Mit 11

Mit 11

1Mizani ya hadaa ni chukizo kwa BWANA;

Bali vipimo vilivyo sawasawa humpendeza.

2Kijapo kiburi ndipo ijapo aibu;[#Dan 4:30]

Bali hekima hukaa na wanyenyekevu.

3Ukamilifu wao wenye haki utawaongoza

Bali ukaidi wao wenye fitina utawaangamiza.

4Mali hazifaidii kitu siku ya ghadhabu;[#Eze 7:19; Sef 1:18; Mwa 7:1]

Bali haki huokoa na mauti.

5Haki yake mtu mkamilifu itamwongoza njia yake;

Bali mtu mwovu ataanguka kwa uovu wake.

6Haki yao wenye haki itawaokoa;[#1 Tim 4:8; Mhu 10:8]

Bali wafanyao fitina watanaswa kwa hila yao wenyewe.

7Mtu mwovu atakapokufa, taraja lake lapotea;

Na matumaini ya uovu huangamia.

8Mwenye haki huokolewa katika dhiki,

Na mtu mwovu ataiingia badala yake.

9Asiyemcha Mungu humpoteza jirani yake kwa kinywa chake;[#Ayu 8:13]

Bali wenye haki watapona kwa maarifa.

10Wenye haki wasitawipo, mji hufurahi;[#Est 8:15]

Waovu waangamiapo, watu hupiga kelele.

11Mji hutukuzwa kwa mbaraka wa mwenye haki;

Bali mji hupinduliwa kwa kinywa cha mwovu.

12Asiye na akili humdharau mwenziwe;

Bali mtu aliye na ufahamu hunyamaza.

13Mwenye kitango akisingizia hufunua siri;

Bali mwenye roho ya uaminifu husitiri mambo.

14Pasipo mashauri taifa huanguka;[#1 Fal 12:1]

Bali kwa wingi wa washauri huja wokovu.

15Amdhaminiye mgeni hakosi ataumia;

Achukiaye mambo ya dhamana yu salama.

16Mwanamke wa adabu huheshimiwa daima;

Na watu wakali hushika mali siku zote.

17Mwenye rehema huitendea mema nafsi yake;[#Mt 25:34]

Aliye mkali hujisumbua mwili wake.

18Mtu mwovu hupata mshahara wa udanganyifu;[#Hos 10:12; Gal 6:8,9]

Apandaye haki ana thawabu ya hakika.

19Haki huelekea uzima;

Afuataye maovu hufuata mauti yake mwenyewe.

20Wenye kuhalifu moyoni ni chukizo kwa BWANA;

Walio wakamilifu katika njia zao humpendeza.

21Hakika, mtu mwovu hatakosa adhabu;

Bali wazao wa wenye haki wataokoka.

22Kama pete ya dhahabu katika pua ya nguruwe,

Kadhalika mwanamke mzuri asiye na akili.

23Haja ya mwenye haki ni mema tu;[#Rum 2:8]

Bali kutaraji kwake mtu mwovu ni ghadhabu.

24Kuna atawanyaye, lakini huongezewa zaidi;

Kuna azuiaye isivyo haki, lakini huelekea uhitaji.

25Nafsi ya mtu mkarimu itawandishwa;[#Mt 5:7]

Anyweshaye atanyweshwa mwenyewe.

26Awanyimaye watu nafaka, watu watamlaani;[#Amo 8:5; Ayu 29:13]

Auzaye nafaka, baraka itakuwa kichwani pake.

27Atafutaye mema kwa bidii hutafuta fadhili;[#Est 7:10]

Atafutaye madhara, hayo yatamjia.

28Azitegemeaye mali zake ataanguka;[#Mk 10:24; Lk 12:21; 1 Tim 6:17; Yer 17:8]

Mwenye haki atasitawi kama jani.

29Ataabishaye nyumba yake mwenyewe ataurithi upepo;[#Mhu 5:16]

Mpumbavu atakuwa mtumwa wa mtu mwenye moyo wa akili.

30Mazao ya mwenye haki ni mti wa uzima;

Na mwenye hekima huvuta roho za watu.

31Tazama, mwenye haki atalipwa duniani;[#1 Pet 4:18; Yer 25:29]

Basi mwovu na mkosaji si mara nyingi zaidi?

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania