The chat will start when you send the first message.
1Ndugu zangu, sitaki mshindwe kutambua umuhimu wa kile kilichowatokea baba zetu waliokuwa na Musa. Walifunikwa na wingu, na walipita katika bahari.[#10:1 Wingu lililowaongoza na kuwalinda watu wa Israeli katika safari yao kutoka Misri, wakavuka Bahari ya Shamu, na wakiwa jangwani. Tazama Kut 13:20-22; 14:19-20.]
2Walibatizwa wote katika Musa katika wingu na katika bahari.[#10:2 Tazama katika Orodha ya Maneno. Hapa, Paulo anamaanisha kuwa kilichofanyika kwa Wayahudi walipokuwa na Musa kinaweza kulinganishwa na ubatizo wa waamini katika Kristo.]
3Wote walikula chakula kilichotolewa na Roho wa Mungu,
4na wote walikunywa kinywaji kinachotolewa na Roho wa Mungu. Kinywaji walichokunywa kilitoka katika mwamba wa roho uliokuwa pamoja nao, na mwamba huo ni Kristo.
5Lakini Mungu hakupendezwa na wengi wao, na hivyo waliangamizwa jangwani.
6Mambo haya yaliyotokea ni tahadhali kwa ajili yetu. Mifano hii itufanye tuache kutamani maovu kama baadhi yao walivyofanya.
7Msiabudu sanamu kama ambavyo baadhi yao walifanya. Na kama Maandiko yanavyosema, “Waliketi chini kula na kunywa kisha wakasimama kucheza.”[#Kut 32:6]
8Tusifanye dhambi ya uzinzi kama baadhi yao walivyofanya na watu ishirini na tatu elfu miongoni mwao wakafa.
9Tusimjaribu Kristo kama vile baadhi yao walivyofanya. Kwa sababu hiyo, waliuawa na nyoka.[#10:9 Nakala zingine za Kiyunani zimeongeza, “Bwana”.]
10Na msinung'unike kama baadhi yao walivyofanya na wakauawa na malaika anayeangamiza.
11Mambo yaliyowapata wale watu ni mifano na yaliandikwa ili kututahadharisha sisi tunaoishi nyakati hizi za mwisho.
12Hivyo kila anayedhani kuwa yuko imara katika imani yake, basi awe mwangalifu asianguke.
13Majaribu mliyonayo ni yale yale waliyonayo watu wote. Lakini Mungu ni mwaminifu maana hataacha mjaribiwe kwa kiwango msichoweza kustahimili. Mnapojaribiwa, Mungu atawapa mlango wa kutoka katika jaribu hilo. Ndipo mtaweza kustahimili.
14Hivyo rafiki zangu wapenzi, zikimbieni ibada za sanamu.
15Ninyi ni watu wenye akili. Upimeni ukweli wa haya ninayosema sasa.
16Kikombe cha baraka tunachokitolea shukrani ni ushirika wa sadaka ya damu ya Kristo, sawa? Na mkate ule tunaomega, ni ushirika wa mwili wa Kristo, sawa?[#10:16 Kikombe cha divai ambacho waamini katika Kristo humshukuru Mungu katika Mlo wa Bwana (Meza ya Bwana au sakramenti).]
17Kuna mkate mmoja, nasi tulio wengi tu mwili mmoja, kwa kuwa tunashiriki katika mkate huo mmoja.
18Na fikirini kuhusu Waisraeli wanavyofanya. Wanapokula sadaka, wanaunganishwa pamoja kwa kugawana kile kilichotolewa kwenye madhabahu.
19Je! ninataka kuthibitisha kitu gani? Je! ninasema kwamba nyama iliyotolewa sadaka kwa sanamu ni hakika najisi kwa kiasi fulani? Je! ninasema kwamba sanamu ni mungu wa kweli? Hapana.
20Lakini ninasema kuwa chakula kinapotolewa sadaka kwa sanamu, ni sadaka kwa mashetani, siyo kwa Mungu. Nami sitaki ninyi muungane na hao wengine katika kuyaabudu mashetani.
21Hamwezi kukinywea kikombe cha Bwana na kisha mkakinywea kiombe kinachotukuza mashetani. Hamwezi kushiriki kula chakula na kunywa pamoja kwenye meza ya Bwana kisha mkaenda kushiriki kula chakula na kunywa pamoja kwenye meza inayotukuza mashetani.
22Kufanya hivyo kunamtia wivu Bwana. Je! mnafikiri tunaweza kujaribu kumfanya Bwana apate wivu? Mnadhani tuna nguvu kuliko yeye?[#10:22 Tazama Kum 32:16-17.]
23Mnasema “Vitu vyote vimeruhusiwa.” Lakini si vitu vyote vinafaa. “Vitu vyote vimeruhusiwa.” Lakini vitu vingine havisaidii katika kuliimarisha kanisa.
24Jitahidi kuwafanyia mema wengine badala ya kufanya mema kwa ajili yako wewe wenyewe.
25Kuleni chakula chochote kinachouzwa sokoni. Msiulize maswali ili kutafuta kujua kama ni sahihi ama la kwako kukila.
26Mnaweza kula chakula hicho, “Kwa sababu dunia na kila kitu kilichomo ndani yake ni vya Bwana.”[#Zab 24:1; 50:12; 89:11]
27Asiye mwamini anaweza kuwaalika kula chakula. Ikiwa mtakwenda, basi mle chochote kitakachowekwa mbele yenu. Msiulize ulize maswali.
28Lakini mtu akiwaambia, “Chakula hicho kilitolewa sadaka katika hekalu la miungu,” basi msile. Kwa sababu kinaweza kumwathiri mtu na uhusiano wake na Mungu.
29Na hapa sizungumzii kuhusu uhusiano wenu na Mungu, bali uhusiano wa mtu yule aliyewaambia na Mungu. Kwa nini uhuru wangu mwenyewe uhukumiwe na mawazo ya mtu mwingine?
30Ikiwa mimi nitakula chakula nikiwa na shukrani, kwa nini basi nisikosolewa kwa sababu ya kitu ambacho kwa hicho ninamshukuru Mungu?
31Ninachosema ni kwamba: ukila, au ukinywa, au ukifanya jambo lolote, lifanye kwa ajili ya utukufu wa Mungu.
32Kamwe usifanye jambo lolote litakalowafanya watu wengine kutenda mabaya, iwe ni Wayahudi, wasio Wayahudi au mtu yeyote katika kanisa la Mungu.
33Ninafanya vivyo hivyo. Ninajitahidi kwa njia yeyote ile kumpendeza kila mtu. Mimi sijaribu kutenda yaliyo mema kwangu. Ninajaribu kutenda yale yaliyo na manufaa kwa watu wengine ili waweze kuokoka.