Danieli 1

Danieli na wenziwe watatu wanafunzwa nyumbani mwa mfalme wa Babeli.

1Katika mwaka wa tatu wa ufalme wa Yoyakimu, mfalme wa Yuda, Nebukadinesari, mfalme wa Babeli, alikuja Yerusalemu, akausonga.[#2 Fal. 24:1-2.]

2Bwana akamtia Yoyakimu, mfalme wa Yuda, mkononi mwake, hata vyombo vinginevyo vya Nyumbani mwa Mungu akavipeleka katika nchi ya Sinari nyumbani mwa miungu yake, kisha akavipeleka hivyo vyombo katika nyumba ya vilimbiko vya miungu yake.

3Mfalme akamwambia Asipenazi aliyekuwa mkuu wa watumishi wake wa nyumbani, alete wana wa Kiisiraeli walio wa uzao wa kifalme na wa watu wenye macheo;[#2 Fal. 20:18.]

4achague wavulana wasio na kilema cho chote, wenye miili mizuri ya kupendeza, wenye ubingwa na ujuzi wote, wenye akili za kujua na za kutambua wanayoelezwa, wenye nguvu za kutumikia jumbani mwa mfalme, apate kuwafundisha maandiko na maneno ya Wakasidi.

5Mfalme akawaagizia siku ya siku vilaji vya urembo, yeye mfalme alivyovila, hata mvinyo, alizozinywa; akataka, wafugwe hivyo miaka mitatu, kisha wamtumikie mfalme.

6Katika hao wana wa Kiyuda walikuwamo Danieli na Hanania na Misaeli na Azaria.

7Naye mkuu wa watumishi wa nyumbani akawapa majina mengine: Danieli akamwita Beltesasari, naye Hanania akamwita Sadiraki, naye Misaeli akamwita Mesaki, naye Azaria akamwita Abedi-Nego.

8Lakini Danieli alisema moyoni mwake: Sitajipatia uchafu nikila vilaji vya urembo vya mfalme au nikinywa mvinyo zake; akamwomba mkuu wa watumishi wa nyumbani ruhusa, asijipatie uchafu hivyo.[#3 Mose 11.]

9Mungu akampatia Daniel upendeleo na utu mbele yake mkuu wa watumishi wa nyumbani.[#1 Mose 39:21.]

10Naye mkuu wa watumishi wa nyumbani akamjibu Danieli: Mimi ninamwogopa bwana wangu mfalme, aniagiziaye vilaji na vinywaji vyenu; kama angewaona ninyi, ya kuwa nyuso zenu zinanuna kuliko zao vijana wengine walio rika moja nanyi, basi, mtakuwa mmeniponza kwake mfalme, akanikata kichwa.

11Ndipo, Danieli aliposema na mtunza mvinyo, maana ndiye, mkuu wa watumishi wa nyumbani aliyemweka kuwasimamia akina Danieli na Hanania na Misaeli na Azaria, akamwambia:

12Tafadhali utujaribu sisi watumwa wako siku kumi tu, tupate maboga tu ya kula na maji tu ya kunywa!

13Kisha tutazamwe mbele yako, tulivyo, nao vijana wanaokula vilaji vya urembo vya mfalme watazamwe nao, walivyo. Kama utakavyoona, basi, ndivyo, utakavyotufanyizia sisi watumwa wako.

14Akawaitikia neno hili, akawajaribu siku kumi.

15Siku kumi zilipokwisha pita, wakatazamwa, wakaonekana kuwa wema, nayo miili yao ilikuwa imenona kuliko vijana wote waliovila vilaji vya urembo vya mfalme.

16Ndipo, mtunza mvinyo alipoviacha vile vilaji vya urembo na mvinyo, walizopewa za kunywa, akawapa maboga tu.

17Naye Mungu akawapa hawa vijana wanne akili za kujifunza ujuzi wote uliokuwamo katika vitabu, naye Danieli akampa kutambua maono na ndoto zote.[#Ez. 28:3.]

18Siku zilipokwisha pita, mfalme alizoziweka za kuwapeleka kwake, mkuu wa watumishi wa nyumbani akawapeleka kwake Nebukadinesari.

19Mfalme alipoongea nao, kwao wote hakuoneka aliyefanana nao akina Daniel na Hanania na Misaeli na Azaria; kwa hiyo wakapewa kumtumikia mfalme.

20Katika mambo yote ya ujuzi wa kutambua neno, mfalme aliyowauliza, akawaona, ya kuwa wanawashinda mara kumi waandishi na waaguaji wote waliokuwako katika ufalme wake.

21Danieli akawapo hata mwaka wa kwanza wa mfalme Kiro.[#Ezr. 1:1.]

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania