2 Tim 4

2 Tim 4

1Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake;[#Mdo 10:42; 1 Pet 4:5; Rum 14:9,10]

2lihubiri neno, uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho.[#Mdo 20:20,31]

3Maana utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti;[#2 Tim 1:13; 1 Tim 4:1]

4nao watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo.[#1 Tim 4:7; 2 The 2:11]

5Bali wewe, uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili, timiliza huduma yako.[#2 Tim 2:3; Efe 4:11]

6Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika.[#Flp 2:17]

7Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;[#1 Kor 9:25; 1 Tim 6:12; Flp 3:14]

8baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.[#2 Tim 2:5; Yn 1:22; 1 Pet 5:4; Ufu 2:10]

Maagizo ya Kibinafsi

9Jitahidi kuja kwangu upesi.[#2 Tim 1:4]

10Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia.[#2 Kor 8:23; Gal 2:3; Kol 4:14; Tit 1:4; Flm 1:24]

11Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi.[#Mdo 12:12,25; 13:13; 15:37-39; Kol 4:10,14; Flm 1:24]

12Lakini Tikiko nalimpeleka Efeso.[#Mdo 20:4; Efe 6:21-22; Kol 4:7-8]

13Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu, hasa vile vya ngozi.[#Mdo 20:6]

14Iskanda, mfua shaba, alionyesha ubaya mwingi kwangu; Bwana atamlipa sawasawa na matendo yake.[#Zab 28:4; 62:12; Mit 24:12; Rum 2:6; 1 Tim 1:20; 2 Sam 3:39]

15Nawe ujihadhari na huyo, kwa sababu aliyapinga sana maneno yetu.

16Katika jawabu langu la kwanza hakuna mtu aliyesimama upande wangu, bali wote waliniacha; naomba wasihesabiwe hatia kwa jambo hilo.[#2 Tim 1:15]

17Lakini Bwana alisimama pamoja nami akanitia nguvu, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie Mataifa yote; nami nikaokolewa katika kinywa cha simba.[#Zab 22:21; Dan 6:21,28; Mdo 23:11; 27:23]

18Bwana ataniokoa na kila neno baya, na kunihifadhi hata nifike ufalme wake wa mbinguni. Utukufu una Yeye milele na milele. Amina.

Salamu za Mwisho na Baraka

19Nisalimie Priska na Akila, na wale wa nyumbani mwa Onesiforo.[#Mdo 18:2; 2 Tim 1:16-17]

20Erasto alikaa Korintho. Trofimo nalimwacha huko Mileto, hawezi.[#Mdo 19:22; 20:4; 21:29; Rum 16:23]

21Jitahidi kuja kabla ya wakati wa baridi. Eubulo akusalimu, na Pude, na Lino, na Klaudia, na ndugu wote pia.

22Bwana na awe pamoja na roho yako. Neema na iwe pamoja nanyi.

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania