1 Wafalme 6

Kulijenga Jumba la Mungu.

(Taz. 2 Mambo 3:1-13.)

1Ikawa katika mwaka wa 480, tangu wana wa Isiraeli walipotoka Misri, katika mwaka wa nne, Salomo alipokuwa mfalme wa Waisiraeli, katika mwezi wa Ziwu, ndio mwezi wa pili, ndipo, alipomjengea Bwana nyumba.

2Nayo hiyo nyumba, mfalme Salomo aliyomjengea Bwana, urefu wake wa kwenda mbele ulikuwa mikono 60, nao upana wake mikono 20, nao urefu wake wa kwenda juu mikono 30.

3Nao ukumbi uliokuwa usoni pake jumba hilo takatifu urefu wake wa kwenda mbele ulikuwa mikono 20, upatane na upana wa nyumba yenyewe, upana wake ulikuwa mikono kumi kuufuata urefu wa nyumba wa kwenda mbele.[#1 Fal. 7:15-21; Yoh. 10:23.]

4Akaitia hiyo nyumba madirisha yenye miti iliyoungwa.

5Tena kando ya ukuta wa nyumba kuizunguka yote akajenga vyumba vilivyozizunguka kuta za nyumba pande zote za hapo Patakatifu napo hapo penye chumba cha nyuma; hivyo vyumba akavitengeneza ubavuni pande zote.

6Navyo hivyo vyumba vya chini upana wao ulikuwa mikono mitano, navyo vya katikati upana wao mikono sita, navyo vya juu upana wao mikono saba. Kwani nje kuta zilipunguka kuwa zenye vipago kuizunguka nyumba yote, kusudi boriti zao hivyo vyumba visishikamane na nyumba yenyewe mle kutani ndani.

7Hapo, nyumba ilipojengwa, ikajengwa kwa mawe yaliyokwisha kuchongwa yalipovunjwa; mahali hapo, nyumba ilipojengwa, hapakusikilika nyundo wala shoka wala chombo cho chote cha chuma.

8Mlango wa vyumba vya ubavuni ulikuwa katikati upande wa kulia wa nyumba; wakapanda kwa ngazi iliyojipinda kufikia vyumba vya katikati, vivyo hivyo kuvitoka vyumba vya katikati kuvifikia vile vya juu.

9Alipokwisha kuijenga hiyo nyumba akaipamba na kutumia boriti na mbao za miangati.

10Navyo vile vyumba vya ubavuni vya nyumba yote nzima akavijenga kuwa vyenye urefu wa kwenda juu mikono mitano, navyo vikashikamana na nyumba yenyewe kwa boriti za miangati.

11Neno la Bwana likamjia Salomo la kwamba:

12Kwa hivyo, unavyoijenga nyumba hii, utakapoendelea katika maongozi yangu na kuyafanya maamuzi yangu na kuyaangalia maagizo yangu yote, uyafuate, ndipo, nitakapolitimiza kwako neno langu, nililomwambia baba yako Dawidi:[#2 Sam. 7:13.]

13Nitakaa katikati yao wana wa Isiraeli, nisiwaache walio ukoo wangu wa Waisiraeli.[#2 Mose 29:45.]

14Salomo alipokwisha kuijenga hiyo nyumba na kuimaliza,[#Tume. 7:47.]

15akazitia kuta za hiyo nyumba upande wa nyumbani mbao za miangati; kuanzia chini penye msingi wa nyumba mpaka juu penye boriti, akazifunika kuta za nyumbani kwa mbao, hata chini nyumbani pa kukanyagia akapafunika kwa mbao za mivinje.

16Kisha akajenga chumba mle nyumbani upande wa nyuma urefu wa mikono 20 kwa mbao za miangati kuanzia chini mpaka juu ukutani; ndivyo, alivyojenga mle nyumbani chumba cha nyuma kuwa Patakatifu Penyewe.

17Lakini chumba kilichokuwa mbele yake kilikuwa cha mikono 40, nacho ndicho chumba cha Patakatifu.

18Hivyo upande wa ndani wa hiyo nyumba ulikuwa miangati tu yenye urembo wa mifano ya matango na ya maua yachanukayo; po pote ni miangati, mawe hayakuonekana.

19Nacho chumba cha nyuma mle ndani nyumbani alikitengeneza cha kuwekea humo Sanduku la Agano la Bwana.

20Hicho chumba cha nyuma urefu wake wa kwenda mbele ulikuwa mikono 20, nao upana wake mikono 20, nao urefu wake wa kwenda juu mikono 20, akakifunikiza chote dhahabu zilizong'azwa. Nayo meza ya kutambikia akaifunikiza kwa mbao za miangati.

21Upande wa ndani wa hiyo nyumba Salomo akaufunikiza dhahabu zilizong'azwa, akapitisha mbele ya chumba cha nyuma minyororo ya dhahabu, nacho akakifunikiza dhahabu.

22Hivyo nyumba yote akaifunikiza dhahabu, akaimaliza nyumba yote nzima hivyo, nayo meza ya kutambikia iliyokuwa mbele ya chumba cha nyuma akaifunikiza dhahabu.

23Mle ndani ya chumba cha nyuma akatengeneza Makerubi mawili ya miti ya michekele, urefu wao wa kwenda juu ulikuwa mikono kumi.[#2 Mose 37:7-9.]

24Kila bawa moja la Kerubi lilikuwa mikono mitano, nalo bawa la pili la Kerubi lilikuwa mikono mitano, ikawa mikono kumi kutoka pembe ya bawa lake moja mpaka pembe ya bawa lake jingine.

25Vilevile Kerubi la pili lilikuwa lenye mikono kumi; Makerubi yote mawili yalikuwa yenye kipimo kimoja na yenye sura moja.

26Urefu wa kwenda juu wa Kerubi moja ulikuwa mikono kumi, nalo Kerubi la pili lilikuwa vivyo hivyo.

27Akayaweka haya Makerubi katikati ya chumba cha ndani, yakiwa yameyakunjua mabawa yao, bawa la moja liligusa ukuta, nalo bawa lake lile la pili liligusa ukuta wa pili, nayo mabawa yao yaliyoelekea upande wa nyumbani kati yaligusana bawa kwa bawa.

28Haya Makerubi akayafunikiza dhahabu.

29Namo katika kuta zote za nyumbani katika chumba cha ndani na cha nje akachora machoro ya mifano ya Makerubi na ya mitende na ya maua yachanukayo.

30Napo pa kukanyagia nyumbani chini akapafunikiza dhahabu katika chumba cha ndani na cha nje.

31Tena pa kukiingilia chumba cha ndani akatengeneza lango lenye milango miwili ya mbao za michekele, vizingiti na miimo ilikuwa yenye miraba mitano.

32Namo katika hiyo milango miwili ya mbao za michekele akachora machoro ya Makerubi na ya mitende na ya maua yachanukayo, kisha akaifunikiza dhahabu; hizo dhahabu za kuyafunikiza Makerubi na mitende zilikuwa zimesanwa.

33Vivyo hivyo hata penye kukiingilia chumba kitakatifu akatengeneza miimo ya miti ya michekele yenye miraba minne,

34na milango miwili ya mbao za mivinje, mlango mmoja ukipata kugeuka pande mbili, nao mlango wa pili uligeuka pande mbili.

35Akachora namo humo Makerubi na mitende na maua yachanukayo, akaifunikiza dhahabu zilizopatanishwa kuwa sawa na yale machoro.

36Kisha akaujengea ua wa ndani ukuta wenye safu tatu za mawe ya kuchonga na safu moja ya boriti za miangati.

37Katika mwaka wa nne msingi wa nyumba ya Bwana uliwekwa katika mwezi wa Ziwu.[#1 Fal. 6:1.]

38Katika mwaka wa kumi na moja katika mwezi wa Buli, ndio mwezi wa nane, nyumba ikamalizika pande zake zote, kama ilivyopasa; basi, ilikuwa miaka saba, aliyoijenga.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania