Omb 1

Omb 1

Mji Uliohamwa

1Jinsi mji huu ukaavyo ukiwa,[#Isa 47:7; Omb 1:9; Ezr 4:20]

Huo uliokuwa umejaa watu!

Jinsi alivyokuwa kama mjane,

Yeye aliyekuwa mkuu kati ya mataifa!

Binti mfalme kati ya majimbo,

Jinsi alivyoshikwa shokoa!

2Hulia sana wakati wa usiku,[#Yer 13:17; Omb 1:16; Ayu 7:3; Zab 6:6; Yer 4:30]

Na machozi yake yapo mashavuni;

Miongoni mwa wote waliompenda

Hakuna hata mmoja amfarijiye;

Rafiki zake wote wamemtenda hila,

Wamekuwa adui zake.

3Yuda amehamishwa kwa sababu ya kuonewa,[#Law 26:14,32,33; Kum 28:64]

Na kwa sababu ya utumwa mkuu;

Anakaa kati ya makafiri,

Haoni raha iwayo yote;

Wote waliomfuata wamempata

Katika dhiki yake.

4Njia za Sayuni zaomboleza,

Kwa kuwa hakuna ajaye kwa sikukuu;

Malango yake yote yamekuwa ukiwa,

Makuhani wake hupiga kite;

Wanawali wake wanahuzunika;

Na yeye mwenyewe huona uchungu.

5Watesi wake wamekuwa kichwa,[#Yer 30:14; Omb 3:39]

Adui zake hufanikiwa;

Kwa kuwa BWANA amemtesa

Kwa sababu ya wingi wa makosa yake;

Watoto wake wadogo wamechukuliwa mateka

Mbele yake huyo mtesi.

6Naye huyo binti Sayuni

Enzi yake yote imemwacha;

Wakuu wake wamekuwa kama ayala

Wasioona malisho;

Nao wamekwenda zao hawana nguvu

Mbele yake anayewafuatia.

7Siku za mateso na misiba yake,[#Mik 4:11]

Yerusalemu huyakumbuka matamaniko yake yote

Yaliyokuwa tangu siku za kale;

Hapo watu wake walipoanguka mikononi mwa mtesi,

Wala hakuna hata mmoja wa kumsaidia;

Hao watesi wake walimwona,

Wakafanya sabato zake kuwa mzaha.

8Yerusalemu amefanya dhambi sana;[#Yer 13:22]

Kwa hiyo amekuwa kama kitu kichafu;

Wote waliomheshimu wanamdharau,

Kwa sababu wameuona uchi wake;

Naam, yeye anaugua,

Na kujigeuza aende nyuma.

9Uchafu wake ulikuwa katika marinda yake;[#Kum 32:29]

Hakukumbuka mwisho wake;

Kwa hiyo ameshuka kwa ajabu;

Yeye hana mtu wa kumfariji;

Tazama, BWANA, teso langu;

Maana huyo adui amejitukuza.

10Huyo mtesi amenyosha mkono wake[#Kum 23:3; Neh 13:1]

Juu ya matamaniko yake yote;

Maana ameona ya kuwa makafiri wameingia

Ndani ya patakatifu pake;

Ambao kwa habari zao wewe uliamuru

Wasiingie katika kusanyiko lako.

11Watu wake wote hupiga kite,[#Yer 38:9]

Wanatafuta chakula;

Wameyatoa matamaniko yao wapate chakula

Cha kuihuisha nafsi;

Ee BWANA, tazama, uangalie;

Kwa maana mimi nimekuwa mnyonge.

12Je! Si kitu kwenu, enyi nyote mpitao njia,[#Dan 9:12; Mt 24:21; Lk 21:22]

Angalieni, mtazame

Kama kuna majonzi yo yote mfano wa majonzi yangu,

Niliyotendwa mimi,

Ambayo BWANA amenihuzunisha kwa hayo

Siku ya hasira yake iwakayo.

13Toka juu amepeleka moto mifupani mwangu,[#Ayu 18:8; Zab 66:11; Eze 12:13; Hos 7:12]

Nao umeishinda;

Ametandika wavu aninase miguu,

Amenirudisha nyuma;

Amenifanya kuwa mtu wa pekee,

Na mgonjwa mchana kutwa.

14Kongwa la makosa yangu limefungwa na mkono wake;[#Kum 28:48; Mit 5:22; Isa 14:25; Mt 11:29,30]

Hayo yameshikamana;

Yamepanda juu shingoni mwangu;

Amezikomesha nguvu zangu;

15Bwana amenitia mikononi mwao,[#Isa 63:3; Ufu 14:19]

Ambao siwezi kupingamana nao.

Bwana amewafanya mashujaa wangu wote

Kuwa si kitu kati yangu;

Ameita mkutano mkuu kinyume changu

Ili kuwaponda vijana wangu;

Bwana amemkanyaga kama shinikizoni

Huyo bikira binti Yuda.

16Mimi ninayalilia mambo hayo;

Jicho langu, jicho langu linachuruzika maji;

Kwa kuwa mfariji yu mbali nami,

Ambaye ilimpasa kunihuisha nafsi;

Watoto wangu wameachwa peke yao,

Kwa sababu huyo adui ameshinda.

17Sayuni huinyosha mikono yake;

Hakuna hata mmoja wa kumfariji;

BWANA ametoa amri juu ya Yakobo,

Kwamba wamzungukao wawe watesi wake;

Yerusalemu amekuwa kati yao

Kama kitu kichafu.

18BWANA ndiye mwenye haki;[#Neh 9:33; Dan 9:7; 1 Sam 12:14]

Maana nimeiasi amri yake;

Sikieni, nawasihi, enyi watu wote,

Mkayatazame majonzi yangu;

Wasichana wangu na wavulana wangu

Wamechukuliwa mateka.

19Naliwaita hao walionipenda

Lakini walinidanganya;

Makuhani wangu na wazee wangu

Walifariki mjini;

Hapo walipokuwa wakitafuta chakula

ili kuzihuisha nafsi zao.

20Angalia, Ee BWANA; maana mimi ni katika dhiki;[#Isa 16:11; Yer 4:19; Hos 11:8; Kum 32:25]

Mtima wangu umetaabika;

Moyo wangu umegeuka ndani yangu;

Maana nimeasi vibaya sana;

Huko nje upanga hufisha watu;

Nyumbani mna kama mauti.

21Wamesikia kwamba napiga kite;[#Yer 46:1]

Hakuna hata mmoja wa kunifariji;

Adui zangu wote wamesikia habari ya mashaka yaliyonipata;

Hufurahi kwa kuwa umeyafanya hayo;

Utaileta siku ile uliyoitangaza,

Nao watakuwa kama mimi.

22Huo uovu wao wote

Na uje mbele zako wewe;

Ukawatende wao kama ulivyonitenda mimi

Kwa dhambi zangu zote;

Kwa maana mauguzi yangu ni mengi sana,

Na moyo wangu umezimia.

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania