu uliogopa,

Na la nne niliona hofu nyingi;

Masingizio ya mjini,

Na umati wa watu wengi,

Na msuto wa uongo,

hayo yote ni magumu kuliko mauti.

6Aidha, mwanamke amwoneaye wivu mwanamke mwingine ni huzuni ya moyo na simanzi hasa, tena msiba mkuu wa mke mwenye maneno mengi ndio upitao mambo yote pamoja.

7Mwanamke mbaya

Ni kama nira ngumu;

Amshikaye ni kama ashikaye nge.

8Mwanamke mlevi

Huchochea ugomvi;

Asitake kuificha fedheha yake.

9Mwanamke malaya

Huinua macho yake;

Utamtambua pote kwa kope zake.

10Mlinde sana binti aliye mshupavu,

Asijipatie uhuru na kuutumia;

11Mwangalie vema aliye mkavu wa macho,

Wala usisituke akikukosa.

12Atafumbua kinywa kama msafiri mwenye kiu,

Na kunywa maji yoyote yaliyo karibu;

Penye kila kituo atakaa kitako,

Alifungue podo lake kwa kila mshale.

Baraka ya Mke Mwema

13Mke mwenye neema

Humpendeza mumewe;

Na maarifa yake yatamnenepesha.

14Mwanamke mtulivu

Ni tunu ya BWANA;

15Wala hakuna badala ya mtaalamu.

Mwanamke mwenye haya

Ni neema juu ya neema;

Tena roho ya utauwa haina bei.

16Kama lilivyo jua kunapopambazuka

Katika mahali pa BWANA palipo juu sana.

Ndivyo ulivyo uzuri wa mke mwema

Katika madaraka ya nyumbani mwake.

17Taa ing'aavyo juu ya kinara kitakatifu,

Kadhalika uzuri wa uso katika uzee;

18-19-20-21-22-23-24-25-26-27Nguzo za dhahabu juu ya kiako cha fedha,

Ni miguu mizuri juu ya nyayo imara.

Vitu Vitatu vihuzunishavyo

28Kwa mambo mawili moyo wangu una huzuni,

Na kwa la tatu hasira imeniingilia;

Askari mwenye taabu ya ukata,

Wenye elimu waliodharauliwa,

Naye aliyerudi nyuma toka haki hata dhambi.

Huyo hakika BWANA atamwekea tayari upanga wake.

Majaribu ya Biashara

29Kwa shida tajiri atajilinda na uovu,

Wala mfanya bishara hataepuka dhambi.

Swahili Revised Union Version Bible © Bible Society of Kenya, and Bible Society of Tanzania, 2005.
Published by: Bible Society of Kenya