Ufu 16

Ufu 16

Ghadhabu ya Mungu

1Nikasikia sauti kuu kutoka hekaluni, ikiwaambia wale malaika saba, Enendeni, mkavimimine vile vitasa saba vya ghadhabu ya Mungu juu ya nchi.[#Isa 66:6; Zab 69:24; Yer 10:25; Sef 3:8]

2Akaenda huyo wa kwanza, akakimimina kitasa chake juu ya nchi; pakawa na jipu baya, bovu, juu ya wale watu wenye chapa ya huyo mnyama, na wale wenye kuisujudia sanamu yake.[#Kut 9:10,11; Kum 28:35]

3Na huyo wa pili akakimimina kitasa chake juu ya bahari, ikawa damu kama damu ya mfu, na vitu vyote vyenye roho ya uhai katika bahari vikafa.[#Kut 7:17-21]

4Na huyo wa tatu akakimimina kitasa chake juu ya mito na chemchemi za maji; zikawa damu.[#Kut 7:17-21; Zab 78:44]

5Nami nikamsikia malaika wa maji akisema, Wewe u mwenye haki, uliyeko na uliyekuwako, Mtakatifu, kwa kuwa umehukumu hivi;[#Zab 119:137; 145:17; Kut 3:14; Kum 32:4; Isa 41:4]

6kwa kuwa walimwaga damu ya watakatifu na ya manabii, nawe umewapa damu wainywe; nao wamestahili.[#Isa 49:26; Zab 79:3]

7Nikaisikia hiyo madhabahu ikisema, Naam, Bwana Mungu Mwenyezi, ni za kweli, na za haki, hukumu zako.[#Zab 19:9; 119:137; Ufu 9:13; 19:2]

8Na huyo wa nne akakimimina kitasa chake juu ya jua, nalo likapewa kuwaunguza wanadamu kwa moto.

9Wanadamu wakaunguzwa maunguzo makubwa, nao wakalitukana jina la Mungu aliye na mamlaka juu ya mapigo hayo; wala hawakutubu wala kumpa utukufu.[#Ufu 16:21; 9:20,21]

10Na huyo wa tano akakimimina kitasa chake juu ya kiti cha enzi cha yule mnyama; ufalme wake ukatiwa giza; wakatafuna ndimi zao kwa sababu ya maumivu,[#Kut 10:21; Isa 8:21,22]

11wakamtukana Mungu wa mbingu kwa sababu ya maumivu yao, na kwa sababu ya majipu yao; wala hawakuyatubia matendo yao.[#Dan 2:19]

12Na huyo wa sita akakimimina kitasa chake juu ya mto ule mkubwa Frati; maji yake yakakauka, ili njia itengenezwe kwa wafalme watokao katika maawio ya jua.[#Isa 11:15; 41:2; 44:27; Mwa 15:18; Kum 1:7; Yos 1:4; Yer 50:38]

13Nikaona roho tatu za uchafu zilizofanana na vyura, zikitoka katika kinywa cha yule joka, na katika kinywa cha yule mnyama, na katika kinywa cha yule nabii wa uongo.[#Ufu 12:9; 13:1,11; Kut 8:3; 1 Fal 22:21-23]

14Hizo ndizo roho za mashetani, zifanyazo ishara, zitokazo na kuwaendea wafalme wa ulimwengu wote kuwakusanya kwa vita ya siku ile kuu ya Mungu Mwenyezi.[#Ufu 13:13; 19:19]

15(Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na kuyatunza mavazi yake, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake.)[#Mt 24:43-44; Lk 12:39-40; Ufu 3:3,18; 1 The 5:2]

16Wakawakusanya hata mahali paitwapo kwa Kiebrania, Har-Magedoni.[#2 Fal 9:27; 23:29; Zek 12:11; Amu 5:19,31]

17Na huyo wa saba akakimimina kitasa chake juu ya anga. Sauti kuu ikatoka katika hekalu, katika kile kiti cha enzi, ikisema, Imekwisha kuwa.[#Isa 66:6]

18Pakawa na umeme na sauti na radi; na palikuwa na tetemeko la nchi kubwa, ambalo tangu wanadamu kuwako juu ya nchi hapakuwa namna ile, jinsi lilivyokuwa kubwa tetemeko hilo.[#Ufu 4:5; 8:5; 11:13,19; Kut 19:16; Dan 12:1]

19Na mji ule mkuu ukagawanyikana mafungu matatu, na miji ya mataifa ikaanguka; na Babeli ule mkuu ukakumbukwa mbele za Mungu, kupewa kikombe cha mvinyo ya ghadhabu ya hasira yake.[#Isa 51:17; Dan 4:30; Yer 25:15; Ufu 14:10]

20Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena.[#Ufu 6:14; 20:11]

21Na mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta, ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno.[#Kut 9:23; Ufu 11:19]

Swahili Union Version (SUV): © Bible Society of Tanzania and Bible Society of Kenya, 1952, 1997. All rights reserved. lt/pgt ltpgtSwahili Union Version (SUV): Hakimiliki -1952, 1997: kwa: Chama cha Biblia cha Tanzania na Chama cha Biblia cha Kenya. Haki zote zimehifadhiwa.
Published by: Bible Society of Tanzania