The chat will start when you send the first message.
1Paulo, na Silwano, na Timotheo, kwa kanisa la Wathesalonike, lililo katika Mungu Baba, na katika Bwana Yesu Kristo. Neema na iwe kwenu na amani.[#Mdo 17:1; 15:40; 2 The 1:1]
2Twamshukuru Mungu siku zote kwa ajili yenu nyote, tukiwataja katika maombi yetu.[#2 The 1:11]
3Wala hatuachi kuikumbuka kazi yenu ya imani, na taabu yenu ya upendo, na saburi yenu ya tumaini lililo katika Bwana wetu Yesu Kristo, mbele za Mungu Baba yetu.[#1 Kor 13:13; Kol 1:4,5]
4Kwa maana, ndugu mnaopendwa na Mungu, twajua uteule wenu;
5ya kwamba injili yetu haikuwafikia katika maneno tu, bali na katika nguvu, na katika Roho Mtakatifu, na uthibitifu mwingi; kama vile mnavyojua jinsi zilivyokuwa tabia zetu kwenu, kwa ajili yenu.[#1 Kor 2:5]
6Nanyi mkawa wafuasi wetu na wa Bwana, mkiisha kulipokea neno katika dhiki nyingi, pamoja na furaha ya Roho Mtakatifu.[#Mdo 17:5-9; 13:52; 1 Kor 4:16; 2 The 3:9]
7Hata mkawa kielelezo kwa watu wote waaminio katika Makedonia, na katika Akaya.[#1 The 4:10; Flp 3:7; 1 Pet 5:3]
8Maana kutoka kwenu neno la Mungu limevuma, si katika Makedonia na Akaya tu, ila na kila mahali imani yenu mliyo nayo kwa Mungu imeenea; hata hatuna haja sisi kunena lo lote.[#Rum 1:8]
9Kwa kuwa wao wenyewe wanatangaza habari zetu, jinsi kulivyokuwa kuingia kwetu kwenu; na jinsi mlivyomgeukia Mungu mkaziacha sanamu, ili kumtumikia Mungu aliye hai, wa kweli;[#Mdo 14:15; Yn 17:3; 1 Kor 12:2]
10na kumngojea Mwanawe kutoka mbinguni, ambaye alimfufua katika wafu, naye ni Yesu, mwenye kutuokoa na ghadhabu itakayokuja.[#1 The 5:9; Tit 2:13; Mdo 17:31]