Mit 15

Mit 15

1Jawabu la upole hugeuza hasira;

Bali neno liumizalo huchochea ghadhabu.

2Ulimi wa mwenye hekima hutamka maarifa vizuri;

Bali vinywa vya wapumbavu humwaga upumbavu.

3Macho ya BWANA yako kila mahali;[#2 Nya 16:9; Ayu 34:21; Mit 5:21; Yer 16:17; Zek 4:10; Ebr 4:13]

Yakimchunguza mbaya na mwema.

4Ulimi safi ni mti wa uzima;

Bali ukorofi wa ulimi huvunja moyo.

5Mpumbavu hudharau kurudiwa na babaye;

Bali yeye aangaliaye maonyo hupata busara.

6Katika nyumba ya mwenye haki mna akiba nyingi;

Bali mapato ya mtu mbaya huwa taabu tu.

7Midomo ya mwenye haki hueneza maarifa;

Bali moyo wa mpumbavu haufanyi hivyo.

8Sadaka ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA;[#Isa 61:8; Yer 6:20; Amo 5:22; Lk 18:11]

Bali maombi ya mtu mnyofu ni furaha yake.

9Njia ya mtu mbaya ni chukizo kwa BWANA;[#Mit 21:21; Isa 51:1,7; 1 Tim 6:11]

Bali humpenda mtu afuatiaye wema.

10Adhabu kali ina yeye aiachaye njia;

Naye achukiaye kukemewa atakufa.

11Kuzimu na Uharibifu vi wazi mbele za BWANA;[#Yn 2:24; Mdo 1:24]

Si zaidi basi, mioyo ya wanadamu?

12Mwenye mzaha hapendi kukaripiwa;

Wala yeye hawaendei wenye hekima.

13Moyo wa furaha huchangamsha uso;

Bali kwa huzuni ya moyo roho hupondeka.

14Moyo wa mwenye ufahamu hutafuta maarifa;

Bali kinywa cha wapumbavu hula upumbavu.

15Siku zote za mtu ateswaye ni mbaya;

Bali ukunjufu wa moyo ni karamu ya daima.

16Kuwa na mali chache pamoja na kumcha BWANA;[#Mit 16:8; Mhu 4:6; 1 Tim 6:6]

Ni bora kuliko mali nyingi pamoja na taabu.

17Chakula cha mboga penye mapendano;

Ni bora kuliko ng’ombe aliyenona pamoja na kuchukiana.

18Mtu wa hasira huchochea ugomvi;

Bali asiye mwepesi wa hasira hutuliza mashindano.

19Njia ya mtu mvivu ni kama boma la miiba;

Bali mapito yao wenye unyofu hufanyika njia kuu.

20Mwana mwenye hekima humfurahisha babaye;

Bali mpumbavu humdharau mamaye.

21Upumbavu ni furaha kwake aliyepungukiwa na akili;[#Efe 5:15]

Bali mwenye ufahamu huunyosha mwenendo wake.

22Pasipo mashauri makusudi hubatilika;

Bali kwa wingi wa washauri huthibithika.

23Mtu hulifurahia jibu la kinywa chake;

Na neno linenwalo wakati wa kufaa ni jema kama nini!

24Kwa mtu mwenye akili njia ya uhai huenda juu;[#Flp 3:20]

Ili atoke katika kuzimu chini.

25BWANA ataing’oa nyumba ya mwenye kiburi;

Bali atauthibitisha mpaka wa mjane.

26Mashauri mabaya ni chukizo kwa BWANA;

Bali maneno yapendezayo ni safi.

27Atamaniye faida huifadhaisha nyumba yake mwenyewe;[#Yos 6:18; 1 Sam 8:3; Mit 1:19; Isa 5:8; Zek 5:3]

Bali achukiaye zawadi ataishi.

28Moyo wa mwenye haki hufikiri jinsi atakavyojibu;[#1 Pet 3:15]

Bali kinywa cha wasio haki humwaga mabaya.

29BWANA yu mbali na wasio haki;[#Efe 2:12; Zab 34:15,16; Yn 9:31; Rum 8:26]

Bali huisikia sala ya mwenye haki.

30Mng’ao wa macho huufurahisha moyo;

Habari njema huinenepesha mifupa.

31Sikio lisikilizalo lawama yenye uhai

Litakaa kati yao wenye hekima.

32Akataaye maonyo huidharau nafsi yake mwenyewe;

Bali yeye asikilizaye lawama hujipatia ufahamu.

33Kumcha BWANA ni maonyo ya hekima;

Na kabla ya heshima hutangulia unyenyekevu.

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania