Danieli 8

Ndoto nyingine ya Danieli ya wafalme wanne.

1Katika mwaka wa tatu wa mfalme Belsasari mimi Danieli nikatokewa na ndoto, ile ya kwanza ilipokwisha kunitokea.

2Yako, niliyoyaona katika hiyo ndoto; napo hapo, nilipoyaona, nilikuwa katika mji wa kifalme wa Susani ulioko katika jimbo la Elamu. Nami nilipoyaona katika hiyo ndoto nilikuwa kwenye mto wa Ulai.

3Nilipoyainua macho yangu, nitazame, mara nikaona dume moja la kondoo aliyesimama hapo penye mto, naye alikuwa na pembe mbili, nazo hizo pembe zilikuwa ndefu, tena moja ilikuwa ndefu kuliko ya pili, nayo hiyo ndefu ndiyo iliyotokea mwisho.

4Nikamwona huyo dume la kondoo, alivyorukia upande wa baharini na wa kaskazini na wa kusini, tena hakuwako nyama yeyote aliyeweza kusimama mbele yake, wala hakuwako aliyeweza kuokoa mkononi mwake, akafanya yaliyompendeza kwa kujikuza.

5Nilipokuwa sijamtambua vema, mara nikaona dume la mbuzi aliyetoka machweoni kwa jua, akapita juu ya nchi yote nzima pasipo kugusa mchanga wa chini kwa miguu; huyo dume la mbuzi alikuwa na pembe kubwa mno katikati ya macho yake.

6Akamjia yule dume la kondoo, mwenye pembe mbili, niliyemwona, akisimama penye mto, akamkimbilia kwa makali ya nguvu zake.

7Nikamwona, alivyomfikia yule dume la kondoo, akamrukia kwa ukali mwenye uchungu, akampiga yule dume la kondoo, akazivunja pembe zake mbili, naye dume la kondoo hakuwa na nguvu ya kusimama mbele yake, kwa hiyo akambwaga chini, akamkanyagakanyaga, tena hakuwako aliyemwokoa yule dume la kondoo mkononi mwake.

8Kisha dume la mbuzi akajikuza kabisa; nguvu zake zilipozidi, ndipo, pembe yake kubwa ilipovunjika, mahali pake pakatokea nyingine nne kubwa mno, zikazielekea pande nne za upepo wa mbinguni.[#Dan. 7:6; 11:4.]

9Kwao hizo katika moja ikatoka pembe moja ndogo, ikakua sanasana, ikaelekea upande wa kusini na wa maawioni kwa jua na wa ile nchi yenye utukufu.[#Dan. 7:8; 11:16.]

10Ikakua kufika kwenye kikosi cha mbinguni, vinginevyo vya hicho kikosi ikavibwaga chini nazo nyota mojamoja, ikaziponda kwa kuzikanyagakanyaga.

11Kisha ikajikuza, imshinde naye Mkuu wa hicho kikosi, kwa hiyo akanyimwa matambiko yake ya kila siku, nalo Kao lake takatifu likaachwa.[#Dan. 11:31.]

12Nacho hicho kikosi kikatolewa pamoja na yale matambiko kwa kupotolewa; nayo mambo ya kweli ikayatupa chini, hivyo yakaendelea iliyoyafanya.

13Ndipo, niliposikia, mtakatifu mmoja akisema: mtakatifu mwingine akamwuliza yuyo huyo aliyesema: Mambo ya hili ono yatakuwa mpaka lini? Hayo ya matambiko ya kila siku na ya mapotovu yanayoangamiza? Nayo yale ya kukitoa Kikao kitakatifu nacho kikosi, vikanyagwekanyagwe?

14Akaniambia: Mpaka zipite 2300 za kuchwa na kucha; ndipo, Patakatifu patakapoyapata yapapasayo.

15Mimi Danieli nilipoiona ndoto hii nikatafuta njia ya kuitambua. Mara nikaona aliyesimama mbele yangu mwenye mwili wa kimtu.

16Nikasikia sauti ya mtu iliyotoka katika mto wa Ulai, ikaita kwamba: Gaburieli, mtambulishe mtu huyu aliyoyaona![#Dan. 9:21.]

17Akaja huko, nilikosimama; lakini alipokuja, nikastuka, nikaanguka kifudifudi, akaniambia: Tambua, mwana wa mtu, ya kuwa hilo ono linaonyesha yatakayokuwa siku za mwisho![#Dan. 10:9.]

18Aliposema nami, nikashikwa na usingizi kabisa, nao uso wangu ukaelekea chini, akanigusa, akanisimamisha tena hapo, nilipokuwa nimesimama,

19akasema: Tazama, mimi nitakujulisha yatakayokuwa penye mwisho wa makali haya, kwani hayo yanayaelekea yale ya mwisho.

20Dume la kondoo, uliyemwona mwenye pembe mbili, ndio wafalme wa Wamedi na wa Wapersia.

21Naye dume la mbuzi mwenye manyoya mengi ni mfalme wa Wagriki, nayo ile pembe kubwa iliyokuwa katikati ya macho yake ni mfalme wa kwanza.

22Tena ikivunjika, mahali pake zikitoka nyingine nne, ni kwamba: Nchi za kifalme nne zitatoka katika taifa lake, lakini hazitakuwa na nguvu yake yeye.

23Penye mwisho wa ufalme wao, wapotovu watakapoyatimiza mapotovu yao, patainuka mfalme mwenye uso mkali atambuaye mizungu mibaya.[#Dan. 11:21.]

24Nguvu zake zitazidi, lakini si kwa nguvu zake yeye; atafanya vioja vibaya vya kuangamiza, tena atakapovifanya atafanikiwa, awaangamize wenye nguvu nao ukoo wao watakatifu.

25Kwa werevu wake atayaendesha madanganyo yaliyomo mkononi mwake, atajikuza moyoni mwake, aangamize wengi kwa kuwajia kwa upole. Lakini atakaposimama, ampingie naye aliye Mkuu wa wakuu, ndipo, atakapovunjwa pasipo kukamatwa kwa mikono

26Nayo, uliyoyaona ya kuchwa na kucha na kuambiwa habari zao, ni ya kweli. Lakini wewe iandike ndoto hii, kisha iweke kifichoni, kwani ni ya mambo ya siku nyingi.[#Dan. 12:4.]

27Kisha mimi Danieli nikazimia, nikawa mgonjwa siku hizo; kisha nikaondoka kitandani, nikafanya kazi ya kumtumikia mfalame. Lakini nikahangaika sana kwa ajili yao hayo, niliyoyaona, lakini hakuwako aliyenitambua.

Swahili Roehl Bible 1937 © Bible Society of Tanzania, 1937.
Published by: Bible Society of Tanzania