1 Samweli 18

Yonatani anafanya urafiki na Dawidi.

1Ikawa, alipokwisha kusema na Sauli, roho yake Yonatani ikafungamana na roho yake Dawidi, Yonatani akampenda, kama alivyojipenda.

2Naye Sauli akamchukua Dawidi siku hiyo, hakumpa ruhusa tena kurudi nyumbani mwa baba yake.[#1 Sam. 16:22; 17:15.]

3Ndipo, Yonatani na Dawidi walipofanya urafiki wa uchale, kwa kuwa alimpenda, kama alivyojipenda.[#1 Sam. 19:1; 20:17; 23:18; 2 Sam. 1:26; 21:7.]

4Yonatani akaivua kanzu, aliyokuwa ameivaa, akampa Dawidi pamoja na mavazi yake ya vitani na upanga wake na upindi wake na mkanda wake.

5Po pote, Sauli alipomtuma, Dawidi akaenda na kuyamaliza kwa werevu yale aliyotumwa; kwa hiyo Sauli akamweka kuwa mkuu wa askari, vikawapendeza watu wote, hata watumishi wa Sauli.[#1 Sam. 18:14.]

Sauli anamwonea Dawidi wivu.

6Ikawa, Dawidi aliporudi akiisha kumwua yule Mfilisti, wanawake wakatoka katika mji yote ya Waisiraeli kumwendea mfalme Sauli wakiimba na kuchezacheza na kupiga patu na vigelegele na matoazi.[#Amu. 11:34.]

7Hao wanawake wakaitikiana katika kuimba kwao kwamba:

Sauli ameua elfu lake, lakini Dawidi ameua maelfu yake kumi!

8Makali ya Sauli yakawaka moto sana, wimbo huo ukawa mbaya masikioni mwake, akasema: Dawidi wamempa maelfu kumi, lakini mimi wamenipa elfu tu. Hivyo itakuwa, ufalme nao uwe wake.

9Siku hiyo ndipo, Sauli alipoanzia kumnunia Dawidi.

10Kesho yake ile roho mbaya ya Mungu ikampagaa Sauli, akawa nyumbani mwake kama mwenye wazimu akipayukapayuka, lakini Dawidi akampigia zeze kwa mkono wake, kama alivyozoea siku zote, naye Sauli akawa akishika mkuki mkononi mwake.[#1 Sam. 16:14.]

11Mara Sauli akautupa mkuki akisema: Na nimchome Dawidi ukutani! Lakini Dawidi akajiepusha mbele yake mara mbili.[#1 Sam. 19:10; 20:33.]

12Sauli akamwogopa Dawidi, kwa kuwa Bwana alikuwa naye, nako kwake Sauli alikuwa ameondoka.

13Kwa hiyo Sauli akamwondoa nyumbani mwake, akamweka kuwa mkuu wa askari elfu; ndipo, alipotoka, akaja kuwaongoza hao watu.

14Naye Dawidi akazifuata kwa werevu njia zote, alizozishika, kwani Bwana alikuwa naye.[#1 Sam. 18:5.]

15Sauli alipoona, ya kuwa ni mwenye werevu sana, akazidi kumwogopa.

16Nao Waisiraeli na Wayuda wote wakampenda Dawidi, kwani alikuwa akiwatangulia kwenda na kurudi vitani

Sauli anamwoza Dawidi mwanawe Mikali.

17Sauli akamwambia Dawidi: Tazama, na nikupe mwanangu mkubwa Merabu, awe mkeo. Ila neno moja tu: Sharti uwe fundi wangu wa vita, umpigie Bwana vita. Maana Sauli alisema moyoni: Mkono wangu usimjie, ila mikono ya Wafilisti na imjie.

18Dawidi akamjibu Sauli: Mimi ni nani? Nayo mambo yangu ya kujitunza ni ya namna gani? Nao ukoo wa baba yangu una ukuu gani kwao Waisiraeli, mimi nipate kuwa mkwe wa mfalme?

19Lakini siku zilipotimia za kumpa Dawidi Merabu, binti Sauli, akaolewa na Adirieli wa Mehola.[#Amu. 15:2.]

20Lakini Mikali, binti Sauli, akampenda Dawidi; walipomsimulia Sauli, jambo hili likampendeza machoni pake,

21maana naye Sauli alikuwa amesema moyoni: Huyu ndiye, nitakayempa, amnase, mikono ya Wafilisti ipate kumjia. Kwa hiyo Sauli akamwambia Dawidi: Leo utakuwa mkwe wangu kwa kumwoa wa pili.

22Kisha Sauli akawaagiza watumishi wake: Semeni njama na Dawidi kwamba: Tazama! Mfalme amependezwa na wewe, nao watumishi wake wote wanakupenda. Sasa sharti uwe mkwewe mfalme.[#1 Sam. 22:14.]

23Watumishi wa Sauli walipoyasema maneno haya masikioni pa Dawidi, Dawidi akawauliza: Ni neno dogo gani kuwa mkwewe mfalme? Nami ni mtu akosaye mali na macheo.

24Kisha watumishi wa Sauli wakampasha habari za kwamba: Maneno kama hayo ndiyo, Dawidi aliyoyasema.

25Ndipo, Sauli aliposema: Mwambieni Dawidi haya: mfalme hataki mali nyingine za ukwe, anataka tu magovi mia za Wafilisti, ajilipize kwao hao adui za mfalme. Lakini Sauli alifikiri moyoni njia ya kumtia Dawidi mikononi mwa Wafilisti.

26Watumishi wa Sauli walipomsimulia Dawidi maneno hayo, jambo hili likampendeza Dawidi kuwa njia ya kuwa mkwewe mfalme. Siku zilipokuwa hazijatimia bado,

27Dawidi akaondoka, akaenda yeye na watu wake, akaua kwao Wafilisti watu 200; kisha akayapeleka magovi yao, akampa mfalme na kumhesabia yote pia, apate kuwa mkwewe mfalme. Ndipo, Sauli alipompa mwanawe Mikali, awe mkewe.

28Sauli akayaona, akayajua, ya kuwa Bwana yuko pamoja na Dawidi; naye Mikali, binti Sauli, akampenda.

29Ndipo, Sauli alipoendelea kumwogopa Dawidi zaidi, kwa hiyo Sauli akawa mchukivu wake Dawidi siku zote.[#1 Sam. 18:12.]

30Ikawa kila mara, wakuu wa Wafilisti walipotoka, Dawidi akawaendea kwa werevu zaidi kuliko watumishi wa Sauli, kwa hiyo jina lake likatukuzwa sana.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania