Mit 29

Mit 29

1Aonywaye mara nyingi akishupaza shingo,

Atavunjika ghafula, wala hapati dawa.

2Wenye haki wakiwa na amri, watu hufurahi;

Bali mwovu atawalapo, watu huugua.

3Apendaye hekima humfurahisha babaye;[#1 Fal 1:48; Flp 2:22; Mit 10:1; 15:20]

Bali ashikamanaye na makahaba hutapanya mali.

4Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu;

Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.

5Mwenye kujipendekeza kwa jirani yake,

Hutandika wavu ili kuitega miguu yake.

6Kuna mtego katika kosa la mtu mbaya;

Bali mwenye haki huimba na kufurahi.

7Mwenye haki huyaangalia madai ya maskini;[#Ayu 29:16; Zab 31:7; Isa 35:3,4; Lk 22:32; Gal 6:1]

Bali mtu mbaya hana ufahamu hata ayajue.

8Watu wenye dharau huwasha mji moto;

Bali wenye hekima hugeuzia mbali ghadhabu.

9Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu;

Akikasirika au akicheka, pia hapana raha.

10Wamwagao damu humchukia mtu mkamilifu;

Bali wenye haki humtunza nafsi yake.

11Mpumbavu hudhihirisha hasira yake yote;

Bali mwenye hekima huizuia na kuituliza.

12Mwenye kutawala akisikiliza uongo;

Basi watumishi wake wote watakuwa waovu.

13Maskini na mdhalimu hukutana pamoja;[#Mt 5:45]

BWANA huwatia nuru macho yao wote wawili.

14Mfalme awahukumuye maskini kwa uaminifu;[#Zab 72:2]

Kiti chake cha enzi kitathibitika milele.

15Fimbo na maonyo hutia hekima;

Bali mwana aliyeachiliwa humwaibisha mamaye.

16Waovu wakiongezeka, maasi huongezeka;[#Zab 37:36]

Bali wenye haki watayatazama maanguko yao.

17Mrudi mwanao naye atakustarehesha;[#Mit 13:24]

Naam, atakufurahisha nafsi yako.

18Pasipo maono, watu huacha kujizuia;[#1 Sam 3:1; Amo 8:11; Yn 13:17; Yak 1:25]

Bali ana heri mtu yule aishikaye sheria.

19Haitoshi mtumwa kuonywa kwa maneno;

Maana ajapoyafahamu hataitika.

20Je! Umemwona mtu mwenye kuhamaki katika maneno?

Afadhali kumtumaini mpumbavu kuliko yeye.

21Amtunduiaye mtumwa wake tangu utoto,

Mwisho wake atakuwa ni mwanawe.

22Mtu wa hasira huchochea ugomvi;

Na mtu mwenye ghadhabu huasi sana.

23Kiburi cha mtu kitamshusha;[#Isa 2:11,12; Mt 23:12; Lk 14:11]

Bali mwenye roho ya unyenyekevu ataheshimiwa.

24Mshiriki wa mwivi huichukia nafsi yake mwenyewe;[#Law 5:1]

Asikia maapizo, wala hana neno.

25Kuwaogopa wanadamu huleta mtego;[#Mwa 12:12]

Bali amtumainiye BWANA atakuwa salama.

26Watu wengi hutafuta upendeleo wa mkuu;

Bali hukumu ya kila mtu hutoka kwa BWANA

27Mtu aliye dhalimu ni chukizo kwa wenye haki;

Na mnyofu wa mwenendo ni chukizo kwa waovu.

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania