The chat will start when you send the first message.
1Hayo yalipokwisha, akafa Nahasi, mfalme wa wana wa Amoni, naye mwanawe akawa mfalme mahali pake.
2Dawidi akasema: Nitamfanyizia Hanuni, mwana wa Nahasi, mambo ya upole, kwani baba yake alinifanyizia nami mambo ya upole. Kwa hiyo Dawidi akatuma wajumbe, wamtulize moyo kwa ajili ya baba yake. Lakini watumishi wa Dawidi walipofika katika nchi ya wana wa Amoni kwake Hanuni, wamtulize moyo,
3wakuu wa wana wa Amoni wakamwambia Hanuni: Je? Dawidi anataka kweli kumheshimu baba yako machoni pako akituma kwako wajumbe wa kukutuliza moyo? Watumishi wake hawakuja kwako kuichunguza nchi na kuifudikiza na kuipeleleza?
4Ndipo, Hanuni alipowakamata watumishi wa Dawidi, akawanyoa nywele, akawakatia mavazi yao nusu kuyafikisha matako yao, kisha wakawapa ruhusa kwenda zao,
5wakaenda zao. Watu walipompasha Dawidi habari za hao watu, akatuma wengine kuwaendea njiani, kwa kuwa watu hao walikuwa wametwezwa sana; mfalme akawaambia: Kaeni Yeriko, mpaka ndevu zenu zikue tena, kisha rudini!
6Wana wa Amoni walipoona, ya kuwa wamejichukizisha kwake Dawidi, ndipo, Hanuni na wana wa Amoni walipotuma vipande elfu vya fedha, ndio shilingi milioni moja na 200000, wakodishe magari na wapanda farasi kwa Washami wa Mesopotamia na kwa Washami wa Maka nako Soba.
7Wakakodisha magari 32000 pamoja na mfalme wa Maka na watu wake, wakaja, wakapiga makambi mbele ya Medeba, nao wana wa Amoni wakakusanyika wakitoka mijini kwao, wakaja vitani.
8Dawidi alipoyasikia, akamtuma Yoabu na vikosi vyote vya mafundi wa vita.
9Wana wa Amoni wakatoka, wakajipanga penye lango la mji, wapige vita, nao wafalme waliokuja wakawa peke yao shambani.
10Yoabu alipoona, ya kuwa wamejipanga kupiga vita usoni na mgongoni kwake, akachagua wengine katika wateule wote wa Waisiraeli, akawapanga, wapigane na Washami.
11Nao watu waliosalia akawatia mkononi mwa ndugu yake Abisai, wakawapanga, wapigane na wana wa Amoni.
12akasema: Kama Washami wanapata nguvu za kunishinda, sharti uje kunisaidia. Tena kama wana wa Amoni wanapata nguvu za kukushinda, sharti nije, nikusaidie.
13Jipe moyo, tushikizane mioyo, tuwapiganie watu wa kwetu na miji ya Mungu wetu! Ndipo, Bwana atakapoyafanya, aliyoyaona kuwa mema.
14Kisha Yoabu na watu wake, aliokuwa nao, wakawasogelea Washami kupigana nao, lakini wao wakawakimbia.[#1 Sam. 3:18.]
15Wana wa Amoni walipoona, ya kuwa Washami wamekimbia, ndipo, nao walipomkimbia ndugu yake Abisai, wakaingia mjini mwao, lakini Yoabu akaja Yerusalemu.
16Washami walipoona, ya kuwa wameshindwa nao Waisiraeli, wakatuma wajumbe, wakawaita Washami walioko ng'ambo ya huko ya jito hilo, waje vitani, naye Sofaki, mkuu wa vikosi vya Hadarezeri, akawaongoza.
17Dawidi alipopashwa habari hizo, akawakusanya Waisiraeli wote, akauvuka Yordani, akawajia, akajipanga mbele yao. Dawidi alipokwisha kujipanga kupiga vita na Washami, wakapigana naye.
18Kisha Washami wakawakimbia Waisiraeli, Dawidi akaua kwao Washamu watu 7000 waliopanda magari na watu 40000 waliokwenda kwa miguu, hata Sofaki, mkuu wa vikosi, akamwua.
19Watumishi wa Hadarezeri walipoona, ya kuwa wameshindwa na Waisiraeli, wakafanya mapatano na Dawidi, wakamtumikia; kisha Washami hawakutaka kuwasaidia wana wa Amoni tena.