The chat will start when you send the first message.
1Na kwa malaika wa kanisa lililoko Sardi andika;[#Ufu 5:6; 1:16]
Haya ndiyo anenayo yeye aliye na hizo Roho saba za Mungu, na zile nyota saba. Nayajua matendo yako, ya kuwa una jina la kuwa hai, nawe umekufa.
2Uwe mwenye kukesha, ukayaimarishe mambo yaliyosalia, yanayotaka kufa. Maana sikuona matendo yako kuwa yametimilika mbele za Mungu wangu.[#Eze 34:4]
3Basi kumbuka jinsi ulivyopokea, na jinsi ulivyosikia; yashike hayo na kutubu. Walakini usipokesha, nitakuja kama mwivi, wala hutaijua saa nitakayokuja kwako.[#Mt 24:43-44; Lk 12:39-40; Ufu 16:15; 1 The 5:2]
4Lakini unayo majina machache katika Sardi, watu wasioyatia mavazi yao uchafu. Nao watakwenda pamoja nami hali wamevaa mavazi meupe, kwa kuwa wamestahili.[#Yud 1:23]
5Yeye ashindaye atavikwa hivyo mavazi meupe, wala sitalifuta kamwe jina lake katika kitabu cha uzima, nami nitalikiri jina lake mbele za Baba yangu, na mbele ya malaika zake.[#Kut 32:32-33; Zab 69:28; Ufu 4:4; 6:11; 7:9; 20:12; Flp 4:3; Mt 10:32; Lk 12:8]
6Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.
7Na kwa malaika wa kanisa lililoko Filadelfia andika;[#Isa 22:22; Ayu 12:14]
Haya ndiyo anenayo yeye aliye mtakatifu, aliye wa kweli, aliye na ufunguo wa Daudi, yeye mwenye kufungua wala hapana afungaye, naye afunga wala hapana afunguaye.
8Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga, kwa kuwa unazo nguvu kidogo, nawe umelitunza neno langu, wala hukulikana jina langu.[#1 Kor 16:9]
9Tazama, nakupa walio wa sinagogi la Shetani, wasemao kwamba ni Wayahudi, nao sio, bali wasema uongo. Tazama, nitawafanya waje kusujudu mbele ya miguu yako, na kujua ya kuwa nimekupenda.[#Isa 49:23; 60:14; 43:4; 45:14; 66:23]
10Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi.[#Ufu 13:10; Ebr 10:36; Lk 21:19; 2 Tim 2:12]
11Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako.[#Ufu 1:3; 2:5,10]
12Yeye ashindaye, nitamfanya kuwa nguzo katika hekalu la Mungu wangu, wala hatatoka humo tena kabisa, nami nitaandika juu yake jina la Mungu wangu, na jina la mji wa Mungu wangu, huo Yerusalemu mpya, ushukao kutoka mbinguni kwa Mungu wangu, na jina langu mwenyewe, lile jipya.[#Ufu 21:2; 14:1; 22:4; Eze 48:35; Gal 2:9; Isa 62:2; 65:15]
13Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.
14Na kwa malaika wa kanisa lililoko Laodikia andika;[#Mit 8:22; Zab 89:37; Yn 1:3; Kol 1:15]
Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.
15Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto.[#Ufu 2:2; Rum 12:11]
16Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu.
17Kwa kuwa wasema, Mimi ni tajiri, nimejitajirisha, wala sina haja ya kitu; nawe hujui ya kuwa wewe u mnyonge, na mwenye mashaka, na maskini, na kipofu, na uchi.[#Hes 12:8; 1 Kor 3:18; 4:8]
18Nakupa shauri, ununue kwangu dhahabu iliyosafishwa kwa moto, upate kuwa tajiri, na mavazi meupe upate kuvaa, aibu ya uchi wako isionekane, na dawa ya macho ya kujipaka macho yako, upate kuona.[#1 Pet 1:7; Isa 55:1; Ufu 16:15]
19Wote niwapendao mimi nawakemea, na kuwarudi; basi uwe na bidii, ukatubu.[#Mit 3:12; Ebr 12:6; 1 Kor 11:32]
20Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami.[#Mk 13:14; Yn 14:23; Lk 12:36; 22:29]
21Yeye ashindaye, nitampa kuketi pamoja nami katika kiti changu cha enzi, kama mimi nilivyoshinda nikaketi pamoja na Baba yangu katika kiti chake cha enzi.[#Mt 19:28]
22Yeye aliye na sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa.