Mit 2

Mit 2

Thamani ya Hekima

1Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu,

Na kuyaweka akiba maagizo yangu;

2Hata ukatega sikio lako kusikia hekima,

Ukauelekeza moyo wako upate kufahamu;

3Naam, ukiita busara,

Na kupaza sauti yako upate ufahamu;

4Ukiutafuta kama fedha,[#Zab 19:10; Mit 3:14,15; Mt 6:19-21]

Na kuutafutia kama hazina iliyositirika;

5Ndipo utakapofahamu kumcha BWANA,

Na kupata kumjua Mungu.

6Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima;[#Lk 21:15; Yn 6:45; Yak 1:5]

Kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu;

7Huwawekea wanyofu akiba ya hekima kamili;[#Zab 84:11]

Yeye ni ngao kwao waendao kwa ukamilifu;

8Apate kuyalinda mapito ya hukumu,[#1 Sam 2:9; 1 Pet 1:5; Zab 37:23,24,28,31]

Na kuhifadhi njia ya watakatifu wake.

9Ndipo utakapofahamu haki na hukumu,

Na adili, na kila njia njema.

10Maana hekima itaingia moyoni mwako,

Na maarifa yatakupendeza nafsi yako;

11Busara itakulinda;[#Mit 6:22]

Ufahamu utakuhifadhi.

12Ili kukuokoa na njia ya uovu,

Na watu wanenao yaliyopotoka;

13Watu waziachao njia za unyofu,[#Yn 3:19; Efe 4:18]

Ili kuziendea njia za giza;

14Wafurahio kutenda mabaya;

Wapendezwao na upotoe wa waovu;

15Waliopotoka katika njia zao;

Walio wakaidi katika mapito yao.

16Ili kuokoka na malaya,

Naam, malaya mwenye kubembeleza kwa maneno yake;

17Amwachaye rafiki wa ujana wake,[#Mal 2:14; Mwa 2:24]

Na kulisahau agano la Mungu wake.

18Maana nyumba yake inaelekea mauti,

Na mapito yake yanakwenda kwenye wafu.

19Katika hao wamwendeao harudi hata mmoja,[#Mhu 7:26; Ebr 13:4]

Wala hawazifikilii njia za uzima.

20Ili upate kwenda katika njia ya watu wema,[#Ebr 6:12]

Na kuyashika mapito ya wenye haki.

21Maana wanyofu watakaa katika nchi,

Na wakamilifu watadumu ndani yake.

22Bali waovu watatengwa na nchi,

Nao wafanyao hila watang’olewa.

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania